MKATABA WA WAMILIKI WA BIASHARA / KAMPUNI: UMUHIMU WAKE NA JINSI YA KUANDIKA | JIFUNZE UJASIRIAMALI

MKATABA WA WAMILIKI WA BIASHARA / KAMPUNI: UMUHIMU WAKE NA JINSI YA KUANDIKA


WCB chini ya Diamond platnumz wakisaini mkataba wa makubaliano ya kibiashara
Kuandikiana mikataba siyo kwenye biashara ndogondogo tu peke yake bali ni jambo muhimu sana hata katika biashara kubwa za mamilioni ya shilingi. Bila ya mkataba wa makubaliano biashara haziwezi kuendelea mbele, migogoro na kutokuelewana kunaweza kuzuka baina ya wenye hisa, wamiliki wa kampuni, wafanyakazi, waajiri, wateja, wasambazaji bidhaa au wadau wengine wowote wale kwenye biashara.


Mkataba ni andiko muhimu linaloikinga biashara dhidi ya migogoro isiyotakiwa inayoweza kujitokeza ndani ya kampuni /biashara

Vitu vinavyounda mkataba baina ya wenye hisa au wabia wa biashara
1.   Haki na wajibu wa kila mwenye hisa. Mkataba ni lazima ueleze bayana kila mmiliki atakuwa na jukumu gani na wajibu kwa niaba ya kampuni.

2.   Utaratibu wa kutatua migogoro endapo itatokea. Migogoro inaweza ikasababishwa na kukosa uzoefu, au tofauti ya kimaono jambo linaloweza kusababisha wabia kushindwa kukubaliana kwenye mambo kama vile ya usimamizi wa fedha, uongozi nk. Hapa mkataba wa ubia utazuia yote hayo kutokea

3.   Mpango wa kuondoka(Exit strategy)
Mwanahisa anaweza asiridhike akaamua kujitoa njiani au biashara inaweza isiweze kutengeneza faida ikavunjika nk. Je mtafanyaje-fanyaje? Ni lazima kuwe na mpango wa mapema. Imeshuhudiwa makampuni mengi hata hapa Tanzania kampuni kama ile ya Wasafi Classic chini ya mwanamuziki nguli na tajiri Diamond Platinumz (Naseeb Abdul). Watu walimlaumu sana Diamond na kampuni yake kwamba ni wabinafsi, hawapendi maendeleo ya wengine nk. pale wamiliki wa WCB Wasafi walipowataka wanamuziki wake kulipa fidia ya mamilioni ya fedha walipotaka kuvunja mkataba na kampuni hiyo.

Kitu kikubwa kilichofanyika pale ni hiki ninachokizungumzia hapa leo. Hivyo unaweza kuona kwamba mikataba kwenye biashara ina maana na umuhimu mkubwa sana vinginevyo mtu anaweza tu kujitoa kienyeji baada ya kuona pengine alichokuwa akikitafuta keshakipata na hii imewafanya waanzilishi wengi wa biashara hasa hasa hizi za ubunifu kama Sanaa kuishia kuwa hohehahe au hata kufa wakiwa masikini wa kutupa baada ya watu waliowakaribisha kwenye biashara zao kupata ujanja na kuota mbawa kabla ya kurudisha kwenye kampuni kile walichokubaliana au kilichotazamiwa.

Wakati huohuo wao wanakuwa wameshakipata kile walichostahili kama umaarufu au malipo ya fedha. Mkataba wa wasanii ikiwa utawekwa kabla utasaidia sana kuondoa shida kama hizi. Ni sawa na uonavyo kwenye mpira, mkataba wa wachezaji ni lazima usainiwe kabla timu haijaanza ligi vinginevyo utakuta mchezaji mmoja kwa mfano unaweza kukuta amesaini timu ya simba kumbe tayari alikuwa keshasaini tena timu ya Yanga na hili linaweza kusababisha hata timu kupewa adhabu na chama cha soka TFF


Mbali na vitu hivyo 3 nilivyovitaja hapo juu mkataba unaweza ukawa rahisi tu au pia unaweza ukawa na vitu vingi kutegemeana na ukubwa wa kampuni au biashara. Mkataba kwa undani unaweza pia ukawa na vitu vya ziada vifuatavyo;
·      Taratibu za uendeshaji wa kampuni
·      Sera za uuzaji wa shea za kampuni
·      Sera za kulinda wale wenye hisa chache kwenye kampuni
·      Aina za shea kampuni inazotoa nk.

Tanzania watu wengi huogopa sana kuunganisha nguvu kuanzisha kampuni au biashara za ubia kutokana na kutokuelewa umuhimu wa kuwekeana mikataba. Kukiwa na mkataba wa makubaliano baina ya wenye hisa au wabia katika kampuni au biashara hakuna kitakachoweza kuja kwenda mrama maana kila kitu huwekwa wazi kabla biashara haijaanza kufanya kazi.


Kuunganisha nguvu za mitaji ni njia bora zaidi ya kujinasua na tatizo la ukosefu wa mitaji na katika nchi za wenzetu zilizoendelea kama vile China na nyinginezo watu baada ya kubaini umuhimu wa mikataba kwenye makubaliano ya kujenga ubia wamepiga hatua kubwa sana na hauwezi tena kuwasikia wakilialia kukosa mitaji ya kuanzisha biashara zao.

Siku hizi biashara nyingi ni zile ndogondogo na za kati, na ndizo zinazoongoza katika ubunifu, ukuaji kiuchumi na kuchangia katika kuondoa tatizo sugu la ajira. Takwimu zinaonyesha zaidi ya asilimia 90% ya makampuni yote Duniani ni kampuni ndogondogo na za kati(SME’s). Unaweza ukafikiria kama hali ndiyo hiyo basi kuanzisha biashara ndogo ni jambo endelevu na rahisi sana lakini kumbe siyo kweli hata kidogo kutokana na tatizo la kukosekana mitaji ya kutosha kuanzisha biashara. Tatizo hili linahitaji mbinu mbalimbali za kijasiriamali kulitatua ikiwemo hii ya kuunganisha nguvu watu wawili au zaidi ambayo ndiyo njia rahisi na nyepesi zaidi ya nyingine zote ya kupata mtaji wa kuanzisha biashara ndogondogo


Biashara inapokuwa inaendeshwa chini ya ubia wa watu wawili au zaidi kunakuwa na uwezekano mkubwa wa kuibuka kutokuelewana kati yao hasa pale biashara inapoanza kutengeneza faida. Ni muhimu kuwa na mkataba utakaowahusu wanahisa/wawekezaji kukubaliana jinsi kampuni itakavyoendeshwa na mkataba huo unatakiwa kuandaliwa vizuri na mwanasheria au mtu anayeelewa mambo ya mikataba vizuri.

Wajasiriamali ni wepesi sana kudai kuweka mikataba kwenye mambo mengine mbalimbali mfano wanapotaka kupanga chumba au eneo la biashara, wanapouziana mali kama kiwanja au nyumba na mtu mwingine au hata pale wanapotaka kuajiri mfanyakazi / wafanyakazi lakini husahau mkataba muhimu sana pale wanapounganisha nguvu kama wabia au wanahisa kwenye biashara/kampuni. Pengine ni kutokana na Watanzania wengi kuhusisha ndugu wa karibu, jamaa au marafiki pale wanapotaka kuungana kibiashara jambo linalowafanya waone hamna haja ya kuwekeana mikataba kama watu wasiojuana.


Mfano mwingine ni ule wa wafanyakazi na mabosi wao (waajiri) katika biashara ndogo mara nyingi sana watu wanakuwa wakipeana kazi kienyeji sana bila ya kuwa na mkataba wa wafanyakazi wowote unaoainisha namna mambo yatakavyokwenda na matokeo yake ni kuja kuibuka sintofahamu kubwa, mfanyakazi anaweza kuihujumu biashara pasipo mmiliki kuwa na uwezo wa kumwajibisha na wakati mwingine pia tajiri kumhujumu mfanyakazi wake bila ya mfanyakazi huyo kuwa na chohcote kile cha kufanya. Lakini kama kunakuwa na mkataba kabla ya kila kitu mambo yanaweza kutatuliwa kwa haki na usawa bila manunguniko kutoka upande wowote.

Katika Ulimwengu wa biashara na ujasiriamali kuna mikataba ya aina nyingi nyingine ukiacha huu wa wamiliki au wabia kwenye biashara, kuna mkataba wa makabidhiano ya mali, mkataba wa wapangaji, makataba wa ujenzi wa nyumba, mkataba wa ukodishaji mali au chochote kile.


Na hata mkataba wa wafanyakazi wa ndani ambao watu wengi hudhania tu kirahisirahisi kwamba kwa vile mfanyakazi wa ndani pengine kamtoa kijijini basi hamna haja ya mkataba wa maandishi naye, kumbe mkataba huo unaweza hata kuja kumlinda mwenyewe tajiri, hebu fikiria kwa mfano mfanyakazi anakuja kujanjaruka na kula njama na majambazi wanakuibia kila kitu ndani, ikiwa ulikuwa huna mkataba wowote naye unadhani ni nani atakayekusikiliza ukienda kulalamika huko kwenye vyombo vya sheria?

Si watakuhoji mkataba wa mfanyakazi  uko wapi, ukikosa na wewe wanakupuuzilia mbali kwa kuwa ulikuwa ukimtumikisha mtoto wa watu kinyume cha sheria akaamua na yeye kukukomesha?

HITIMISHO

Ukitaka kufanya biashara ya kisasa katika karne hii ya 21 iwe ni biashara ndogo au hata biashara kubwa, usikubali kamwe kufanya makubaliano yeyote yale ya kibiashara hasa ukiwa wewe ndiye mmiliki wa biashara au kampuni kienyeji bila ya kusini mkataba wa kisheria utakuja kulia, na siyo lazima kumshirikisha mwanasheria au wakili, mikataba mingine inahitaji tu mashahidi au ushahidi ili pindi mgogoro ukizuka basi kuwe na ushahidi wa kile mlichokubaliana pande mbili. Ukiona upande wa pili hautaki mkataba basi achana naye mapema.

………………………………………

Kwa vitabu na Michanganuo ya Biashara mbalimbali tembelea duka letu mtandaoni la SMART BOOKS TZ

0 Response to "MKATABA WA WAMILIKI WA BIASHARA / KAMPUNI: UMUHIMU WAKE NA JINSI YA KUANDIKA"

Post a Comment