Jinsi ya kupata wateja wengi kwenye biashara yako kwa kufanya kile wajasiriamali wengi wanachosahau kukifanya. | JIFUNZE UJASIRIAMALI

Jinsi ya kupata wateja wengi kwenye biashara yako kwa kufanya kile wajasiriamali wengi wanachosahau kukifanya.

SUMAKU YA KUNASA WATEJA KWENYE BIASHARA

Sisimulii hadithi bali ni mbinu niliyowahi kuijaribu mwenyewe binafsi na kuona inazaa matunda. Kwa kipindi kirefu nimekuwa natuma Makala mbalimbali za ujasiriamali kupitia e-mail(Jiunge na blogu hii). Katika mirejesho ya wasomaji wangu mara kwa mara sikuwa nikitilia maanani sana ushauri waliokuwa wakinipa wateja wangu hasa kwa upande wa uboreshaji wa Makala zangu nilizokuwa nikiwatumia. Kwa kifupi sikuzingatia kujifunza jinsi ya kuvutia wateja kwenye biashara yangu.


Niliamini kwamba kwa kuwa mimi ndio niliyekuwa nikiziandaa Makala hizo basi hakukuwa na mtu wa kunishauri la kufanya na zaidi ikiwa kama anayenishauri alikuwa ni msomaji wa Makala zangu hizo. Lakini kumbe sikuwa najua kosa kubwa nililokuwa nikilitenda la kuielekeza biashara yangu ‘kaburini’. Kuna wasomaji wengi walinitumia maoni yao wakitaka niongeze vitu kadha wa kadha, wengine wakashauri nipunguze hiki na kile na hata wengine wakawa wananishauri muda sahihi wa kutuma Makala zangu mtandaoni. (Kitu wateja walichokuwa wakinishauri nikifanye sitaweza kukitaja hapa kwa leo kwani ni mada nzima ya siku nyingine inayojitegemea)

SOMA: Jinsi ya kutengeneza mvuto wa ajabu na kupendwa haraka na kila mtu, wapenzi, wateja ndugu na hata jamaa.

Lakini bado nikaweka pamba masikioni na kuendelea kuamini kwamba nilichokuwa nakifanya ndio sahihi na kuendelea kupuuzia kujifunza jinsi ya kukuza biashara ya mtandao. Ilifikia mahali baadhi ya ushauri ukawa unajirudiarudia kila mara kutoka kwa watu tofauti ambao hata hawajuani mpaka nikawa nashangaa ni kwa vipi wameweza kutuma maoni yanayofanana, wamejuaje? Au labda kuna namna nilikosea nikatuma meseji yenye maudhui yanayofanana na swala hilo kwa wasomaji wangu, lakini nilipochunguza nikagundua wala hakukuwa na uhusiano wowote baina ya wasomaji waliokuwa wakinitumia maoni yao.

Sasa kidogo nilianza kushituka na kuanza kufuatilia kwa karibu maoni yote ya wasomaji wangu bila kuruka hata mmoja huku nikitendea kazi yale yote waliyonishauri na kuona yanafaa. Baada ya muda kidogo kupita nilipata mshangao mkubwa! Moja ya maoni yaliyojirudiarudia sana katika mirejesho ya wasomaji wangu na nikayafanyia kazi yalianza kutoa matokeo mazuri ya kushangaza. Nilishuhudia ongezeko kubwa la wafuatiliaji wa kazi zangu zilizohusiana na mawazo yale. Watu wengi walilipenda sana wazo lile. Kidogokidogo nikajikuta naanza kufahamu jinsi ya kupata wateja mtandaoni

SOMA: Jinsi ya kuendesha biashara ya duka la rejareja(Hatua 6 za kuanzisha biashara ya rejareja)

Nilichokifanya kupata wateja wengi zaidi haikuwa sayansi ya roketi wala ile ya kwenda mwezini bali nilichofanya ni KUKIVAA KIATU CHA MTEJA, niliamua kuvaa viatu vya wateja wangu nikajifanya kama vile na mimi ningelikuwa msomaji wa makala zile ni vitu gani ningelipendelea mwandishi awe anaandika kwenye makala anazotuma mara kwa mara.

Baada ya kugoma kuchukua hatua kwa kipindi kirefu ya kujua jinsi ya kukuza biashara yangu, hatimaye niliamua kufanya kitu ambacho nafikiri pia hata wajasiriamali wengi na wafanyabiashara wadogo husahau kukifanya. Wanahangaika sana kutafuta wateja kwa tabu huku wakikosa fursa kubwa za kupata pesa. Kwanini? Ni kwa sababu wajasiriamali hao wanaamua kumfikiria mtu mmoja tu kwenye biashara zao na mtu huyo siyo mwingine bali ni wao wenyewe(Wewe/mimi nk.)

SOMA: Jinsi ya kukuza biashara ya duka lako(Makosa 12 yatakayofukuza wateja dukani kwako na kudhani umelogwa)

Ili uweze kupata wateja wengi kwenye biashara yako unatakiwa kila siku ya Mungu, katika kila hatua ya biashara yako unayopitia ujiulize swali hili lifuatalo; “KITU HIKI NIFANYACHO NI SAHIHI KWELI KWA WATEJA WANGU?”  Swali hili linapaswa liwe moja kati ya nguvu kubwa zinazochochea maamuzi yako yote kwenye biashara yako kwani ndio kiini hasa cha watu wanaofanikiwa kujua jinsi ya kutafuta masoko ya biashara zao kwenye kila aina za biashara wanazozifanya.

Katika makala hii nimetumia mfano wa biashara  ya kwangu mwenyewe ya mtandaoni lakini zipo aina za biashara nyingi nyingine, haijalishi aina ya biashara unayoifanya, maoni na mirejesho ya wateja huja kwa staili tofauti na unatakiwa kulingana na aina ya biashara yako basi utambue ni kitu gani wateja wnachosema juu ya biashara yako ili uweze kukifanyia kazi au kuboresha zaidi.

Nakusihi ndugu msomaji endelea kuwa nami kwenye kila Email ninazokutumia mara kwa mara na moja kati ya hizo nitakuja kukuelezea exactly kile wateja wangu walichokuwa wakikirudiarudia kwenye maswali na mirejesho yao kwangu, kikanifanya hadi kubadilisha moyo wangu uliokuwa mgumu kama jiwe kutekeleza kile walichokuwa wakikitaka wao na hatimaye mimi kupata faida.

SOMA: Mmiliki biashara ya kuuza nyama na samaki agundua siri ya kupata wateja wengi wa kipato cha chini.

Kwa sasa wewe endelea tu kufikiria kuhusiana na WATEJA WAKO, Je, unatenda kwa namna inayowapatia faida wateja wako? Kama siyo, bado nafasi ya kubadilika ipo, badilika sasa kwani ukiwapatia FAIDA na wao watakurudishia FAIDA kwenye biashara yako.

...................................................



v Kujipatia vitabu vyetu mbalimbali na Michanganuo ya Biashara fungua duka letu la Vitabu na Michanganuo mtandaoni hapa.

v Kujiunga na group letu la Whatsapp pamoja na Telegramu kupata masomo ya fedha kila siku na michanganuo, lipia sh. elfu 10 na utume ujumbe wa "NIUNGANISHE NA GROUP PAMOJA NA OFFA YA VITU 7" kupitia namba yetu ya wasap: 0765553030

0 Response to "Jinsi ya kupata wateja wengi kwenye biashara yako kwa kufanya kile wajasiriamali wengi wanachosahau kukifanya."

Post a Comment