UKIJUA GHARAMA HALISI ZA WAFANYAKAZI KWENYE BIASHARA YAKO, UTAWAFUKUZA KAZI | JIFUNZE UJASIRIAMALI

UKIJUA GHARAMA HALISI ZA WAFANYAKAZI KWENYE BIASHARA YAKO, UTAWAFUKUZA KAZI

kuajiri mfanyakazi katika biashara yako
Kuajiri wafanyakazi katika biashara ni jambo lisiloepukika hata kidogo ikiwa mmiliki wa biashara au mjasiriamali atataka mafanikio katika biashara yake. Wakati biashara inapoanzishwa mjasiriamai anaweza akavaa kofia zote yeye mwenyewe kwa kufanya majukumu yote kuanzia kuwa mkurugenzi, meneja wa biashara, mlinzi, karani, mpokeaji wageni(receptionist), mtunza pesa(cashier), mtunza stoo(store keeper) na hata mhasibu peke yake.

Lakini kwa kadri muda unavyozidi kwenda na biashara kupanuka zaidi, maendeleo hayo yatahitaji nguvukazi zaidi katika kuhakikisha majukumu muhimu ya biashara yanatekelezwa kwa ufanisi wa hali ya juu na kwa weledi unaotakiwa. Kumbuka mjasiriamali au mmiliki wa biashara anapokuwa akivaa kofia hizo zote kuna baadhi ya kazi ambazo anakuwa anazimudu zaidi kuliko nyingine na nyingine anakuwa anazifanya bila ya kuwa na weledi wa kutosha ama uzoefu unaotakiwa lakini hana budi kufanya hivyo kwani anakuwa hana chaguo mbadala kutokana na ufinyu wa mtaji.


Baada sasa ya kuvuka hatua hiyo ya kuanza biashara na kuingia katika hatua mpya ya upanuzi wa biashara kwa kuajiri wafanyakazi au wasaidizi, zipo faida nyingi zitokanazo na kitendo cha kuweka wasaidizi lakini pia kama ilivyokuwa kawaida kwa ujasiriamali changamoto ni lazima ziwepo na kwa kuwa mjasiriamali hupaswi kuogopa changamoto unatakiwa ufahamu namna ya kukabiliana na changamoto hizo kusudi uweze kupata mafanikio katika biashara yako uliyokusudia kuyapata.

Moja ya changamoto kubwa mfanyabiashara au mjasiriamali atakayokutana nayo ni gharama au mzigo wa gharama zitakazosababishwa na kuajiri mfanyakazi au wafanyakazi katika biashara yake. Kumbuka huko nyuma mjasiriamali huyu alizoea kufanya kila kitu peke yake na hivyo hakuwa na gharama yeyote kuhusiana na mfanyakazi. Hata hivyo zipo changamoto zingine nyingi kama vile wafanyakazi kukosa uaminifu, kuwa wezi na hata kufanya uzembe wa aina mbalimbali unaoweza kusababisha biashara kutokuweza kutengeneza faida kama inavyokusudiwa lakini nyingi ya changamoto hizo zinaweza zikapatiwa suluhisho kupitia mbinu mbalimbali.

Kwa kiasi kukubwa matatizo ya kuajiri wasaidizi katika biashara au changamoto zozote zile msingi wake mkubwa upo katika gharama za biashara. Hii inamaanisha kwamba ikiwa utaajiri mfanyakazi, tayari unaongeza gharama katika biashara, ikiwa mfanyakazi atakuibia maana yake gharama kwenye biashara itazidi kuwa kubwa, halikadhalika ikiwa mfanyakazi atafanya uzembe wowote ule, ni mzigo pia kwa biashara.


Hata unapompa marupurupu mfanyakazi wako pia unaongeza gharama kwenye biashara. Hivyo basi unaweza ukaona kwaba mfanyakazi katika biashara ni suala nyeti sana linalohitaji umakini wa hali ya juu kushughulika nalo. Kama mjasiriamali makini unapaswa kujua mbinu zote sahihi za namna ya kuajiri wafanyakazi na jinsi ya kuwatendea kusudi waweze kuifanikisha biashara yako badala ya kuiua.

Gharama halisi za wafanyakazi wako
Mara nyingi tunapowaajiri watu wa kutusaidia katika biashara zetu huwa tunaangalia zaidi ule mshahara wa mwezi tunaokubaliana nao tu, hatuzingatii gharama nyinginezo mbalimbali ambazo huwa tunaingia wakati mfanyakazi huyo akiwa anaendelea kufanya kazi. Zipo gharama utakazolazimika kumlipia mfanyakazi wako nje ya mshahara wake penda usipende ikiwa utataka kweli mambo yaende na biashara yako iweze kufanikiwa na kinyume cha hapo basi ndipo hukuta mambo hayaendi, wafanyakazi wanaamua kugeuka wezi, wazembe, kutokufanya kazi kwa motisha, kuacha kazi baada ya muda mfupi na hata kula njama na wezi au majambazi kwa ajili ya kukudhuru au kukutia hasara.


Haitoshi tu kumlipa mfanyakazi mshahara wake mliokubaliana hasa hasa mishahara yetu hii ya kibongo ambayo mara nyingi unakuta haitoshelezi hata gharama za maisha za mtu za nusu mwezi. Mbali hata na gharama kwa maana ya fedha kitu cha kwanza mfanyakazi anachokihitaji ni mazingira rafiki na wezeshi ya kazi ambayo yatamvutia mfanyakazi hata kutopenda kukaanyumbani kwake, kila mara atamani kuwa maeneo ya kazini tu. Na hili ni lazima likuingize gharama kidogo kwa mfano maeneo ya kazi kuwa na vivutio kama chai, chakula, eneo zuri la mapumziko, vifaa bora vya kazi, na vitu kama intaneti nk.

Katika biashara kubwa kuna gharama zaidi kwa mfanyakazi, kama vile, gharama za mafunzo, kodi ya mishahara(PAYE TAX), malipo ya uzeeni, bima za afya, gharama za sherehe na viburudisho mbalimbali, malipo na likizo baada ya kujifungua nk. Si hivyo tu zipo gharama nyingine hata mtu huwezi kuzifikiria kama zipo kwa mfano kumbuka hata bili za umeme, maji, jengo na simu mfanyakazi wako atakazotumia pengine nje ya shughuli za kawaida za biashara kama vile kuwasiliana na ndugu jamaa na marafiki au kuchati masula yake binafsi nayo huongeza gharama zinazotakiwa kulipwa na wewe mmiliki wa biashara. Unatakiwa unapopiga gharama ya mfanyakazi wako kwa mwezi basi uhakikishe na gharama hizi nyingine unazizingatia pia.

Kwa mfano unaweza kuwa mfanyakazi unamlipa shilingi kaki tatu kwa mwezi,utakapoamua kukokotoa gharama nyinginezo zote zilizojificha unaweza kuja kukuta gharama halisi ya mfanyakazi huyo ni zaidi hata ya shilingi lkaki tano kwa mwezi mmoja. Sasa hebu fikiria unao labda wafanyakazi wane au watano itakuwa kiasi gani? Ukiwa na roho ndogo unaweza hata kuwapunguza au kuwafukuza wote ukidhani labda utapunguza gharama kumbe wakati mwingine wala siyo sahihi. Kujaribu kupunguza sana matumizi kwa kubana kupita kiasi gharama unazowalipa wafanyakazi wako ni kosa kubwa sana litakalosababisha mazingira ya kazi kuwa magumu na mwishowe wafanyakazi hao kutokufanya kazi katika ubora unaotakiwa.

SOMA: Ajira siyo laana, bali mtaji wa uhakika kuliko aina nyingine zote za mitaji.

Siyo vibaya kujua ni kiasi gani wafanyakazi wako wanakugharimu lakini hakikisha pia unawatumia kwa ufanisi unaolingana na zile gharama unazowalipa, na kuwatumia kwa ufanisi siyo kuwawekea sheria na taratibu kali kupindukia, ndiyo, wapo watu wasiokuwa na masikhara kabisa na wafanyakazi wao, wao muda wote huhisi wanaweza kuwaibia, watahangaika kuweka ulinzi wa kila aina, macctv camera, masoftware ya kila aina ya kompyuta lakini wanachoshindwa kufahamu ni kwamba haiwezekani kabisa kudhibiti utashi wa mtu mwenye akili timamu kama wa kwako, na njia pekee ya kufanya hivyo ili kujenga utengamano katika biashara yako na mwishowe uzalishaji uliokuwa na tija ni kuwapa motisha wafanyakazi wako kwa kadiri inavyowezekana, kuwawezesha, kuwapa uhuru wawe wabunifu, kuwatia moyo,  lakini pia huku ukihakikisha wanafanya kazi kwa mujibu wa taratibu zinavyowataka kufanya.


Usimamizi imara wa biashara yako uwe palepale na mfanyakazi anayekiuka kwa makusudi taratibu zilizowekwa awajibishwe bila kuchelewa kabla mambo hayajawa mabaya zidi.


...........................................................................................

Kwa elimu zaidi ya biashara na ujasiriamali, pata moja kati ya vitabu vifuatavyo au vyote kwa pamoja kutoka self help books Tanzania.
1
2

3

Vitabu vya kawaida vya karatasi(hardcopy) vinapatikana katika ofisi yetu, Mbezi Kwa Msuguri stendi.

Softcopy kwa njia ya e-mail, unatuma pesa na anuani yako ya email kisha tunakutumia kitabu/vitabu muda huohuo.

Bei ya vitabu kutoka juu, ni; 
1. Tsh. elfu 20 hardcopy kwa sh elfu 10 softcopy.
2. Tsh. elfu 10 hardcopy kwa tsh. elfu 5 softcopy
3. Tsh. elfu 5 hardcopy kwa tsh. elfu 3 softcopy

SIMU: 0712202244   AU   0765553030 
JINA:  Peter Augustino Tarimo.

Kwa vitabu zaidi na Michanganuo, tembelea SMART BOOKS TZ

0 Response to "UKIJUA GHARAMA HALISI ZA WAFANYAKAZI KWENYE BIASHARA YAKO, UTAWAFUKUZA KAZI"

Post a Comment