SIRI YA KUPATA MTAJI WA BIASHARA KIRAHISI KWA MJASIRIAMALI MDOGO ASIYE NA DHAMANA MJINI NA KIJIJINI | Jifunzeujasiriamali

SIRI YA KUPATA MTAJI WA BIASHARA KIRAHISI KWA MJASIRIAMALI MDOGO ASIYE NA DHAMANA MJINI NA KIJIJINI

Mtaji wa biashara mjini na kijijini

Hakuna Jinsi Mjasiriamali mdogo masikini anavyoweza kupata mtaji wa uhakika wa biashara ya ndoto yake zaidi ya kutumia Akili, Ubunifu na Nguvu zake mwenyewe kwanza kwenye hatua za awali za biashara 

Kuna dhana ya siku nyingi kwamba tatizo la wajasiriamali wengi masikini siyo mtaji bali ni ukosefu wa mawazo bora ya biashara zinazolipa jambo linalowafanya washindwe kupata mafanikio ya kiuchumi wanayotamani

Lakini hata pale wanapojitahidi kutafuta mawazo mazuri ya biashara zinazolipa bado wanashindwa kutoboa kwa urahisi na wengi wanaendelea tu kubakia kwenye mzunguko uleule wa umasikini miaka nenda miaka rudi

Ukweli ni kwamba mtaji wa kwanza kabisa katika biashara yeyote ile duniani siyo pesa bali ni akili ya mtu kichwani mwake kwa kuona matatizo na fursa mbalimbali kisha kufikiria mbinu na mikakati sahihi ya kuyatatua kwa njia itakayomletea faida kiuchumi

Hata hivyo kufikiria kichwani tu peke yake hakutoshi bado, kunamhitaji mjasiriamali kuchukua hatua ya kuwekeza nguvu, muda na rasilimali nyingine alizokuwa nazo ili wazo lake liweze kumletea faida

Katika hatua hizo za mwanzo haiwezekani mtu kutajirika au kupata mafanikio ya maana, zinahitajika bado juhudi nyingi, ubunifu, mbinu na mikakati mbalimbali

Kitu wajasiriamali wengi wanacholalamika kuwa kimekuwa kikwazo kikubwa kwao licha ya kuwa na mawazo mazuri mno ya biashara vichwani ni MTAJI, na mtaji si ule wa kuanza tu bali ni mtaji wa kuendeleza au ‘kuboost’ biashara zao pindi zinapotaka kutoka katika ile hatua ya unyonge ya awali

Unakuta mtu anaanzisha biashara vizuri tu yenye faida lakini kabla hata haijaanza kuleta matunda inakufa shauri ya kukosa mzunguko chanya+ wa kutosha wa fedha. Kinachoua biashara nyingi siyo ukosefu wa wateja bali mzunguko mdogo wa fedha

Wachache wanaofanikiwa aidha wana bahati ya kupata mitaji mahali pengine ya kuongezea au hutumia mbinu ya kujibana sana na kurudisha faida wanayoipata kwenye mitaji yao

Mbinu hii ya kujibana na kurudisha faida kwenye mtaji ingawa ni nzuri sana na ya uhakika lakini ina changamoto zake kubwa kwani wajasiriamali wengi masikini hutegemea moja kwa moja vipato vyao vidogo katika matumizi ya kawaida ya kujikimu kimaisha na hawana kabisa njia ya kulikwepa hili

Na mbaya zaidi ni pale kunapojitokeza dharura za kimaisha zisizoweza kuepukika kirahisi mfano magonjwa, vifo na majanga mengine mbalimbali ya kimaisha na kukuta hakuna njia nyingine ya kuyatatua zaidi ya kutumia fedha kidogo zilizokuwepo kwenye mzunguko wa biashara

Katika hali ngumu kama hizo ni vigumu sana kumwambia mjasiriamali mdogo atenganishe fedha za biashara na zile za matumizi yake binafsi – kanuni muhimu sana kwenye biashara

Kumbuka faida anayoipata kwenye biashara bado ni kidogo kutokana na mtaji pia nao kuwa ni mdogo mno halafu anahitaji kutumia mtaji huohuo kutatulia shida za kila siku za maisha zinazomkabili

Suluhisho la tatizo hili ikiwa biashara ina uwezo wa kutengeneza faida kubwa ingeliweza kuwa ni kukopa mahali licha ya hatari za riba na kushindwa marejesho lakini bado kwa mjasiriamali mdogo masikini anakabiliwa na kikwazo kingine kikubwa zaidi cha DHAMANA, masikini hakopesheki kirahisi iwe ni katika taasisi rasmi za kifedha au kwa ndugu, jamaa na marafiki

Unaijua siri ya Mikopo?

Wakopeshaji wakishagundua tayari umesimamisha biashara yenye mifumo yote muhimu kwa kutumia nguvu zako mwenyewe hujileta wenyewe kwako kirahisi wala huhitaji juhudi za kuwatafua

Sasa ni nini hasa suluhisho la vikwazo vyoote hivi na kukataliwa kila kona kwa mjasiriamali masikini asiye na dhamana za uhakika?

Jibu ni kutumia mbinu, mikakati na ubunifu kwenye biashara hizohizo ndogo zizalishe faida kubwa kwa haraka zaidi kuliko vile ambavyo mjasiriamali anatumia faida hiyo kwenye matumizi yake ya kujikimu kimaisha (kujilipa gawio) maana ndio njia yake kuu ya kupata mahitaji ya kila siku vinginevyo hataweza kuishi

Mahitaji ya msingi sana kwa binadamu ni chakula, malazi na mavazi. Vitu hivi ni lazima avipate piga ua, iwe ni kwa kutumia fedha za mshahara, ruzuku au faida ya biashara anayoifanya

Kumzuia asiyapate kabisa mahitaji hayo biashara au kazi anayofanya haina maana yeyote kwake na ndiyo sababu wajasiriamali wengi masikini hawawezi kamwe kukuelewa unapowaambia juu ya kuweka akiba wakati hawana kipato cha kujikimu na mahitaji hayo ya kila siku – kanuni nyingine tena muhimu zaidi kwenye biashara

Kuna njia kuu mbili (2) za kuifanya miradi / biashara ndogo zizalishe faida/mapato makubwa haraka kuliko matumizi ya mjasiriamali ya msingi

1.   Kuchagua biashara / miradi ambayo moja kwa moja ina sifa za kutengeneza faida kubwa kwa muda mfupi

2.   Kutumia mbinu na mikakati ya kiubunifu kuufanya mradi wowote ule wa kawaida kuwa ni wenye faida kubwa na ya haraka

Kumbuka ninaposema FAIDA KUBWA NA YA HARAKA simaanishi miradi ile ya kitapeli (Pyramid schemes) hapana, namaaanisha miradi hii hii ya ukweli ya kawaida tunayoifanya kila siku 

Na pia simaanishi kwamba miradi hii unaifanya leo ukilala usiku mmoja tu kesho yake unaamka tajiri hapana, inahitaji muda kamili mfano ikiwa kama mchicha unahitaji siku 21 ukomae ndipo uuze, unahitaji kweli kusubiria siku hizo 21 na siyo blaa blaa za kudanganyana eti mchicha siku 10 tu unavuna! hiyo hapana

Inawezekana mtu akachagua mbinu moja kati ya hizo mbili nilizozitaja hapo juu au akachanganya mbinu zote 2 kwa mara moja kupata matokeo makubwa na ya uhakika zaidi

Lakini bado mjasiriamali anaweza akajiuliza hivi;- “hizo mbinu zipoje na zinatumika-tumika vipi ili kumpatia mtu faida kubwa haraka kuliko matumizi yake ya kawaida?

Kulijibu swali hili sitatumia maneno ya nadharia bali mifano hai ya biashara ambazo mimi binafsi nazifanya/nimezifanya na watu wengine pia wanazifanya, na uzuri zaidi ni kwamba nimeanzisha madarasa halisi ya mfano kama Mashamba darasa mtu yeyote anaweza kukopi na kupaste mbinu halisi zinazotumika bila kufanya majaribio tena (Trial & error)

Biashara/Miradi michache nitakayoitaja hapa inawakilisha biashara na miradi mingine mingi mtu yeyote anaweza akaanzisha, kikubwa tu ni ubunifu, mbinu na mikakati inayotumika kuifanikisha

Kwa wajasiriamali wa Mijini na Majiji makubwa

Simaanishi biashara hizi mtu wa kijijini hawezi kuzifanya hapana bali namaanisha hufanywa zaidi na watu waishio mijini kuliko vijijini. Hii ni biashara ya REJAREJA aina yeyote ijapokuwa mimi nimetumia Duka la rejareja maalumu kuwakilisha biashara nyingine zote za rejareja

Mjasiriamali yeyote yule mdogo wa mjini mara nyingi kimbilio lake la kwanza ni biashara ya rejareja kutokana na asili/nature ya mtaji wake mdogo, ni dadra sana kufikiria biashara ya jumla

Biashara ya Duka la Rejarja yenyewe kama biashara huwezi ukasema ni biashara yenye ile sifa niliyoitaja pale juu ya kuzalisha faida haraka ndani ya kipindi kifupi hapana, inategemea eneo na vigezo vingine vingi kama mtaji nk, lakini mimi kwa kesi yangu hapa utaona nilitumia ubunifu, mbinu na mikakati ya kipekee kuifanya biashara hii kutoa matokeo yale niliyokusudia kuyapata yaani faida kubwa ndani ya kipindi kifupi kwa kadiri ilivyowezekana

Kwa kutumia mfano hai wakwangu mwenyewe nimeeleza na kuonyesha jisi nilivyofanikiwa kuanzisha biashara ya duka la rejareja lenye wasaidizi 2 nikiwa sina hata mia mfukoni ndani ya kipindi cha miezi 12 tu Kariakoo. Mbinu, ubunifu na mikakati niliyoitumia mtu mwingine yeyote yule anaweza akaikopi na kuitumia kama ilivyo mahali pengine popote pale hata kama ikiwa siyo Kariakoo

Wajasiriamali wadogo waishio mijini na majiji makubwa tayari nimemalizana nao kwenye kitabu changu chenye kurasa 334 kiitwacho “MAFANIKIO YA BIASHARA YA DUKA LA REJAREJA- NEW TECH EDITON”. Najua wengi wanafahamu kile cha kurasa 176 toleo la zamani ambacho kinakosa mambo mengi mapya

Gharama ya kitabu hiki softcopy ni sh. 15,000/= lakini kuna offa ya muda mfupi ya sh. 10,000/= Kukipata muda huu huu popote kwenye simu au kompyuta yako kwa bei ya offa ya sh. elfu 10 malipo ni kupitia namba, 0761002125 jina Peter Augusino Tarimo, kisha nitakutumia kiungo cha kupakua kitabu chako na coupon ya offa muda huohuo

Lakini pia ukitaka kukinunua moja kwa moja mtandao wa Selar kwa bei ya kawaida ya sh. elfu 15 bofya kiungo kifuatacho; SIRI YA MAFANIKIO YA BIASHARA YA DUKA LA REJAREJA -NEWTECH EDITION 2026

 

Kwa wajasiriamali wa Vijijini na Nje kidogo ya Miji & Majiji

Miradi hii simaanishi ni ya watu wa vijijini tu hapana, bali ni miradi ambayo hufanywa zaidi na watu waishio vijijini kulingana na asili/nature yake lakini hata waishio mijini na nje kidogo ya majiji makubwa pia wanaweza wakaifanya kukuza mitaji ya biashara za ndoto zao

Nimefanya tafiti kwa ajili ya miradi mingi ya kilimo na ufugaji ndani ya kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja (tangu Agosti mwaka jana mpaka sasa) na tayari ninayo miradi/biashara 3 za mfano ambazo nipo tayari kuzishea kwa yeyote anayehitaji kuiga/kukopi ubunifu, mbinu na mikakati niliyoitumia kuzifanya biashara hizo ziweze kutengeneza mtaji haraka

Kuthibitisha ukweli na uhalali wa mbinu hizi yeyote anayetaka kujifunza hatajifunza kwa nadharia zilizozoeleka bali kupitia darasa maalumu la vitendo ambalo mimi mwenyewe kama mwezeshaji tayari ninayo miradi yangu inayoendelea na mingine mipya itakayokwenda sambamba na ile ya wanafunzi kusudi waweze kujifunza katika wakati halisi (real time)

Nikimaanisha kama shamba la mwalimu nyanya ina mwezi mmoja halikadhalika na shamba la mwanafunzi nalo nyanya ina mwezi mmoja huohuo kusudi aweze kuona ‘live’ mbinu, mikakati na ubunifu unaofanyika na hatimaye faida inavyopatikana

Nimeamua kuanza na shamba-darasa la nyanya, mkakati wangu ni kumfanya mjasiriamali mdogo asiyekuwa na mtaji kabisa au mwenye mtaji kidogo sana aweze kufanya kilimo cha nyanya kipindi cha masika ijayo kuanzia mwezi wa Desemba mwaka huu 2026 mpaka Mei mwakani kutengeneza Mtaji wa biashara ya ndoto yake

Umekaa miaka mingi ukiwaza utapata vipi mtaji kwa ajili ya biashara yako pengine ya kuagiza mzigo kutoka China, kufungua saluni, kufuga kuku kisasa nk. lakini matumaini yanazidi kufifia na wala huoni taasisi / mtu yeyote anayeonyesha dalili za kukukopesha mtaji?. Basi acha kulia suluhisho limepatikana

Zao la nyanya huchukua miezi mitatu tu tangu kuhamishwa kitaluni mpaka mavuno ya kwanza na soko lake ingawa hubadilikabadilika kulingana na msimu lakini ni zao lenye uhakika mkubwa wa soko kwani hakuna binadamu asiyetumia tunda hili kwenye chakula

Kwa kutumia ubunifu, mbinu na mikakati sahihi hasa “timing” ya soko na msimu mkulima anaweza akajitengenezea kiasi kikubwa sana cha fedha ambazo hawezi kuamini kama anaweza kuzipata ndani ya kipindi kifupi hivyo kisichozidi miezi 5

Tayari ninayo mashamba ya nyanya za majaribio niliyokuwa nikifanya na pia kuna mengine naanzisha hivi karibuni kwa ajii ya madarasa, sitaki kujaza nadharia hapa tukutane shambani ikiwa upo tayari kuanza

Kwenye ‘propject’ hii sitaki kabisa mtu anifuatilie kinadharia akisoma post zangu bila vitendo na nimeshasema miradi yangu hii niliyofanyia tafiti zaidi ya mwaka 1 sasa nikitumia gharama kubwa nisingependa iishie hivihivi tu kinadharia, napenda iwanufaishe wajasiriamali masikini nione wakiinuka na kutengeneza biashara za mamilioni waache kusemwa kuwa ni wavivu kisa tu wamekosa mitaji

Hivyo basi ikiwa huna kabisa mtaji au una mtaji kidogo sana ili kwenda sambamba na mimi kwa vitendo kwenye hii project nakuomba ufanye jambo lifuatalo mara baada tu ya kumaliza kusoma hapa;-

Nenda sokoni au gengeni kwa muuzaji wa nyanya muombe MASALO kidogo au nunua hata nyanya za buku ukiweza zilete nyumbani unakoishi, si huna kabisa mtaji wa kununua hata mbegu ya nyanya dukani ya shilingi elfu 5? Sasa hapa ndio utanielewa kwa wewe unayesema huna hata mia ya mtaji wa kuanzia

Kisha kwenye madarasa yangu yatakayofuata huko mbele nitakueleza cha kufanya na hayo masalo au nyanya za buku ulizonunua gengeni

Ninachohitaji hapa ni kukupatia “crash program”-mafunzo maalunu ya haraka maana msimu wa masika tayari unakaribia. Miezi hii kuanzia huu wa Agosti mpaka Desemba nataka tufanye shamba darasa la nyanya live litakalokupa tu uzoefu wa kilimo cha nyanya huku nikikupa na mbinu za kulima nyanya msimu wa masika wenye soko la ‘dhahabu’ kwa zao la nyanya

Hakuna biashara yeyote ile ulimwengu wa leo inayowezekana pasipo kuwekeza mtaji hata kidogo wa nguvu, maarifa na fedha. Miradi hii tangu mwanzo nimetangulia kusema si kwamba hutawekeza chochote hapana, Bali uwekezaji wake ni mdogo lakini mapato ni makubwa sana ukiweza kutumia ubunifu, mbinu na mikakati sahihi iliyofanyiwa majaribio na kuthibitika kufanya kazi

Kwahiyo chochote kile ufanyacho sasa hivi kama shughuli ya kiuchumi inayokuingizia pesa hata ikiwa unapata ruzuku/msaada mahali fulani, rai yangu kwako ni hii- mega hapo kiasi kidogokidogo jiwekee akiba kwa ajili ya mradi wetu huu wa kihistoria wa kimkakati kuanzia Desemaba wa kutengeneza mtaji wa biashara ya ndoto yako, usiniambie eti huingizi chochote, kwani unaishije?

Hata kama wewe ni ombaomba mjini bado kuna kipato cha namna fulani unaingiza na hichohicho ndio ukimege kwa ajili ya maandalizi ya pembejeo za kulima nyanya za msimu wa masika, asikudanganye mtu hakuna mradi usiokuwa na mtaji hata kidogo, nitakuwa nikikupa mbinu na mikakati ya kulifanikisha hili hapa kila siku nifuatilie

Haijalishi upo kijijini au mjini, midhali una ndoto ya kutengeneza mtaji wako mwenyewe wa uhakika inawezekana tu. Kwani hapo mjini ulipo pana umbali gani na maeneo ya nje ya mji unayoweza kufanya kilimo cha nyanya?

Nafahamu majiji yote kuanzia Dar, Arudha, Mwanza na hata Mbeya ukitoka nje kidogo tu ya miji hii kuna maeneo kibao unaweza kukodi shamba au hata kuomba kwa muda ufanye kilimo cha bustani, Panga kuondoka kwa muda hapo unapofanya biashara yako ndogo bila mtaji wa uhakika lakini ukijua kabisa utarudi baada ya miezi michache ukiwa na mtaji wa maana wa kukusongesha mbele haraka zaidi

Ikishindikana basi kwanini usirudi hata kijijini kwako kabisa ulikozaliwa ambapo mashamba ni ya bure kabisa wala hulipi chochote?

Kuendelea kujifariji eti itatokea siku moja upate mtaji wa maana kimiujiza hapo mjini hiyo ni ndoto ya mchana labda tu ikiwa utatumia mbinu na ubunifu niliotumia Kariakoo, ni lazima ukubali kufanya maamuzi magumu leo kwa faida na maslahi ya kizazi chako baadae. Kata huu mnyororo wa umasikini wajukuu zako na vitukuu wasijeteseka kama wewe

Kampeni hii ndio inaanza, kadiri siku zitakavyosonga mbele tutaendelea kujuzana mengine mengi zaidi hapahapa bure bila malipo yeyote lakini ikiwa upo ‘serious’ zaidi unaweza ukajiunga na Shambadarasa langu live kwa uwekezaji wa shilingi elfu 10 kwa msimu wote mpaka mavuno ya nyanya. Kulipia uungwe kwenye kundi muda huu huu namba yangu ni 0761002125 jina Peter Augustino Tarimo

Zipo huduma nyinginezo pia kwa anayehitaji kama vile Michanganuo ya kilimo cha nyanya za masika, kilimo cha nyanya msimu wa kawaida na Muongozo wa Ujenzi wa Greenhouse ya gharama nafuu kwa ajili ya kilimo cha nyanya nyakati za masika na mchanganuo wake

Kwa wajasiriamali waishio mijini au maeneo yenye ufinyu wa ardhi ya kulima hata bustani ndogo tu ya majaribio kuna mbinu maalumu nitawapatia wakati huu wa shamba darasa la majaribio, kipindi kabla ya mvua za masika wakijitayarisha kuhama kwa muda kutoka maeneo yao ya faraja (partial migration from their places of comfort zone) waliyoyazoea

Kumbuka nimetangulia kusema kwamba mjasiriamali hulazimiki kuachana moja kwa moja na biashara yako uhamie jumla kwenye kilimo cha nyanya hapana, bali mradi huu ni wa kimkakati unapaswa kuufanya ukupatie mtaji wa maana kwa ajili ya hiyohiyo biashara yako inayokutesa hapo mjini miaka na miaka pasipo kukua kisa mtaji mdogo

Niamini wewe huna mkosi wala si kweli kwamba hujui biashara bali tatizo lako kubwa ni mtaji finyu, haiwezekani mtaji huohuo ndio uutumie kupanua biashara yako wakati huohuo ukiutumia kwa ajili ya mahitaji yako ya kila siku na mbaya zaidi kama una familia inakutegemea huku ukiwa huna sifa yeyote ile ya kukopesheka, mwishowe ni lazima tu utakufa masikini wala huna haja ya kwenda kwa nabii au mganga kupiga ramli ya kumtafuta mchawi

Mbali na mradi huu wa nyanya za masika, ninayo miradi mingine 3 ya kimkakati mmoja wa kilimo na miwili ya ufugaji ambayo yote nimeshakamilisha utafiti wake wa kina nasubiri tu kuitambulisha kwa wahitaji. Yote ni miradi bunifu iliyo na sifa ama uwezo wa kuzalisha faida kubwa haraka ukitumia mbinu na mikakati sahihi

Hayo ndiyo majibu ya Safari yangu ya mwaka 1+ kijijini kwa wasomaji wa blogu yangu ya Jifunzeujasiriamali mliokuwa mkiniuliza kila mara ikiwa nimeacha kuandika ama la

0 Response to "SIRI YA KUPATA MTAJI WA BIASHARA KIRAHISI KWA MJASIRIAMALI MDOGO ASIYE NA DHAMANA MJINI NA KIJIJINI"

Post a Comment