NINA MTAJI WA MILIONI MOJA YA MKOPO, NIFANYE BIASHARA GANI INAYOLIPA? | JIFUNZE UJASIRIAMALI

NINA MTAJI WA MILIONI MOJA YA MKOPO, NIFANYE BIASHARA GANI INAYOLIPA?


Maswali mengi yanayofanana na hili yamewahi kuulizwa hapa na wadau wengine mbalimbali na siku za nyuma nimewahi pia kutoa  majibu yake katika blogu hii ya jifunzeujasiriamali likiwemo hili la Mtaji wa kuanzisha biashara ya kuuzavochaza simu jumla, million mbili inatosha?

Sababu kubwa iliyonifanya leo kujibu swali lililoulizwa na mdau wetu mmoja ajulikanaye kwa jina la James ni kuwa kuna kitu kimoja cha tofauti nilichokiona katika swali lake hili nacho ni kuwa, ana mtaji wa milioni moja lakini alioipata kwa njia ya mkopo kutoka mahali fulani na anataka auzungushe mtaji huo ndani ya miezi mitatau tu kabla hajatakiwa kuurejesha wote kwa wenyewe.

Maswali mengine mengi niliyokuwa nikiwajibu wadau hapo kabla yali ‘base’ zaidi kwenye mitaji waliyojidundulizia wenyewe kutokana na shughuli zao mbalimbali, zawadi au ruzuku na hakuna wa kuwadai endapo mitaji hiyo ingemezwa kwenye biashara walizotaka kufanya.

Bwana James kupitia njia ya watsap aliuliza kama ifuatavyo, 

“Nina mtaji wa Milioni 1 kwa sasa. Hiyo hela nimekopa kwa miezi 3 riba yake 10% kwa muda huo. Malengo niliyokuwa nimejiwekea  yamekufa hivyo nimebaki na pesa hiyo ambayo natakiwa kuirejesha kwa wausika. Je nifanye nini kwa hiki kipindi kilichobaki kuhakikisha narejesha mkopo, riba pamoja na kupata faida kidogo?” 
  
Majibu kwa swali la Bwana James;
Habari Mr. James na nashukuru kwa kuuliza swali juu ya changamoto ya kimtaji inayokukabili kwa sasa.

Ijapokuwa pesa za mkopo ni chanzo kizuri sana cha mtaji wa kuanzisha na kuendeshea biashara mbalimbali, lakini pia ni vigumu sana kuzitumia fedha za mkopo kuanzishia biashara mpya kabisa tena ambayo wala hukuwa na malengo ya kuifanya muda ulipokuwa ukikopa hizo fedha. Isitoshe pia haishauriwi mahali popote pale Duniani mtu kwenda kukopa kwanza ndipo uje ufikirie biashara ya kufanya na huo mkopo. Kanuni inamtaka kila mkopaji awe na chakufanya kwanza kabla hajainua mguu wake kwenda benki au taasisi yeyote ile ya mkopo.

Kwa mantiki hiyo, fedha za mkopo watu hufanyia biashara ambazo tayari zilishaanza kuzalisha faida, au la basi ikiwa utaamua kuanzishia mradi mpya kabisa, basi uwe tayari unao mradi mwingine kama “back up” ambao utatumika kufanya marejesho ya mkopo endapo itatokea huo mradi mpya umefeli kuzalisha faida ya lulipa marejesho ya mkopo.

Hata hivyo Bwana James ikiwa tayari umejikuta katika situesheni kama hiyo kama ulivyoeleza, basi mimi nakushauri, jitahidi kutafuta walau njia yeyote ile utakayoitumia kujiingizia kipato bila ya kuhatarisha kabisa hiyo hela ya mkopo uliyonayo uhakikishe umelipa kwanza denial watu kasha sasa ndipo uje ujipange mwenyewe upya kwa ajili ya malengo mengine ukiwa hauna deni lolote linalokupa msongo wa mawazo. Ukisha hakikisha sasa una chanzo cha kipato ambacho kina uwezo wa kuzalisha pesa pasipo kutegemea mkopo basi unaweza kwenda kukopa ili kutanua zaidi wigo wa biashara hiyo na kwa kufanya hivyo haitakuwa tena rahisi mtaji wako au mkopo kumezwa katika biashara.

Nikutakie shughuli njema,

Peter Augustino Tarimo.
Mshauri Biashara & Ujasiriamali na Mwanaviwanda 2020
WHATSAPP: 0765553030
SIMU: 0712202244


1 Response to "NINA MTAJI WA MILIONI MOJA YA MKOPO, NIFANYE BIASHARA GANI INAYOLIPA?"

  1. Nikiwa na millioni moja na nusu ila co za mkopo ni zangu binafsi,,,je nifanye biashara gani ambayo inaweza kuniridhisha ndani ya miezi 6?

    ReplyDelete