SEMINA SIKU YA 4: MRADI WA MASHINE YA KUSAGA UNGA SAFI NA SALAMA WA DONA (MCHANGANUO HATUA KWA HATUA) | JIFUNZE UJASIRIAMALI

SEMINA SIKU YA 4: MRADI WA MASHINE YA KUSAGA UNGA SAFI NA SALAMA WA DONA (MCHANGANUO HATUA KWA HATUA)


Leo ni siku ya 5 ya semina yetu hii na tunakwenda kujifunza jinsi ya kuandika hatua kwa hatua sura inayoitwa MIKAKATI NA UTEKELEZAJI. Sura hii pia ni muhimu kwani baada ya kulijua vizuri soko lako ndipo sasa unapanga ni mambo gani utakayoyafanya, mbinu mbalimbali utakazotumia ili uweze kuyafikia malengo uliyojiwekea kibiashara. 

Mathalani umelenga kuwa na mauzo ya shilingi milioni moja katka kipindi cha mwezi mmoja, ni lazima ukae na kujua utatangaza vipi biashara yako hiyo, utauza namna gani na hata utasambaza kwa njia zipi  bidhaa zako. Ili kufahamu kinagaubaga sehemu hii ni vizuri zaidi ukawa na MCHANGANUO HUO WA usado Milling pamoja na Kitabu cha MICHANGANUO YA BIASHARA NA UJASIRIAMALI.


Basi hebu moja kwa moja tukaone USADO Milling mikakati yao waliiweka vipi;


5.0 MIKAKATI NA UTEKELEZAJI
Hebu kwanza kabla ya kufanya chochote tuweke mezani vipengele vidogo vitakavyotuwezesha kuandika sura hii nzima, vipengele hivi ndio dira yetu itakayotuongoza;

5.1 Nguvu za kiushindani
5.2 Mkakati wa soko
5.2.1 Kauli ya kujipanga katika soko
5.2.2 Mkakati wa bei
5.2.3 Mkakati wa matangazo/promosheni
5.2.4 Programu za masoko
5.3 Mkakati wa mauzo
5.3.1 Makisio ya mauzo
5.3.2 Programu za mauzo
5.4 Mkakati wa ushirikiano
5.5 Vitendo na utekelezaji au Uendeshaji

Katika kipengele kidogo cha, “5.5 Uendeshaji” kwenye mchanganuo huu wa USADO hakijawekwa hapo kilipo bali niliamua kukifanya kuwa moja kati ya Vipengele vikuu au SURA inayojitegemea. Hili halina neno na mchanganuo huu utakuwa na Sura 9 badala ya 8 kama ilivyozoeleka mara nyingi kwenye michanganu mingine katika Kitabu chetu cha MICHANGANUO YA BIASHARA NA UJASIRIAMALI.

Mara nyingi sana Vitendo na utekelezaji ama Uendeshaji katika baadhi ya michanganuo ya biashara huwa hakipo au huandikwa aya chache tu kutokana na aina ya biashara hizo kutokuwa na shughuli hizo au kutokuwa na umuhimu wa kuviweka. Lakini biashara kama hii ya kiwanda ni lazima kipengele hiki kiwepo kwani uendeshaji ndiyo shughuli mama na muhimu zaidi.

Basi kama kawaida tunaanza na Muhtasari mdogo wa Sura hii ambao lakini huja kuandikwa mwishoni, kisha nitarukia moja kwa moja kipengele kidogo kifuatacho;

5.1 Nguvu za kiushindani
Kwenye nguvu za kiushindani za USADO Milling nimetaja na kuelezea jumla ya vitu vitatu ambavyo ni UBORA, ENEO na KAULIMBIU yao. Vitu hivi ndiyo USADO wanavyofanya kwa uzuri kuwazidi washindani wao wote na ndivyo wanavyojivunia sokoni.

Kauli ya WANAUME WA DAR HULA DONA kwenye nembo na matangazo yao itakuwa ni ya kipekee na iliyo na uwezo mkubwa wa kuwahamasisha wateja wao walengwa ambao ni wanawake walioolewa wenye umri kuanzia miaka 25 – 60 kununua unga wao kama njugu. Hakuna mwanamke anayependa mume au familia goigoi.

5.2 Mkakati wa soko
Kati ya mikakati mikubwa 2 kwenye sura hii, SOKO na MAUZO, mkakati wa soko umegawanyika katika mikakati midogomidogo 4 ambayo ni mkakati wa kujipanga kwenye soko (Positioning), Matangazo/promosheni, mkakati wa bei na mkakati wa usambazaji. Na yote hiyo imeelezewa vizuri kabisa kama unavyoona kwenye mchanganuo wako huo wa USADO Milling.

5.2.2 Kaulimbiu yetu ya kujipanga sokoni,
Hapa nilielezea jinsi USADO Milling ilivyojipanga katika soko la unga wa dona kama kampuni itakayotengeneza na kusambaza unga safi na salama wa dona kwa lengo la kukidhi mahitaji ya soko lake lengwa. Kujua mahitaji hayo maalumu na ambayo hakuna kampuni nyingine yeyote katika eneo zima la Mikoa ya Pwani na Jiji la Dar es salaa inayoweza kuyakidhi kwa ufanisi kama wao soma kwenye mchanganuo huu kipengele hiki. Hivyo ndivyo USADO ‘walivyojiposition’ kwa wateja wao wawaone na kuwachukulia sokoni.

5.2.2 Promosheni na Matangazo
Kipengele hiki kidogo chini ya mkakati wa soko la USADO Milling nimeelezea kinagaubaga namna ambavyo kampuni ya USADO itafikisha ujumbe kwa wateja wake walengwa kuhusiana na uwepo wa bidhaa yao ya Dona. Nimetaja njia mbalimbali watakazozitumia kama unavyoona lakini pia ningeweza kutaja njia nyingine nyingi zaidi kama wamiliki wangeona zinafaa kulingana na utafiti wao jinsi walivyoufanya.

5.2.3 Mkakati wa Bei
Kwenye soko bei ni kitu muhimu sana na ambacho inatakiwa kuwekewa mkakati madhubuti ili kuweza kuwanasa wateja kwa urahisi. USADO nao hawajabaki nyuma kwani wamehakikisha watatumia mbinu ya kutokupandisha bei kupita washindani wao kusudi wateja waamue kuchagua kununua kwao kutokana na zile faida za ziada wasizoweza kuzipata kutoka kwa hao wshindani wao. Hii yote ni kuhakikisha wateja wasipate kisingizio chochote cha kuukataa unga wao wa dona.

5.2.4 Mkakati wa Usambazaji.
Kwenye usambazaji kitu muhimu walichofanya ni kuhakikisha wanakuwa na kituo kikuu cha usambazaji eneo la kimkakati la Mbezi Mwisho, Mbezi mwisho ni stendi inayofikika kwa urahisi siyo tu kutoka kila kona ya jiji la Dar es salaam na Pwani bali kutoka maeneo mengine yote ya Tanzania yanayolima mahindi kwa wingi na Afrika Mashariki kupitia barabara kuu ya Morogoro.

5.3 Mkakati wa Mauzo.
Kama kipengele kidogo kinachojitegemea katika Sura hii baada ya kile cha mkakati wa soko, mkakati wa mauzo nao una kipengele chake kingine kidogo kinachoitwa, makisio ya mauzo. Katika mkakati wa mauzo kuna mambo makubwa mawili yaliyotajwa pale ambayo yakitekelezwa vizuri mauzo yataongezeka haraka zaidi.

5.3.1 Makisio ya Mauzo na Gharama za Mauzo.
Kama nilivyosema katika kipengele kilichotangulia, Makisio ya mauzo ni kipengele kidogo cha Mkakati wa mauzo na huwa kipengele hiki basi ndipo tunakutana tena kwa mara ya pili na namba baada ya pale mwanzo kama utakumbuka kwenye sura ya 2 ya “Maelezo ya biashara” tulipoona kwa mara ya kwanza namba katika jedwali la Mahitaji ya kuanzia biashara au Mtaji.

Jinsi makisio ya mauzo yalivyofanyika;
Kwanza kabisa nilitambua mauzo yatatokana na vitu gani ambapo kwa USADO Milling vitu vitakavyouzwa ili kuleta mapato vipo viwili 2, unga wa dona pamoja na Mifuko (viroba) baada ya kutumika kubebea mahindi

Tulikisia mauzo ya tani 1 mpaka tani 1.5 kwa wiki, hii inamaanisha kwamba makisio ya mauzo ya unga kwa mwezi (wiki 4) ni tani (1 – 1.5 ) x 4 sawa na tani 4 - 6 kwa mwezi. Hivyo miezi mauzo ni mazuri kabisa huweza kufikia tani 6 na kwa miezi ambayo mauzo ni madogo kabisa tumekisia kuwa ni wastani wa tani 4 kwa mwezi. Bei ya mfuko/kiroba kitupu kimoja ni shilingi 500.

Mauzo huambatana na Gharama za mauzo ambazo kwa USADO gharama za mauzo ni zile zinazotokana na ununuzi wa mahindi kama malighafi, usafirishaji wake pamoja na gharama za kuyahudumia kabla ya kusagwa mfano malipo kwa vibarua wanaopeta mahindi, msagishaji, umeme wa kusagia pamoja na vifungashio.

Katika jedwali kwenye mchanganuo wetu Mauzo na gharama za mauzo vyote vimeonyeshwa vizuri.


Kama chati ya mauzo kila mwezi kwa mwaka 2020 inavyoonyesha hapo juu mauzo ya unga wa dona yanatarajiwa kubadilika kulingana na vigezo mbalimbali mfano miezi ya Mei na Juni mauzo ni makubwa, Agosti yatashuka kidogo na kupanda tena mwezi Januari na Februari. Tofauti hii itasababishwa na vigezo vingi vikiwemo, misimu tofauti, wingi au upatikanaji wa mahindi sokoni, washindani na bei ya unga inayobadilika kila wakati sokoni.

Baada ya kukisia mauzo na gharama zake kila mwezi sasa nahamia mauzo na gharama zake kwa mwaka mzima wa kwanza wa 2020 kisha miaka mingine miwili inayofuata, 2021 na 2022. Mwaka wa kwanza nilipata kwa kujumlisha mauzo ya miezi yote 12 niliyopata pale juu lakini miaka 2 inayofuata nimefanya makisio kwa kutumia asilimia 25% mwaka wa pili na asilimia 50% mwaka wa 3. Ili kuelewa kwa uzuri zaidi nakusihi ufuatilie vyema majedwali na chati zote katika mchanganuo wako kamili wa USADO Milling.

Kufikia hapo ndugu mfuatiliaji wa course hii, nimefika mwisho wa Sura ya 5 iliyohusu Mikakati na Utekelezaji. Lakini kama ulivyoona kipengele cha Utekelezaji au Uendeshaji sikukiweka hapa na nimekipa Sura yake chenyewe kutokana na unyeti wake kwenye aina hii ya biashara ya kiwanda. Hivyo kaa tayari kujifunza kipengele hicho katika Sura inayofuata. Asante sana.


SEMINA SIKU-3                SEMINA SIKU-5



0 Response to "SEMINA SIKU YA 4: MRADI WA MASHINE YA KUSAGA UNGA SAFI NA SALAMA WA DONA (MCHANGANUO HATUA KWA HATUA)"

Post a Comment