TULIKOSEA WAPI TANZANIA CORONA IKARUDI TENA KWA KASI HII? | JIFUNZE UJASIRIAMALI

TULIKOSEA WAPI TANZANIA CORONA IKARUDI TENA KWA KASI HII?

Mashine ya kujifukiza
Mnamo tarehe 14/06/2020 katika blog hii niliandika makala moja iliyokuwa na kichwa cha habari;  JINSI YA KUTUMIA MAAJABU YALIYOPUNGUZA CORONA TANZANIA KUBUSTI UCHUMI WAKO UNAOSAMBARATIKA. Katika makala hiyo nilijaribu kwa kadri ya uwezo wangu kuchambua  ni nini hasa kilichotokea mpaka Tanzania ikaweza kujijengea uwezo wa kustaajabisha wa kukaribia kuishinda corona.

Mbinu iliyotumika kwa wakati ule iliweza kufanya kazi vizuri sana lakini mara ghafla tukaja kujikwaa mahali fulani. Pamoja na kujaribu kujadili kile kilichosababisha corona kuibuka tena Tanzania(wimbi la pili la maambukizi ya corona) katika makala hii, lakini mimi lengo langu mahsusi leo si hilo, ila ni kutaka tu kuzidi kukusisitizia juu ya umuhimu wa kutumia mbinu zilizoweza kushinda wimbi la kwanza la Corona Tanzania zilizoasisiwa na viongozi wetu wa nchi hasa Rais wetu Dr. John Pombe Magufuli katika kupambana na kuyashinda matatizo mengine magumu likiwemo lile la mapambano ya kiuchumi kuboresha maisha yetu kifedha.

Ikiwa hukuweza kusoma makala hiyo au hukupata email niliyotuma basi unaweza ukaipata hapa kwenye kiungo kifuatacho, JINSIYA KUTUMIA MAAJABU YALIYOPUNGUZA CORONA TANZANIA KUBUSTI UCHUMI WAKOUNAOSAMBARATIKA. Ikiwa wewe si mpenzi wa maoni, basi unaweza tu kuishia hapa huna sababu ya kuendelea kusoma zaidi makala hii mpaka mwisho.

Sasa hebu tuendelee na mjadala wetu kama utapenda lakini, kwani haya ni maoni yangu tu mimi binafsi kama Peter, nikiamini naandika kwa nia njema kabisa kama mchango wangu kwenye mapambano ya janga hili linaloisumbua Dunia nzima sasa hivi.

Sambamaba na mbinu ile iliyotumika katika wimbi lile la kwanza la ugonjwa wa corona tokea mgojwa wa corona wa kwanza Tanzania kugundulika, kila kiongozi kuanzia Rais wetu Dr. John Pombe Magufuli mpaka Waziri wa Afya wakati huo Mama Ummy Mwalimu, wote walihimiza watu kutumia njia zote za kisayansi na zisizokuwa za kisayansi katika kupambana na janga la corona.

SOMA: Aina nne (4)  za biashara zenye kinga ya majanga vikiwemo virusi vya corona (covid 19)

Tulishuhudia kauli hizo zikitekelezwa kwa vitendo kila mahali kama vile, kuvaa barakoa, kunawa mikono mara kwa mara, matumizi ya vitakasa mikono(sanitizer), kudumisha umbali wa mita moja mtu na mtu, kujifukiza na hata kutumia malimao, vitunguu swaumu, tangawizi na ndimu kwa wingi ilimradi tu kila mtu alichukua tahadhari zote zilizotakiwa.

Lakini chakusikitisha baada tu ya ugonjwa wa corona kudhibitiwa kwa kiasi kikubwa, Watanzania wengi tulisahau na wengine kuachana kabisa na tahadhari zile na ushahidi kila mtu anao mwenyewe, wengine hata tulitupa na kuchoma barakoa, ndoo za maji tukafanya za kufulia nk. tukajidanganya kuwa corona imetoweka Tanzania hivyo hatukuwa tena na haja ya kuchukua tahadhari zilizowekwa na Serikali yetu pamoja na Shirika la Afya Duniani(WHO).

SOMA: Ebola: Tuachane na dawa za kizungu turudi kwenye asili, kikombe cha babu na muarobaini?

Karibu kila mmoja wetu ungemsikia akijisemea; “Mungu wetu ni Mkubwa ametuepusha na corona” bila ya kukumbuka kuwa Dunia yote ni mali ya Mwenyezi Mungu na huwa habagui watu wake kwa Taifa, Dini, wala Kabila mtu atokako, wote hupata magojwa au kupona sawa kama vile ilivyo kwa mvua na jua, tena isitoshe yapo Mataifa mengine athari za ugojwa huu ni kidogo kushinda nchi yetu.

SOMA: Ndege wa ajabu aliyetoweka Duniani ni funzo kubwa kwa biashara zetu kipindi hiki cha janga la corona(covid 19)

Kumbuka tena kuwa wakati Tanzania tukisherehekea kuidhibiti corona kwa kiasi kikubwa, jirani zetu hapo Kenya, Rwanda na Uganda walikuwa bado wakilia na ongezeko la wagojwa kila uchwao wala hatukutilia maanani tena kama kuna kina Mangi kibao waishio Nairobi na Mombasa na pindi ifikapo Krismasi ni lazima “wakahiji” makwao Kilimanjaro.

Ni nani ajuae kama wimbi hili la pili limechangiwa na safari za watu tokea huko mwishoni mwa mwaka 2020?. Kwa kauli za namna hii za kumtupia Mwenyezi Mungu kila majukumu hata yale ambayo tayari amekwishatupa nyenzo na uwezo tayari wa kushughulika nayo, kwakweli hatuwezi kuwa tofauti na ndege Mbuni ambaye huficha kichwa chake mchangani wakati kiwiliwili na makalio vyote vikiwa nje akifikiri anajikinga na hatari. Ni ukweli usipingika kwamba janga hili hakuna binadamu anayeweza akalizuia isipokuwa Mungu mwenyewe kupitia mbinu mbalimbali alizotujaalia.

SOMA: Mbinu na mikakati ya kuikwamua biashara yako kwenye hali ngumu kipesa

Tumeweza kuona hata huko Marekani baadhi ya wachambuzi wanasema moja ya sababu kubwa zilizomfanya Rais Trump kushindwa Urais (ingawa pia kuna sababu nyinginezo)  ilikuwa ni hasira za wananchi wale walioonja machungu ya corona kwa namna moja ama nyingine wakajikuta wakielekeza hasira zao hizo kwa utawala wa nchi bila ya kujua kwamba janga hili hata angelikuwa rais Malaika asingeliweza kulishughulikia  kama ilivyo kwa Malaria au Ukimwi. Rais Trump pamoja na uzalendo wake wote wa kutaka kuifanya Marekani kuwa ‘Mkuu tena’ akajikuta akilazimika kumwachia kiti Biden.  

 

TUFANYEJE SASA?

Tumshukuru Mungu kwani Rais wetu na Serikali yake kwa ujumla wanaendelea kusisitiza matumizi ya mbinu iliyotuvusha lile wimbi la kwanza la janga la corona ingawa sasa hivi hatuna budi pia kuongezea na mbinu zingine ili kuleta ufanisi zaidi. Hata Malaria kuna kipindi chloroquine ilifanya kazi kwa ufanisi mkubwa sana lakini ikafika kipindi ikaanza kupunguza ufanisi ndipo wataalamu wakaja na mbinu mbadala ya dawa mseto zikiwemo aina nyingine za dawa kama, SP, artmether nk.

 SOMA: Kwanini chanjo ya malaria imekuwa ngumu hivyo kupatikana?

Kwa maoni yangu mimi hapa, sioni haja ya kuanza kulumbana wala kulaumiana. Kwenye vita mkishaanza tu kutupiana lawama adui ndio mnampa nafasi ya kuwapiga vizuri zaidi. Cha msingi kila mmoja wetu tushirikiane kwa kutumia mbinu na silaha zote tunazohisi zinaweza zikatusaidia ili janga hili litoweke tena, haijalishi tunatumia mashine ya kujifukiza au chanjo, lakini kila mbinu ikithibitika tu haina madhara mengine kiafya kama alivyotahadharisha Rais wetu kwenye chanjo, basi mara moja na sisi tuagize hizo chanjo kama ilivyo kwa wenzetu majirani waliotuzunguka.

Kimsingi Rais wetu hakusema chanjo haifai ila alitoa maagizo kabla ya kuchanjwa watu wake ithibitike ni salama asilimia 100%. Kwahiyo Wizara husika ingeongeza kasi ya kufanya tathnmini aliyoagiza Rais ili tusije baadae kusema kwanini hatukujua mapema.

SOMA: 

Taasisi mbalimbali zikiwemo za kidini baada ya waumini wake wengi kukumbwa na vifo isivyo kawaida vinavyohusishwa na changamoto ya upumuaji tayari zimetoa mpaka takwimu za viongozi wao kufariki dunia kwa dalili zinazofanana na zile za gonjwa la Uvico 19 ( Covid 19). Lakini bado watu hatujaonyesha kwa dhati mwamko wa kujilinda tuliouonyesha katika lile wimbi la kwanza la covid 19 mwaka 2020. Iko wapi tena ile amsha-amsha ya Mama yetu Ummy Mwalimu ambayo pengine ndiyo iliyosaidia watu tukachukua tahadhari kwa kiasi kile tatizo likapungua?

 SOMA: Mungu hutenda kwa namna ya ajabu!

Tofauti na viumbe wengine, Mwenyezi Mungu tayari ameshatupa Wanadamu maarifa kwa makusudi  ili tuweze kuyatumia kukabiliana na mazingira yetu wenyewe, tukishindwa kufanya hivyo basi Mungu hawezi kutusaidia kwa njia za kimiujiza ingawa pia anaweza kufanya hivyo akipenda mwenyewe. Tuzidishe kumuomba lakini kamwe tusitegemee miujiza, akipenda mwenyewe kutushushia miujiza basi ni vizuri wala hatuwezi kumhoji.

Kama Rais wetu John Pombe Magufuli alivyotuasa kuwa HOFU ni hatari kuliko hata Corona yenyewe, hivyo badala ya kutiana hofu na woga huku mitandaoni tujitahidi kuelezana ukweli kwa njia ambazo hazitatuzidishia HOFU, Hata mtu anayejua atakufa muda mfupi ujao anapoambiwa ukweli wenye matumaini kamwe hofu haina nafasi kwake.  

…………………………………………………

Mpenzi msomaji wa makala hizi, ikiwa wewe ni mpenzi wa makala na chambuzi za kina zinazohusiana na Fedha, Ujasiriamali na Biashara nakukaribisha sana kwenye MASTERMIND-Group na Channel yetu ya MICHANGANUO-ONLINE, mahali ambapo unaweza kupata kila siku masomo yasiyopatikana mahali kwingine kokote.

Kiingilio kwa mwaka mzima ni sh. 10,000/= na unapata bure kitabu (Mashuhuri )toleo jipya la 2021 cha MICHANGANUO YA BIASHARA NA UJASIRIAMALI. Unaunganishwa pia na Group la Whatsapp kwa ajili ya masomo ya kila siku lakini pia Channel ya Telegram ambayo unaweza kudownload bure masomo mengine yote ya fedha yaliyowahi kufundishwa katika group hili siku za nyuma.

Katika group kila siku pamoja na masomo ya fedha(exclusively) pia tunafanya uchambuzi wa michanganuo ya Biashara zile zilizokuwa na uwezo mkubwa wa kuzalisha faida haraka Tanzania. Michanganuo yetu ni halisi inayozingatia kanuni zote za mlolongo wa biashara kuanzia muhtasari, Bishara, Bidhaa/Huduma, Soko, Mikakati & Utekelezaji, Uongozi, Fedha, mpaka Viambatanisho muhimu. Kitabu kina michanganuo 10 ya biashara za Kitanzania zenye fursa kubwa ya kutengeneza faida.

Kujiunga, Lipia kiingilio sh. 10,000/= kupitia namba zetu, 0765553030 au 0712202244 jina Peter Augustino Tarimo kisha ujumbe usemao, “NIUNGE NA MASTERMIND GROUP LA MICHANGANUO-ONLINE NA CHANNEL YA MASOMO” Utaunganishwa muda huohuo pamoja na kutumiwa OFFA yako kisha masomo ya kipekee jioni saa 3 mpaka saa 4 usiku.  

Nafasi katika group zimebaki chache hivyo ni vizuri ukawahi mapema isijekuwa kama mwaka jana nilipata lawama nyingi sana baada ya nafasi kujaa. Sisi huwa hatuendeshi magroup zaidi ya moja la whatsapp kutokana na kujali zaidi ubora wa kile tunachofundisha katika kutekeleza moja ya kaulimbiu yetu ya mwaka huu isemayo;  KUMJALI MTEJA KWA KIWANGO CHA HALI YA JUU KABISA

Asante sana, na chukua tahadhari ya corona bila kuruhusu HOFU wala WOGA;

Ni mimi

Peter A. Tarimo

Mwandishi na Mhamasishaji wako.

0 Response to "TULIKOSEA WAPI TANZANIA CORONA IKARUDI TENA KWA KASI HII?"

Post a Comment