NDEGE WA AJABU ALIYETOWEKA DUNIANI NI FUNZO KUBWA KWA BIASHARA ZETU KIPINDI HIKI CHA JANGA LA CORONA (COVID 19) | JIFUNZE UJASIRIAMALI

NDEGE WA AJABU ALIYETOWEKA DUNIANI NI FUNZO KUBWA KWA BIASHARA ZETU KIPINDI HIKI CHA JANGA LA CORONA (COVID 19)

Hakuna mtu yeyote leo hii Duniani hata awe Donald Trump mwenyewe anayeweza akasimama na ‘kujimwambafy’ kuwa eti biashara yake inadunda kama kawaida wala Covid 19 haijaitikisa. Hata ukiangalia zile biashara zenye kinga maalumu dhidi ya majanga nilizoziandikia makala wiki chache zilizopita, tayari sasa nazo zimekwishaanza kusukwasukwa na mawimbi ya corona mithili ya meli kubwa inayokumbwa na dhoruba kali.

Wengi wetu tumebakia tu tumeduwaa tusijue ni nini cha kufanya. Hakika haijawahi kutokea miongo ya hivi karibuni!

Pamoja na hali hiyo ya kutisha ngoja nikusimulie mkasa wa ndege mmoja mpole sana lakini cha kusikitisha mpaka ninapoandika hapa sasa tayari ndege huyo alishatoweka katika uso wa dunia hii siku nyingi na inasemekana kuwa ni sisi Binadamu tuliochangia kutoweka kwake.

SOMA: Wanasayansi wagundua mnyama wa ajabu

DODOO ni ndege wakubwa walioishi katika mapori na misitu ya Kisiwa cha Mauritius kilichopo katika Bahari ya Hindi. Kabla ya Wazungu kuingia katika kisiwa hiki miaka ya 1500, Mauritius kilikuwa hakijawahi kukaliwa na binadamu yeyote yule wala wanyama zaidi ya aina chache tu za ndege akiwamo na huyu Dodoo.

Hivyo Dodoo waliishi Mauritius kwa Amani na utulivu pasipo hatari yeyote ile kwa mamilioni ya miaka iliyopita huko nyuma. Kwa mara ya kwanza kabisa Wareno ndio waliokuwa binadamu wa kwanza kukanyaga katika kisiwa hiki hapo mwaka 1505 na mara moja Kisiwa cha Mauritius kikaanza kuwa kama kituo kikubwa cha Meli zilizokuwa zikifanya biashara ya viungo baina ya Ulaya na nchi nyingine za Mashariki ya mbali na Asia.

SOMA: Kumbe sokwe hugawana vitu sawa na binadamu.

Dodoo waliokuwa na uzito hadi kilo 20 wakaanza kugeuka wahanga kwa kuwa kitoweo cha Mabaharia wa meli zilizotia nanga katika kisiwa cha Mauritius. Baadae Wadachi nao walikitumia kisiwa hiki kama makazi kwa wafungwa waliohamishwa kutoka huko kwao. Wafungwa hawa walihamia huko wakiwa na wanyama mbalimbali wafugwao na wasiofugwa kama vile Nguruwe, Nyani, Paka na mbwa.

Taratibu ndege Dodoo waliendelea kupungua siyo tu kwa sababu ya kufanywa kitoweo bali pia wanyama waliohamia na Wadachi nao walianza kuwawinda Dodoo kila kona na kuwatafuna. Ndani ya kipindi cha takribani miaka 100 tu mpaka kufikia1680 Dodoo wakawa ni ndege waliotoweka kabisa Duniani.

SOMA: Njia mpya za kufanya mambo, Dunia, Biashara, Ajira vinabadilika kwa kasi ya ajabu

Sasa basi stori hii inatufunza nini kuhusiana na biashara zetu wakati huu mgumu wa Janga la Corona (Covid 19)?

Sawa tu na Dodoo walivyoishi kisiwani Mauritius kabla ya Wazungu kuingia kisiwani humo, biashara nyingi kabla ya Desemba 2019 zilikuwa zikishamiri kama kawaida na hakukuwa na hatari kubwa iliyozikabili na uchumi kote duniani ikiwemo Tanzania ulikuwa ukikua kwa viwango vya kuvutia.

Lakini ujio wa Corona tangu December 2019 ilikuwa sawasawa na kipindi cha ujio wa Wareno kule Mauritius mikaka ya 1500. Mpaka kufikia hii Apili 2020 biashara karibu zote zinachechemea, zimepoteza wateja na hazina tena uwezo wa pesa wa kujitangaza wala muda kwani watu kote duniani imewabidi wajifungie majumbani mwao.

SOMA: Kufa au kuanguka kwa biashara yako ndogo fanya vitu hivi 9 kujiepusha

Hamna tofauti na jinsi ndege Dodoo walivyopoteza uhuru wao wa kutembea kokote wapendako kisiwani Mauritius. Imekuwa ni sawa na kipindi kile cha ujio wa Wadachi wakiwa na wanyama kama nguruwe, nyani, paka na mbwa kuja kupiga kambi kwenye kisiwa hicho kilichokuwa hakikaliwi na mtu kwa mamilioni ya miaka hapo kabla.

Sasa basi tunaweza kufanya kitu gani kuweza kuzinusuru biashara zetu kama hali yenyewe ndio hivyo ilivyo?

Hakuna njia nyingine zaidi ya kubadilika na kuendesha biashara zetu kulingana na mazingira yalivyo. Badala ya kuanza kujifungia majumbani na kusubiri serikali ije ituletee unga, ni lazima tuwe wabunifu, tusibakie tu kuwa wapole kwa corona kama Dodoo walivyoendelea kubakia kuwa wapole mpaka wakamalizwa wote.

SOMA: Unawezaje kuyakabili magumu, maanguko na mikasa ya kutisha maishani kama hii?

Wangelijua mapema wakajifunza hata kujificha kwenye mapango au kuruka juu kama ndege wengine mfano Tai nk. pengine Dodoo wangelikuwa wanaishi mpaka leo hii. Lakini badala yake Dodoo hawakufanya mabadiliko yeyote zaidi ya kuendelea kuishi maisha waliyozoea kuishi hapo kabla

Mwanasayansi mashuhuri Charles Darwin aliwahi kusema hivi;

Viumbe watakaopona na kuishi duniani siyo wale wenye nguvu nyingi sana bali ni wale watakaojibadilisha ili kuendana na mabadiliko ya kimazingira wanayoishi

Tusikubali kuwa kama Dodoo, tubadilishe namna ya kufanya biashara zetu kabla hazijafa.

Tutafute njia mbadala za kufanya biashara zetu sasa kwa mfano, tuvae barakoa(mask), tuoshe mikono kila mara, tuzingatie umbali wa mita moja na hata zaidi ya huo. Ikiwa biashara inafaa kutumia mtandao wa intaneti basi tuitumie zaidi nk. Cha kutia faraja ni Serikali yetu kutambua umuhimu huo wa kutumia njia mbadala za kupambana na janga hili kuliko kufungia watu moja kwa moja (total lock down).

SOMA: Usiogope, mabadiliko katika maisha ni kama plasta, ikishabanduka kidonda hupona chenyewe.

Basi na sisi wananchi tujiongeze maambukizi yasiongezeke ili tuendelee kuwa angalao na huru tukifanya biashara zetu. Katika nyumba zetu za ibada pia tuwe makini tusali tukiwa na tahadhari zote, tofauti na wanyama Mungu ametupa akili na maarifa yote ya kisayansi kwa lengo la sisi kuyatumia maarifa hayo kujisaidia na siyo kujibweteka na kusubiri Mungu atuokoe na Janga pasipo sisi kuwajibika.

Kitu kingine cha msingi sana cha kufanya kipindi hiki ili biashara zetu zisiwe kama Dodoo ni KUTOA THAMANI KWA MTEJA. Uza thamani na wala siyo bidhaa au huduma, kwa kuwauzia thamani wateja wako hawatakusahau kamwe hata baada ya janga hili kupita. Kuwauzia wateja thamani maana yake ni kutatua shida walizokuwa nazo kwa weledi kushinda matarajio yao.

…………………………………….

TANGAZO MUHIMU


2.   Kujiunga na Group letu la Watsap na Telegram la masomo ya Fedha na Michanganuo kila siku, lipa kiingilio shilingi 10,000/= kupitia namba; 0765553030 au 0712202244 kisha utume ujumbe usemao, “NIUNGANISHE NA GROUP LA MICHANGANUO-ONLINE NA OFFA YA VITU 6

3.   Unaweza pia kujipatia vitabu vyetu vifuatavyo (softcopy) kwa bei ya punguzo, ukinunua vyote 3 ni shilingi elfu 15 tu badala ya elfu 18. Punguzo hili ni kwa muda mfupi. Hardcopy pia vinapatikana .

  5,000/=

 3000/=


0 Response to "NDEGE WA AJABU ALIYETOWEKA DUNIANI NI FUNZO KUBWA KWA BIASHARA ZETU KIPINDI HIKI CHA JANGA LA CORONA (COVID 19)"

Post a Comment