JINSI YA KUMTAMBUA MTEJA KATIKA BIASHARA YA UMACHINGA (NAOMBA USHAURI) | JIFUNZE UJASIRIAMALI

JINSI YA KUMTAMBUA MTEJA KATIKA BIASHARA YA UMACHINGA (NAOMBA USHAURI)

mbinu za kumjua mteja wako ni nani

Hili ni swali alilonitumia mfuatiliaji wa blogu hii kwa kutumia njia ya wasap na swali lake lilikuwa hivi bila kuongeza kitu wala kupunguza; (huwa hatuchapishi jina la muuliza swali kama hajatupa idhini)
Asante, mimi  naitwa ‘Y’.  naomba unielekeze mbinu  za kumtambua  mteja katika  biashara ya umachinga.

MAJIBU:
Wewe kama mfanyabiashara unapaswa kabla ya kuanza kuifanya biashara yako kufahamu kwa uhakika wateja wale unaotaka kuwauzia biashara yako. Kwa kifupi kabisa unatakiwa kufanya utafiti ili kujua bidhaa au huduma utakazouza, wateja wake ni kina nani. Kuna njia nyingi unazoweza kuzitumia ili kuweza kuwajua wateja wa biashara utakayoifanya na kubwa ni ile ya kuangalia ni matatizo gani yanayosumbua sana watu kisha wewe ukaja na suluhisho la matatizo hayo.



Katika biashara ya umachinga unaweza ukawatambua wateja wako aidha kwa kuifanya biashara hiyo na kupata uzoefu kidogo au pia unaweza kuwatambua wateja kwa kuwauliza wafanyabiashara wengine wanaofanya biashara ya umachinga kama unaotarajia kuifanya.

Kila biashara huwa ina kundi fulani la wateja ambalo wewe mfanyabiashara ndiye unayepaswa kulijua kulingana na biashara yako unayoifanya. Kwa mfano ikiwa unauza nguo za watoto, basi wateja wako wakubwa watakuwa ni kina mama hasa wale waliokuwa na watoto wadogo.

Ukitaka kutambua mteja wako kwanza fahamu wewe unauza kitu gani na kitu hicho kitawafaa au kuwanufaisha watu wa aina gani hasa. Hivyo utakapokutana na mtu wa kundi hilo unalolilenga basi moja kwa moja utajua kuwa mtu huyo ana uwezekano wa kuwa mteja wako.


Mara nyingi wateja wenyewe huwa hawafahamu kabisa ni kitu gani wanachokitaka mpaka pale watakapogundua kuwa kuna mtu mwenye suluhisho la tatizo fulani linalowakabili, kwa hiyo wewe ng’ang’ana zaidi na kutambua shida za watu kisha watafutie suluhisho la shida hizo na hapo moja kwa moja utakuwa umeshatambua wateja wako ni akina nani.

Ukiwajua wateja wako itakuwa rahisi zaidi kuwauzia kuliko kubahatisha sokoni kama mtu anayejaribu kukamata senene gizani. Kama mmachinga ukishawafahamu wateja wako vizuri utakuwa ukifanya biashara yako kwa malengo na utakuwa tofauti na wamachinga wengi wanaozunguka wakibahatisha wateja mitaani. Zunguka mtaani lakini ungali ukijua kabisa unawafuata kina nani kwenda kuwauzia, si kila mtu ni mteja wako.

Asante sana ‘Y’, ni matumaini yangu kuwa majibu haya yatakuridhisha,  na ikiwa bado basi unaweza kuuliza zaidi illimradi maswali yawe mafupi.

0 Response to "JINSI YA KUMTAMBUA MTEJA KATIKA BIASHARA YA UMACHINGA (NAOMBA USHAURI)"

Post a Comment