SEMINA SIKU YA 1: KAMPUNI/BIASHARA, HUDUMA/BIDHAA NA SOKO(JANE RESTAURANT) | JIFUNZE UJASIRIAMALI

SEMINA SIKU YA 1: KAMPUNI/BIASHARA, HUDUMA/BIDHAA NA SOKO(JANE RESTAURANT)

Mgahawa wa Jane Restaurant
Kwanza kabisa hebu tujikumbushe maana ya Mpango wa biashara ni nini. Kwa mujibu wa kitabu chetu cha MICHANGANUO YA BIASHARA NA UJASIRIAMALI ambacho naamini kila mtu hapa katika group letu anacho, Mchanganuo wa Biashara una maana hii hapa;

Mchanganuo wa biashara au mpango wa biashara kwa kimombo (Business plan) ni maandishi yanayoelezea kila jambo kuhusu biashara unayoiendesha, mambo hayo ni, malengo, mikakati, bidhaa/hudumu utakayouza, soko (wateja), shughuli mbalimbali za masoko na uongozi, gharama, mahitaji, na masuala yote yanayohusiana na fedha.

 

Au maana nyingine unaweza ukasema hivi;

 

Mchanganuo wa biashara ni dira au ramani ya biashara yako kuonyesha unakotoka na unakokwenda

 

Sasa tunaanza anzaje kuandika mchanganuo wetu?


Ili uweze kuaandika mchanganuo wa biashara yeyote ile kitu cha kwanza kabisa cha kufanya ni UTAFITI WA HIYO BIASHARA, wengine husema UTAFITI WA SOKO


Kwa kifupi kabisa Utafiti wa biashara unayotaka kuiandikia mchanganuo mfano hii yakwetu ya Mgahawa, unapaswa kuchunguza mambo mbalimbali yanayoihusu biashara hiyo kuanzia Wateja(soko), Washindani, Bidhaa, Eneo la biashara, Mahitaji ya pes(mtaji) na kila kitu kinachohusiana na biashara ya Mgahawa. Mchakato wa utafiti au upembuzi yakinifu umeelezewa kwa kina kwenye Kitabu hicho, hapa tutagusa zile pointi muhimu tu.

 

Njia nyepesi ya kufanya utafiti ni kwa kuwauliza maswali wateja watarajiwa kwa mfano unaweza kuwauliza wanapendelea zaidi aina gani za vyakula (menu), ni nini kinachowaudhi wanaponunua kutoka kwenye migahawa iliyokuwepo na pia unaweza kuchunguza katika eneo unalotarajia kuweka mgahawa wako kuna idadi ya wateja wangapi kwa makisio nk.


Nenda mjini maduka yanayouza vifaa vya migahawa uliza bei zake, nenda sokoni uliza bei za vyakula na viungo mbalimbali uwe nazo zote.

 

Njia nyingine ya kutafiti soko/biashara yako ni kwa kusoma machapisho mbalimbali kuihusu pamoja na kufuatilia vyombo vya habari vinasemaje juu ya biashara hiyo ama sekta nzima inayohusiana na hoteli na migahawa. Majibu utakayoyapata kutokana na utafiti wako au uelewa wa kina wa biashara hii vitakusaidia uweze kupata kitu cha kuandika katika mchanganuo wako vinginevyo utakuwa ukisimulia hadithi ambayo haina uhalisia.

 

Sasa tuchukulie (tuassume) kwamba tumekwishafanya utafiti wetu na tayari tumekwishafahamu ‘nje ndani’ kuhusiana na biashara hii ya mgahawa, soko tunalolenga (wateja), mahitaji yote yanayotakiwa ili uweze kuanza, bidhaa ikiwemo jinsi ya kupata malighafi mbalimbali na bei zake zote pamoja na washindani wanaokuzunguka udhaifu na nguvu zao. Baada ya hatua hii saa tupo tayari kuanza kuandika MCHANGANUO WETU.

 

Ili tuweze kuwa na lengo (focus) tutaweka katika karatasi vipengele vyote vinavyounda mpango mzima wa biashara ili tuandike kipengele baada ya kipengele, hii itatusaidia kuweka nguvu (concetration) kwenye kipengele kimoja mpaka kiishe ndipo tuhamie kingine.  Kwahiyo tutaongozwa na vipengele hivyo kwenye kila hatua tutakayopita.

1.0 MUHTASARI

2.0 MAELEZO YA KAMPUNI

3.0 MAELEZO YA BIDHAA/HUDUMA

4.0 TATHMINI YA SOKO

5.0 MIKAKATI NA UTEKELEZAJI

6.0 UTAWALA NA NGUVUKAZI

7.0 MPANGO WA FEDHA

8.0 VIELELEZO   

Ingawa kipengle cha kwanza kinaonekana ni MUHTASARI, lakini hatutaanza nacho huwa kinakuwa cha mwisho kabisa, Kwa hiyo tutaanza moja kwa moja na cha pili, MAELEZO YA KAMPUNI ambacho nacho kinakuwa na vipengele vyake vidogo chini yake. Tungeliweza kuanza na kipengele kingine chochote kile hata cha soko na si lazima kiwe hiki.

 

2.0 MAELEZO YA KAMPUNI / BIASHARA

Maelezo kuhusu Biashara / kampuni kwa kiasi kikubwa yanahusu taarifa za ndani ya biashara zaidi kuliko kutoka nje ya biashara. Hapa chini naorodhesha vipengele vidogo nitakavyozingatia wakati nikiandika kipengele hiki kikubwa, kwa ujumla tutatoa maelezo kulingana na vipengele hivi vidogo. Siyo lazima kuandika juu ya kila kipengele kwani itategemea biashara inahitaji kitu gani, kama kitu hakina umuhimu hukiweki

 

2.1 Dhamira kuu (mission)

2.2 Vision (Maono)

2.3 Malengo (Objectives)

2.4 Siri za mafanikio

2.5 Umiliki

2.6 Jina

2.7 Usajili

2.8 Kianzio

2.9 Eneo na vifaa vilivyopo.


Aya ya kwanza inayoanza na namba “2.0 Maelezo ya biashara/kampuni” huandiki chochote kwanza panabaki wazi  kwani ni muhtasari mdogo wa vipengele hivyo vingine vidogo vidogo chini yake.


“2.1 Dhamira kuu”

Dhamira kuu ni ile biashara unayoifanya. Kwa mfano sisi hapa tutasema hivi;, “Kutoa  huduma bora ya chakula na vinyaji vyenye afya kwa wateja  katika mazingira rafiki na ya kuvutia

2.2 Maono
Maono ni picha ya biashara yako unayotaka uione baada ya kipindi fulani kupita, mfano tungeweza tukasema hivi “Kuja kuwa na mgahawa mkubwa zaidi jijini Da es salaa” lakini katika mchanganuo wetu huu hatujaweka kipengele cha maono.

 

2.3  Malengo
Hapa tunataja vile vitu tunavyokusudia kuvitimiza baada ya kutekeleza mpango wetu. Malengo mazuri ni lazima yawe halisi, yanayopimika, yenye kutekelezeka na yaliyokuwa na muda maalumu wa utekelezaji. Nayataja baadhi hapa chini;

 

·       Kuongeza mauzo kwa asilimia 10% kila mwaka kwa kutoa chakula na vinywaji bora.

 

·       Kuongeza idadi ya wafanyakazi kutoka 10 mpaka 12 ifikapo mwaka wa 4

 

2.4 Siri za mafanikio.
Hapa tutaorodhesha yale mambo tutakayoyapa kipaumbele katika biashara yetu kusudi tuweze kufanikiwa, nayo ni;

·       Kudumisha usafi na afya katika mazingira yote ya mgahawa

·       Ubora na uhalisia katika vyakula na vinywaji.

·       Mazingira mwanana na rafiki.

 “2.5 Umiliki na historia ya biashara”

Hapa tunataja jina la biashara ambalo ni “Mgahawa wa Jane”, majina ya wamiliki ambao ni Bibi Janeth Mwalugaja na Bibi Grace Lyimo. Tutaelezea na historia ya biashara ilivyoanza.  Katika kipengele hiki kidogo, tutataja pia eneo biashara itakapokuwa ambalo ni Kijitonyama Sayansi jijini Dar es salaam

 

“2.6 Kianzio

Biashara hii japo siyo mpya lakini imefanyiwa mabadiliko makubwa mno kiasi cha kuwa kama ni biashara inayoanza hivyo tutaichukulia kama biashara mpya.

 

Hapa tutaorodhesha kwenye jedwali mahitaji yote tukianza na gharama mbalimbali mpaka assets zitakazohitajika. Namba tutakazozitumia hapa zitatokana na utafiti ule tulioufanya pale mwanzoni mfano gharama za usajili, malighafi na vifaa. Chini yake tutaweka Jedwali la mali na madeni.

 

Baada ya kumaliza sasa tutarudi pale mwanzoni katika aya tuliyoiacha wazi kwenye namba “2.0 Maelezo ya Biashara.” Ilipoanzia sura yetu hii. Tutachagua katika kila kipengele kidogo tulichokwisha andika mstari mmojammoja au maneno muhimu na kuyapanga katika hii aya kutengeneza muhtasari mdogo wa kipengele au sura nzima.

 

2.7 Maombi ya fedha (fund request)

Kama unafuatailia makala hizi tokea mwanzo, kuna mahali nilisema kuwa unapoandika mchanganuo wa biashara kwa ajili ya kuombea fedha mahali iwe ni mkopo au hata uwekezaji unatakiwa katika mchanganuo wako uweke kipengele rasmi cha maombi hayo. Hamna mahali mahsusi kinapokaa lakini ni vizuri kukiweka katika sura ya Kampuni/biashara kwenye kianzio au katika kipengele cha fedha.

 

Fund Request / Maombi ya mkopo ni andiko linaloweza kusimama peke yake bila ya kujumuishwa kwenye mchanganuo kamili wa biashara na ukalipeleka kama lilivyo kwa mkopeshaji wako na unapoandika kipengele hiki ndani ya mchanganuo wa biashara basi kinakuwa ni sehemu ya mpango huo na hakitakuwa na vitu vingi sana kama vile umeamua kukiwakilisha kikiwa chenyewe kama kilivyo.

 

Kipengele hiki unatakiwa kuweka mambo yafuatayo;

 

Maelezo ya buiashara yako kwa kifupi

Ikiwa maombi ya mkopo ni sehemu ya mchanganuo wa biashara basi hapa hutaandika kwa kirefu kwani tayari maelezo ya biashara unakuwa umeshayaandika kwa kirefu kwenye sura inayohusu biashara kwenye mpango wako lakini ikiwa maombi ya mkopo unayapeleka yenyewe kama yalivyo kwa mkopaji basi ni lazima uandike kwa kina zaidi.

 

Kiasi cha fedha unachoomba.

Hapa unataja ni kiasi gani unahitaji kwa sasa na hata baadae unatarajia kuhitaji kiasi gani pia.

 

Matumizi ya fedha hizo ni nini?

Je ni kwa ajili ya mtaji wa kuendeshea biashara? Kununulia vifaa, mashine au majengo? Kulipia pango, Kununulia malighafi au Ni kwa ajili ya kutangaza biashara yako? Chochote kile utakachoombea pesa eleza kitagharimu kiasi gani kila kimoja.

 

Dhamana za mkopo

Orodhesha vitu unavyotarajia vitakuwa dhamana ya kulinda mkopo wako ikitokea umeshindwa kulipa.

 

Jinsi utakavyoulipa mkopo wako

Eleza unatarajia kulipa katika muda gani, riba ni kiasi gani na marejesho ya mkopo kiasi gani kwa mwezi nk. Ikiwa maombi ya mkopo ni andiko linalojitegemea siyo sehemu ya mpango wa biashara itakubidi hapa uweke mahesabu kwa kirefu kidogo lakini ikiwa ni sehemu ya mpango wa biashara tayari basi utaandika tu kwa kifupi kwani Mahesabu yatakuwa yameshaonyeshwa kwa kirefu katika sura yenyewe ya fedha.

 

Na hapa ndio mwisho wa kipengele chetu hiki cha Maelezo ya Biashara

 

3.0 MAELEZO YA BIDHAA / HUDUMA

Katika sura ama kipengele hiki cha maelezo yanayohusu bidhaa au huduma, hapa ndipo unapotakiwa utoe maelezo ya ndani kabisa yanayohusu kile kitu biashara yako inachouza. Kwa biashara yetu hii ya Mgahawa wa Jane bidhaa zetu kubwa ni vyakula na vinyaji baridi.


Kama ilivyo kwa vipengele vingine vikubwa vinavyounda mpango mzima wa biashara, hiki nacho kina vipengele vyake vidogovidogo kadhaa ambavyo ndivyo tutakavyoelekeza nguvu zetu kwake. Vipengele vidogo ni hivi;


3.1 Maelezo ya bidhaa/huduma

3.2 Utofauti/upekee wa bidhaa/huduma na za

washindani

3.3 Vyanzo vya malighafi/bidhaa

3.4 Kopi za matangazo

3.5 Teknolojia

3.6 Bidhaa au Huduma za baadae


Kwahiyo maelezo yetu kwenye kipengele hiki yatajikita katika mada hizi ndogondogo hapo juu. Hata hivyo siyo sheria wala lazima kuweka vipengele vyote kwenye Sura yako, unaweka tu kipengele unachoona kinafaa kulingana na mazingira ya biashara yako yalivyo lakini angalao kuna vipengele kwa mfano “Maelezo yenyewe ya bidhaa/huduma" ni lazima yawepo.


Kama tunavyoona kwenye mchanganuo wetu huu wa mgahawa wa Jane siyo vipengele vyote vidogo vimeelezewa. Kwa mfano hapa utaona ni maelezo ya bidhaa tu kwenye muhtasari halafu chini yake kuna Bidhaa za baadae na Tathmini ya NUFUVI ambayo hata haipo kwenye vipengele vyetu pale juu.

 

Unaweza kuandika maelezo mafupi tu (Muhtasari) kuhusiana na bidhaa zako kama aya mbili au tatu hivi pasipo kuorodhesha kila kipengele na maelezo yake. Lakini katika maelezo hayo hakikisha yanagusa sifa muhimu za huduma au bidhaa zako pamoja na upekee wake.


4.0 TATHMINI YA SOKO

Tathmini ya soko nayo imegawanyika katika vipengele vidogovidogo kadhaa ambavyo vyote ili uweze kuviandika unahitaji kupata takwimu na taarifa mbalimbali nje ya biashara yako zinazohusiana na soko au wateja watarajiwa, sekta ya biashara uliyopo pamoja na ushindani.

 

Taarifa hizi na takwinu mbalimbali kama tulivyoona pale mwanzo niliposema ni lazima kabla hujaanza kwanza ufanye utafiti wa soko, hapa ndio mahali penyewe hasa pa kuzitumia taarifa tulizopata kwenye ule utafiti


Vipengele vidogo kwenye sehemu hii ya Soko ni hivi vifuatavyo;


4.1 Mgawanyo wa soko
4.2 Mkakati wa soko lengwa
4.2.1 Mahitaji ya soko
4.2.2 Mwelekeo wa soko
4.2.3 Ukuaji wa soko
4.3 Tathmini ya sekta
4.3.1Washiriki katika sekta
4.3.2 Usambazaji ulivyo
4.3.3 Vigezo vya ushindani
4.3.4 Washindani wakuu

Hata hivyo kama tulivyokwishaona huko nyuma wingi wa vipengele hivi utategemea mpango wako wa biashara ni kwa ajili ya nini. Ikiwa katika mpango wako wa biashara kitu fulani hakina umuhimu basi huna haja ya kukiweka. Kwahiyo unaweza kukuta katika vipengele vyote vidogo vilivyotajwa hapo juu pengine unaweka viwili, vitatu au hata vyote kulingana na aina ya mchanganuo unaoandika, urefu au aina ya biashara unayoandikia.

 

Kwa upande wa biashara yetu hii ya Jane Rstaurant, kwenye tathmini ya soko kama kawaida kuna muhtasari pale mwanzoni kabisa ambao umeandikwa mwishoni baada ya kukamilisha vipengele vingine vyote vidogovidogo.


Ngoja sasa tuangalie vipengele vidogo jinsi vilivyoelezewa,


4.1 Mgawanyo wa Soko.

Katika mgawanyo wa soko tutataja ni makundi mangapi ya wateja watarajiwa ambapo hapa yametajwa kuwa ni;

 

1. Wafanyakazi katika taasisi binafsi na za serikali

2. Wamiliki wa Biashara.

3. Wakaazi wenye umri zaidi ya miaka 18 wanoishi peke yao.

 

Kila kundi tunaelezea sifa zake za ‘kidemografia’ mfano umri, jinsia, na hata tabia zao zinazowatofautisha kundi moja na jingine.

 

4.2 Mkakati wa Soko Lengwa.

Ni kipengele kingine kidogo kilichopo katika Sura au kipengele kikubwa cha SOKO kwenye mchanganuo huu wa Jane Restaurant, wamiliki wake waliamua kulenga makundi yote matatu, Wangeliweza pia kulenge kundi moja tu au mawili lakini kulingana na utafiti wao wameona makundi yote 3 ni muhimu kwao.

 

Unaweza pia kuelezea jinsi utakavyohudumia kila kundi, kwa mfano Jane wameeleza ni kwa namna gani watahudumia makundi hayo matatu.

 

4.3 Tathmini ya Sekta.

Kwenye tathmini ya sekta tutaeleza ni sekta ipi biashara hii inaangukia ambapo ni sekta ya Hoteli na Migahawa. Kwa kawaida hapa unaweza kueleza jambo lolote lile “linalotrend” kuhusiana na sekta husika pamoja na kutaja wahusika mbalimbali kwenye hiyo sekta, kwa mfano kwenye hoteli na migahawa tutasema, “Sekta hii imegawanyika kwa kiasi kikubwa sana na inajumuisha wauzaji wadogowadogo wa vyakula maarufu kama mama na baba lishe, vituo vya chipsi (fast foods), cafeteria, mabaa, wapikaji kwenye shughuli mbalimbali hadi migahawa mikubwa na hoteli

 

4.3.1 Ushindani.

Katika kipengele hiki tutaelezea hali ya ushindani ilivyo, tutataja washindani wakubwa ambapo kwa upande wa Jane Restaurant wao wamewaweka washindani wao katika makundi 3

 

(1) Washindani wa Moja kwa moja.

(2) Washindani wasiokuwa wa moja kwa moja.

(3) Mama na Baba lishe.


Kwa kila mshindani/kundi tutaelezea nguvu na udhaifu waliokuwa nao  kwa kuzingatia, bidhaa, ubora, bei, usimamizi, hali ya kifedha, kuaminika, mfumo wa usambazaji na teknolojia tukilinganisha na biashara ya Jane Restaurant. Tunaweza pia kueleza na kipande cha soko wanachokilenga na jinsi tutakavyoweza kukabiliana nao.

 

4.3.2 Mahitaji ya Soko.

Kwenye kipengele hiki tunatakiwa kuonyesha ni kwanini soko linahitaji huduma za Jane Restaurant kwa mfano tutasema Dar es salaam hususan maeneo ya Kijitonyama utakapokuwa mgahawa huu, kuna ongezeko kubwa la watu (hapa tungeliweza kuweka hata na takwimu za sensa ya watu na makazi kuthibitisha hilo) Sababu nyingine ni kwamba kila mtu anahitaji kula mlo kamili na wenye afya kigezo ambacho Jane Restaurant ndiyo kaulimbiu yao.

 

4.3.3 Mwelekeo wa soko.

Katika mwelekeo wa soko tutaeleza sababu inayoonekana kubadilisha hali ya soko au biashara. Kwa mfano tutasema kwamba, “wateja wetu watarajiwa wanaongezeka uelewa katika mitindo yao ya maisha wakitambua kati ya vyakula vinavyoboresha afya na vile vinavyoharibu afya au kuchangia kuleta magonjwa ya tabia”.

Tumemaliza Kipengele (Sura) za BIDHAA na SOKO, kesho tutaendelea na sura za Mikakati & Utekelezaji pamoja na Uongozi. Nitajitahidi kuziweka mchana ili jioni tumalizie na Kipengele cha Fedha

 

Mwishoni nitacompile sehemu zote toka juzi kuwa PDF moja halafu pia nitaweka hapa Mchanganuo huo kamili kwa kiingereza na kwa kiswahili.

 

Unaweza kuona kama ni vigumu kuelewa lakini unapojifunza sehemu ndogondogo kama ninavyoweka hapa mwishowe utaona ni rahisi na utaelewa, huwezi kujifunza siku moja ukaelewa ndio maana tukawa na hili group kusudi kwa kujifunza michanganuo mbalimbali yule mwenye nia ya dhati ya kuelewa aweze kuelewa.


 

FUATILA ZAIDI HAPA

UTANGULIZI WA SEMINA

SEMINA SIKU YA 2

SEMINA SIKU YA 3

SEMINA SIKU YA 4

0 Response to "SEMINA SIKU YA 1: KAMPUNI/BIASHARA, HUDUMA/BIDHAA NA SOKO(JANE RESTAURANT)"

Post a Comment