Wahenga hawakukosea waliposema; Kikulacho kii nguoni
mwako na mchelea mwana kulia hulia yeye. Haya ndiyo yaliyomkuta kijana mmoja
aitwaye Sam, mfanyabiashara mdogomdogo wa matunda na mbogamboga kama nyana,
vitunguu, kabeji, karoti, pilipili hoho na matango katika maeneo ya mbezi
mwisho.
Sam kwa muda mrefu alikuwa akijihusisha na biashara ya
kuuza matunda na mbogamboga katika eneo la Mbezi mwisho lakini mwaka huu mwezi ule
wa 6 alipata wazo la kutanua zaidi biashara yake kwa kwenda kuomba mkopo kutoka
katika taasisi moja ya fedha iliyopo palepale Mbezi mwisho. Baada ya kujiunga
na kikundi cha watu wengine wanne walikwenda katika taasisi hiyo na
wakakubaliwa kupewa kila mmoja shilingi laki tatu na nusu(350,000/=) fedha
ambazo Sam alikuwa na malengo ya kufungua tawi la biashara yake ya matunda na
mbogamboga eneo jingine.
SOMA: Kushuka bei ya mchele, kilo moja hatuuzi, tunaanzia kilo 5 na kuendelea.
SOMA: Kushuka bei ya mchele, kilo moja hatuuzi, tunaanzia kilo 5 na kuendelea.
Baada ya kufanya utafiti wa kina alibaini kuwa tawi la
biashara yake mpya angeliweka eneo jingine tofauti na Mbezi Mwisho na akaamua
tawi hilo afungue maeneo karibu na stendi ya Kwa Msuguri. Ingawa maeneo hayo ni
hifadhi ya barabara hata hivyo haikumzuia kuweka biashara yake hapo kwani
asingeliweka banda la kudumu. Wafanyabiashara wengi huweka vibanda vya muda
ambavyo inakuwa rahisi kuhamishia eneo jingine pale serikali inapowataka
kufanya hivyo ili kupisha ujenzi wa barabara au shughuli nyingine zozote zile
za umma.
Kijana Sam huku akiendelea na biashara katika “goli” lake
la zamani pale Mbezi Mwisho, aliiba muda wake kidogo kwa siku mbili tatu, na
kwenda kusimamia ujenzi wa meza kwa ajili ya biashara yake hiyo mpya. Alijenga
meza safi pale stendi kwa Msuguri akitumia fedha alizotoa kwenye biashara yake
kiasi cha shilingi laki moja na nusu hivi. Kumbuka wakati huo bado ndio
anafanya mchakato wa kupata zile fedha sh. 350,000/= kutoka taasisi ya fedha.
SOMA: Je, unakopesheka na taasisi za fedha au benki?
SOMA: Je, unakopesheka na taasisi za fedha au benki?
Bada ya kukamilisha ujenzi wa meza na kuweka turubai la kuzuia jua na mvua
sasa alianza kazi nyingine ya kumtafuta mtu atakayeuza kwenye biashara hiyo
kwani asingeweza kuwa Mbezi kwenye biashara yake ya zamani na wakati huohuo
tena awe Kwa Msuguri kwenye biashara mpya. Mwishowe alifanikiwa kumpata kijana
mmoja mdogo aliyemaliza darasa la saba hivi karibuni, ukimwangalia anaweza kuwa
na umri wa miaka 15 hivi.
Baada ya kuchukua ule ‘mzigo’(fedha) kutoka katika
taasisi waliyokopa, mara moja alikwenda kuagiza bidhaa mbalimbali akianza na
matenga 2 ya nyanya, gunia la viazi mviringo, gunia la vitunguu, karoti na
mbogamboga na matunda mengine madogomadogo. Alinunua pia na mzani kwa ajili ya
kuwapimia wateja wanaopenda kununua vitu kama nyanya, viazi au vitunguu kwa
kilo. Meza ilipendeza sana kwa mpangilio wa vitu vilivyoenea vyote hata wateja
wakaanza kuhama kutoka magenge mengine ya jirani na kuja kununua vitu pale.
SOMA: Kweli huduma hii kwa wateja ni Customer care au ni customer Kero?
SOMA: Kweli huduma hii kwa wateja ni Customer care au ni customer Kero?
Mama lishe na baba lishe wote wa eneo lile wengi
walikimbilia pale, na ungewasikia wakisema, “Huyu dogo anauza vitu bei rahisi
sana na ukiomba kuongezewa siyo mchoyo hata kidogo”. Wakati yote hayo
yakiendelea Sam alikuwa bize na biashara yake ya zamani kule Mbezi mwisho na
alifika pale tu muda wa kwenda kuchukua bidhaa zilizokwisha. Bidhaa hazikuwa
zikikaa muda mrefu, akileta nyanya leo siku ya kwanza, ya pili zimeisha! Halikadhalika
na vitu vingine ilikuwa ni hivyohivyo.
Kuna kitu kingine cha ajabu nilichoshuhudia kwa yule ‘dogo’
muuuza genge, jirani palikuwa na vijana wauza chipsi na supu waliojenga ukaribu
wa ajabu na huyu dogo, kila muda unapofika walimletea vyakula bila hata yeye
kuagiza, asubuhi walimletea supu chapatti na chai. Mchana chipsi, kuku na mayai
pembeni, na jioni walimletea kongoro au paja la kuku na chipsi kidogo.
SOMA: Unajua biashara ya chipsi kuku, mayai na soda inavyolipa Dar?
SOMA: Unajua biashara ya chipsi kuku, mayai na soda inavyolipa Dar?
Haikuwa rahisi mtu wa pembeni labda kumpa kijana yule
tahadhari yeyote kwani kwanza huelewi yeye na mwenye biashara wana uhusiano
gani na wala wakati akiletewa hivyo vyakula kulikuwa hamna dalili yeyote ya
yeye kukataa, walikuwa wanacheka kama kawaida.
Jambo jingine lililoanza kunipa tashwishi ni siku moja kumsikia
yule dogo akimlalamikia muuza chipsi mmoja akimwambia; “Mimi sipendi bwana, kwanza
nakudai hela zangu nyingi tu, kila ukichukua, baadae unasema umeshanilipa, mimi
nakuachia Mungu tu ndiye atakayekulipa”
Du! Kauli aliyoitoa yule dogo ilinishtua sana nikaanza
kuhisi dhahiri kuwa yule Dogo alikuwa akinyanyaswa kwa namna fulani na
wafanyabiashara waliomzunguka bila tajiri yake kugundua na walitumia udogo wake
na ugeni wake katika biashara kumkandamiza na kujinufaisha isivyokuwa halali na
mali zilizokuwa pale gengeni.
SOMA: Ukijua gharama halisi za wafanyakazi kwenye biashara yako utawafukuza!
SOMA: Ukijua gharama halisi za wafanyakazi kwenye biashara yako utawafukuza!
Baadae ilikuja kubainika kuwa kumbe wale vijana wauza
chipsi walikuwa wamefikia hatua ya kuja kujichukulia chenji wenyewe katika droo
ya pesa ya huyu dogo hata bila ridhaa yake. Dogo wakati mwingine akitoka kidogo
kwenda haja, akija mteja gengeni vijana wa chipsi hujiuzia kama shamba la bibi
na kuweka fedha mifukoni mwao.
Binafsi kwa kuwa eneo hilo nilikuwa nikifika tu kwa muda
kwa ajili ya kuangalia na mimi maendeleo ya biashara yangu niliyokuwa
nimemwachia mtu, baada ya kugundua picha ile niliazimia kumtafuta Sam kwa kuwa
tulikuwa tukifahamiana japo si sana, nimueleze jinsi ambavyo angeweza kuzuia
uharamia uliokuwa ukifanyika pale kwenye biashara yake.
Wakati nikiwa katika harakati hizo za kuonana naye siku
mbili tatu nilisikia kuwa ile meza ilikuwa imefungwa na dogo alikuwa
ametimuliwa kwa upotevu wa karibu mtaji wote wa shilingi laki tatu na nusu
ndani ya muda mfupi tu. Sam aliamua kuifunga ile biashara na kuelekeza zaidi
nguvu zake katika biashara yake ya zamani kule Mbezi mwosho ili angalao aweze
kumudu marejesho ya ule mkopo ambao bado ni mbichi kabisa.
Biashara ya Sam haikufa kutokana na ukosefu wa mtaji wa
kutosha, wala haikufa kutokana na kukosa wateja wa uhakika. Biashara ile
ilikufa kutokana na ukosefu wa usimamizi makini, kijana aliyewekwa pale
hakupewa mafunzo stahiki na wala tajiri yake hakujishughulisha angalao kufanya
uchunguzi mapema wa jinsi muenendo wa biashara ile ulivyokuwa. Aidha pia
alishindwa kuweka mfumo madhubuti wa mahesabu ambao ungemuwezesha kubaini
mapema zaidi upotevu wa pesa kabla hali haijawa mbaya kiasi kile.
SOMA: Jinsi ya kusimamia hesabu katika biashara ndogo unayomwachia mfanyakazi akuuzie.
SOMA: Jinsi ya kusimamia hesabu katika biashara ndogo unayomwachia mfanyakazi akuuzie.
Angeweza kwa mfano wakati anaanza, kumwekea mafungu
kadhaa tu ya vitu mbalimbali, mfano mafungu 20 ya viazi, mafungu 30 ya nyanaya,
vitunguu nk. kisha jioni achukue hata nusu saa au lisaa la kuja kufanya
tathmini kujua ameuza mafungu mangapi na ni mafungu mangapi yaliyobakia. Hata hawa
vijana wauza chipsi na majirani waliokuwa wakimiminika gengeni hapo
kujichukulia vitu kwa bei ya mteremko na nyongeza kubwa bila shaka
walishatambua biashara ile haikuwa na usimamizi makini na yule dogo hakuwa
kabisa anafahamu kama anafanya makosa makubwa.
Maadui wa biashara yako hawawezi kutoka mbali, wakati
mwingine ni baadhi ya walewale wateja wanaofika kukuungisha, inawezekana
wengine hata wasijue kama wanakuumiza kwa kuwa mteja siku zote yeye hupendelea
unafuu lakini kazi kubwa ya kuzuia madhara yanayoweza kuletwa na wateja wa
namna hiyo ni yakwako wewe mjasiriamali kwa kuamua kuweka sera imara
zitakazoiongoza biashara yako hata ikiwa wewe haupo pale umemuachia mtu
mwingine.
SOMA: Kama unaona ni kazi ngumu kusimamia hesabu za biashara yako, bora uachane nayo vinginevyo utavuna mabua.
SOMA: Kama unaona ni kazi ngumu kusimamia hesabu za biashara yako, bora uachane nayo vinginevyo utavuna mabua.
Kwa mfano unaweza kuandika katika karatasi mambo yote
asiyotakiwa kuyafanya mfanyakazi wako ukampatia akakaa na hiyo karatasi mfukoni
au ukabandika ukutani ili ajikumbushe kila siku. Vitu kama vile, Utoaji holela
wa chenji, kuruhusu mtu akope, kutoruhusu mtu mwingine yeyote afanye mauzo kwenye
biashara hata ikiwa ni ndugu yake, matumizi binafsi kama chakula nk. Ni lazima
kila kitu uwe na utaratibu wake na utaratibu huo uhakikishe unafuatwa
vinginevyo mfanyakazi huyo hakufai mwachishe utafute mwingine kabla mtaji wako
haujamalizika kama wa Sam.
...........................................................
Kwa vitabu katika lugha ya kiswahili kutoka SELF HELP BOOKS tembelea, SMART BOOKS TZ
Kujiunga na Group la masomo ya kila siku Wasap(0765553030) MICHANGANUO-ONLINE, kuhusiana na mzunguko wa fedha kwenye biashara na Michanganuo ya biashara mbalimbali bunifu zinazolipa, toa kiingilio chako sh elfu 10 Kupitia namba za simu, 0765553030 au 0712202244 kisha tuma ujumbe wa "NIUNGANISHE NA GROUP LA MICHANGANUO"
Kupata kitabu maarufu cha KANUNI YA KUJIFUNZA ELIMU YA PESA NA MAFANIKIO KWA UFANISI na vitabu vingine vingi bila malipo yeyote, 'free of charge', Jiunge(subscribe) katika blogu hii kwa kubonyeza hapa, >>>JIUNGE NA BLOGU HII. kisha ufuate maelekeza pamoja na kucheki email yako.
...........................................................
Kwa vitabu katika lugha ya kiswahili kutoka SELF HELP BOOKS tembelea, SMART BOOKS TZ
Kujiunga na Group la masomo ya kila siku Wasap(0765553030) MICHANGANUO-ONLINE, kuhusiana na mzunguko wa fedha kwenye biashara na Michanganuo ya biashara mbalimbali bunifu zinazolipa, toa kiingilio chako sh elfu 10 Kupitia namba za simu, 0765553030 au 0712202244 kisha tuma ujumbe wa "NIUNGANISHE NA GROUP LA MICHANGANUO"
Kupata kitabu maarufu cha KANUNI YA KUJIFUNZA ELIMU YA PESA NA MAFANIKIO KWA UFANISI na vitabu vingine vingi bila malipo yeyote, 'free of charge', Jiunge(subscribe) katika blogu hii kwa kubonyeza hapa, >>>JIUNGE NA BLOGU HII. kisha ufuate maelekeza pamoja na kucheki email yako.
0 Response to "MAADUI WAKUBWA WA BIASHARA YAKO USIOWADHANIA HATA KIDOGO (KIKULACHO…)"
Post a Comment