Kama mwandishi wa blogu kuhusiana na masuala ya maendeleo
na mafanikio ya watu nilihisi kuwa na wajibu wa kuandika japo kidogo kuhusiana
na mchango wa Hayati Mzee Mkapa kama nilivyowahi kuandika juu ya michango ya
watu wengine mashuhuri hapa nchini waliopata kunivutia na kunifanya nipende
kufuatilia maisha yao mfano Wafanyabiashara, Hayati Mzee Reginald Abrahamu
Mengi, Ali Mufuruki, Ruge Mutahaba na wengineo.
SOMA: Siri kubwa 2 za mafanikio ya Ruge Mutahaba Clouds FM: Wengi hatukuzijua mpaka anaumwa, kufariki na kuzikwa leo
SOMA: Siri kubwa 2 za mafanikio ya Ruge Mutahaba Clouds FM: Wengi hatukuzijua mpaka anaumwa, kufariki na kuzikwa leo
Hata hivyo katika siku zile za maombolezo nilipanga
nipost kitu lakini roho yangu ikawa nzito, si kwa sababu sikuwa na cha kuandika
hapana, bali niliishiwa tu nguvu ya kuandika kutokana na kukata tamaa.
Nilijiuliza moyoni, “Kwanini wale watu ninaowahusudu sana kutokana na michango yao katika
maendeleo ya Watanzania na binadamu kwa ujumla Mwenyezi Mungu huwa anawachukua wakati ninaohisi siyo sahihi
kuwachukua?”
“Ni juzijuzi tu kamchukua Ruge Mutahaba, hatujakaa vizuri
akamchukua Mzee wetu Reginald Mengi, hata hatujapoa akamchukua tena Mzee Ally Mufuruki.
Basi Moyo wangu ulinyongonyea nikaona hata sina sababu ya kuandika, ni bora
nikae tu kimya lipite hivihivi, nikiomboleza ndani kwa ndani”.
Jana wakati nikipekuapekua makabrasha yangu ya zamani,
nikakutana na nakala za magazeti yangu ya zamani miaka ya 2000 wakati
nilipokuwa nafanya uandishi wa habari katika vyombo vya habari hususani katika
magazeti(Print Media). Nilikutana na gazeti(Jarida) nililokuwa nikilimiliki
mimi mwenyewe binafsi lililoitwa SAYARI MPYA, mbele katika stori
zilizoongoza niliona picha ndogo ya Hayati mzee Mkapa kipindi hicho akiwa Raisi
wa nchi na kichwa cha habari kilichosema; SIRI
ILIYOJIFICHA KIPINDI CHA UTAWALA WA MKAPA”
Makala hii niliyoiandika miaka 15 iiliyopita nilikuwa
wakati huo nataka kufichua mambo mbalimbali aliyokuwa ameyafanya Rais Mkapa
wakati akimalizia muhula wake wa pili na wa mwisho madarakani, mambo ambayo
inawezekana kuna watu wengi walikuwa hawayajui au pengine walikuwa
hawayachukulii kwa uzito unaostahili.
SOMA: Mzee Reginald Mengi hajafa, ataendelea kuishi katika roho zetu siku zote
SOMA: Mzee Reginald Mengi hajafa, ataendelea kuishi katika roho zetu siku zote
Kukutana na majarida hayo kuliamsha upya moyoni mwangu
moto na ari kubwa ya kuandika chochote kile kumhusu Hayati Mzee Benjamini
William Mkapa. Nilihisi upya kuwiwa na kuona sitakuwa nimemtendea haki Mentor
wangu huyu niliyempenda na kuzihusudu mno kazi zake. Mara moja niliketi kitini na
kuanza kuandika makala unayoisoma sasa hivi.
Nilijifariji
kwa kuikumbuka Zaburi 90:10,
“Miaka ya kuishi ni sabini, au
tukiwa wenye afya, themanini; lakini yote ni shida na taabu! Siku zapita mbio,
nasi twatoweka mara!”
Wanadamu sote tutalala mavumbini na siku zetu za kuishi
ni miaka 70 au 80, na Kwa Mzee Mkapa alishapita miaka 70 hivyo sina sababu kubwa
ya kuendelea kuomboleza bali kukumbuka hima yote mazuri aliyotufanyia wakati
tukiwa nae hapa Duniani huku tukienzi yale aliyotuachia kupitia kitabu chake
cha MY LIFE MY PURPOSE sawa sawa na
kile cha Mzee Mengi, I Can, I Must, I Will: The Spirit ofSuccess
Kiukweli naweza kusema Mzee Mkapa alikuwa ni “Role Model”
wangu na mtu aliyenifanya niipende kazi
ya uandishi wa habari. Ni katika kipindi chake ndipo nilipopata msukumo wa
kwenda kujiunga na chuo cha uandishi wa habari, nilihusudu sana na kuzipenda
hotuba zake kila nilipozisikia nikawa nazirekodi kwa taperecorder yangu ndogo
na kisha kuja kuzisikiliza baadae.
Kilichonifanya nimpende Mkapa kiasi hicho ni kauli zake
za kuuchukia sana umasikini, kama ile, “Mtaji wa masikini ni nguvu zake
mwenyewe”, maswala ya utandawazi pamoja na Sayansi na teknolojia. Rais Mkapa
aliamini katika ukweli kwamba, UKITAKA KUMSAIDIA BINADAMU MWENZAKO, BASI
MPATIE MSAADA UTAKAOMWEZESHA KUJISAIDIA YEYE MWENYEWE (Usimpe samaki
bali mpe nyavu na mafunzo ya kuzitumia nyavu zenyewe)
SOMA: Bilionea Dr. Reginald Mengi hakufa na siri yeyote moyoni, unajua siri zote alimwachia nani?
SOMA: Bilionea Dr. Reginald Mengi hakufa na siri yeyote moyoni, unajua siri zote alimwachia nani?
Mkapa aliamini maendeleo yanaweza tu yakaletwa kwa njia
za kisayansi na kiteknolojia jambo ambalo litabakia kuendelea kuwa kweli mpaka
kesho. Namimi kama kuitikia na kuunga mkono juhudi zile za Mheshimiwa Mkapa
sawasawa na vile watu wafanyavyo siku hizi kwa Mheshimiwa Rais John Pombe
Magufuli, niliamua kwa udi na uvumba kuanzisha gazeti japo sikuwa hata na mtaji
wa kuliendesha zaidi ya nguvu zangu mwenyewe kama mwenyewe Mkapa alivyokuwa
akituasa Watanzania,kuwa “Mtaji wa masikinini nguvu zake mwenyewe”.
Katika kila toleo la gazeti langu hilo nilihakikisha
natenga nafasi ya kutosha kwa ajili ya kuandika mambo mbalimbali ya kimaendeleo
aliyokuwa akiyapa kipaumbele Mheshimiwa Rais Mkapa. Nakumbuka hata katika Toleo
nililochapisha Makala hii ya Siri iliyojificha kipindi cha utawala wa
Mkapa niliandika pia na Tahariri iliyokuwa na kichwa cha habari
kisemacho, “MKAPA ALITUDANGANYA?”
Niliweka pia safu maalumu ya UTANDAWAZI ambayo ilikuwa ni kwa ajili ya kuandika mikakati
mbalimbali tu ya Kitaifa dhidi ya Umasikini na fursa za utandawazi. Safu hii
niliweka zaidi nukuu mbalimbali muhimu za Rais Mkapa wakati huo kama
utakavyoziona hapo chini.
Isitoshe kulikuwa na safu moja ukurasa wa mwisho wa 31
iliyoitwa, UKWELI KUHUSU UKIMWI,
katika safu hii nilipenda sana kuweka nukuu za Rais Mkapa juu ya ugonjwa hatari
wa Ukimwi kama hii hapa chini,
Kwa kifupi gazeti la SAYARI MPYA Sera yake kubwa ilikuwa
ni kuandika masuala mbali mbali yahusuyo maendeleo katika mlengo wa Kisayansi
na Kiteknolojia. Kazi yake kubwa ilikuwa ni kuamsha ari na moto wa maendeleo
kwa vijana na Watanzania wote ili kujiletea maendeleo yao wenyewe bila ya kumtegemea
‘mjomba’ wala ‘shangazi’ kutoka nje, na maono haya sikuyatoa kwingine bali kwa
Hayati Rais Mtaafu Benjamini William Mkapa.
SOMA: Hatimaye ile nyama ya kutengenezwa maabara yaanza kuliwa.
SOMA: Hatimaye ile nyama ya kutengenezwa maabara yaanza kuliwa.
Nilikuwa kwa mfano naweza kuandika Makala inayohusiana na
Safari
za Warusi na Wamarekani anga za juu, lakini lengo langu kubwa hapo hasa
likiwa ni kuonyesha jinsi Sayansi inavyoweza kufannya maajabu endapo tu
itatumika vizuri na kwa malengo yaliyokusudiwa.
Makala nyingi kwa kweli zilikuwa ni za kusisimua sana
mfano zile za Viumbe wa ajabu (UFO) kutoka sayari nyingie, Samaki Mtu(Nguva), Safina
ya nuhu iliyosadikiwa kugunduliwa mlimani huko uturuki, Lugha ya ajabu na siri
ilyopo ndani yake, Siri ya mtu aliyeishi miaka 122, na habari za Wagunduzi
mbalimbali wa Kitanzania waliokuwa wamegundua vitu mbalimbali vya kiteknolojia mfano mkazi mmoja wa Manzese aliyebuni jiko la
kutumia mionzi ya jua kwa kutumia makaratasi ya sigara yanayotupwa ovyo mitaani
na ‘Ford wa Tanzania’, mzee mmoja
aliyebuni jiko linalotumia Oil chafu huko Arusha. Vyote hivi na mengineyo mengi
vilichapishwa katika jarida hili kila mwezi.
Nakumbuka sana kipindi kile Rais Mkapa yeye kama
mwandishi nguli wa habari na makini alikuwa akipenda sana kutuasa waandishi
tusiwe wavivu, alichukia sana waandishi wanaoandika mambo pasipo kufanya
utafiti wa kina na kubalance stori zao kiasi kwamba baadhi ya waandishi walimchukulia
kama mtu asiyewapenda Waandishi wa habari wakati yeye mwenyewe ni zao la tasnia
hiyo. Hata hivyo baadae tulimwelewa vizuri kwamba aliwapenda waandishi pale
walipoonyesha kujituma na kuwajibika kitaaluma sawa na yeye mwenyewe alivyokuwa
akiwajibika enzi zake akiwa mwandishi wa magazeti ya chama na serikali.
Kwa kweli hivi ndivyo na mimi ninavyoweza kuukumbuka mchango
wa Hayati Rais Mtaafu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa ambaye jina lake
halitafutika kamwe katika vitabu vya historia ya nchi hii ya Tanzania, alifanya
makubwa mengi ya maana ambayo pengine kwa bahati mbaya hatukuweza kuyaona
kipindi kile akiwa madarakani na hata muda baada ya kuondoka madarakani lakini
kidogokidogo tumekuja kutambua kumbe aliyoyafanya yalikuwa ni mambo makubwa
ambayo pengine kama asingeliyafanya tusingelikuwa hapa tulipo leo hii.
SOMA: Seth Katende, Mwanaume utajiitaje bikira?
SOMA: Seth Katende, Mwanaume utajiitaje bikira?
Ni kweli hakuna binadamu aliyekamilika duniani na Mkapa
kama binadamu wengine naye hakosi kuwa na mapungufu yake japo ni vema
tukayachukua tu yale mazuri na kuacha mapungufu kwani hata yeye mwenyewe
aliwahi kukiri hivyo.
Naipenda kauli yake moja ambayo pia aliinukuu kutoka
katika hotuba ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere siku za nyuma isemayo;
“Kupanga ni kuchagua, kwenye kila hatua ya
maendeleo yetu yapo mambo tunayoweza kwa wakati huo na yapo mengine ambayo
hatuyawezi kwa wakati huo, na kwa kadiri nchi ilivyo masikini ndivyo ambavyo
ilivyo vigumu kuchagua baina ya mahitaji ambayo yote yanaonekana ni muhimu”- Benjamin William
Mkapa.
0 Response to "SIRI ILIYOFICHIKA KIPINDI CHA UTAWALA WA MKAPA"
Post a Comment