SEMINA SIKU YA 6: MPANGO WA FEDHA MCHANGANUO WA BIASHARA KIWANDA CHA DONA (USADO MILLING | JIFUNZE UJASIRIAMALI

SEMINA SIKU YA 6: MPANGO WA FEDHA MCHANGANUO WA BIASHARA KIWANDA CHA DONA (USADO MILLING

Kiwanda cha unga safi na salama wa dona Usado milling
Sura hii ya Fedha ni ndefu lakini ni muhimu katika mpango wa biashara, nimeweka mkazo sana katika Ripoti ya Faida na hasara kwani ndiyo chanzo cha namba katika ripoti nyingine zote mbili za Mtiririko wa fedha(cash flow) na Mizania ya biashara(Balance sheet)

8.0 Mpango wa Fedha
Kama zilivyo Sura nyingine zote zilizopita hii nayo kuna muhtasari mdogo unaogusa zile sehemu muhimu zote za Sura yote. Lakini kabla hatujaendelea hebu kwanza tuone ni vipengele gani vidogo vinavyounda sura nzima ya fedha;

7.1 Dhana/makisio muhimu
7.2 Tathmini ya mauzo ya kurudisha gharama (Break Even Analysis)
7.3 Makisio ya faida na hasara
7.4 Makisio ya mtiririko wa fedha
7.5 Makisio ya mali na madeni (mizania ya biashara)
7.6 Sehemu muhimu za biashara

8.1 Makisio muhimu
Kwenye makisio muhimu nimeorodhesha tu vile vigezo (assumptions) nilizotumia katika kuamua hesabu zangu ziwe vipi. Kwa mfano ukuaji wa mauzo mwaka wa pili na wa tatu nilitumia kigezo cha kuongezeka kwa asilimia 25% na asilimia 50%, haya ni makisio (assumptions) kulingana na tafiti.

Pia kukisia vitu kama wafanyakazi 3 mwaka wa kwanza, kodi ya mapato na riba ya mkopo kama mpango huu ungehusisha mkopo pia vyote hivyo ni makisio muhimu ambayo ningepaswa kuandika hapa kwa kifupi kusudi msomaji wa mpango huu wa USADO Milling atambue hesabu zangu zimefikajefikaje pale zilipo na wala sikuzitoa hewani tu.


8.2 Tathmini ya Mauzo yatakayorudisha Gharama zote kwa mwezi (Break Even Analysis)
Kipengele hiki kidogo ingawa nimekiweka hapa lakini kimsingi kinapaswa kuandikwa baada ya kumaliza kipengele kinachofuata cha Ripoti ya faida na hasara kwasababu data zake zote inabidi zitokane na ripoti hiyo. Hata hivyo nitaeleza namna nilivyokokotoa lakini ukumbuke data hizo zimetokana na kipengele kinachofuata baada ya hiki.

“Break Even Analysis” ni tathmini ya kiasi cha mauzo yanayohitajika ili kurudisha gharama zote zilizotumika katika kipindi fulani, inaweza ikawa mwezi, mwaka au kipindi kingine chochote kile ila mwezi ndiyo hutumika mara nyingi zaidi.

Namba zote zinazotumika kwenye tathmini hii zinapatikana kutoka katika jedwali la Ripoti ya Faida na Hasara, hivyo ni vizuri kuifanya tathmini hii baada ya kukamilisha jedwali hilo.

Ili kukokotoa Mauzo hayo tutahitaji kuwa na vitu 3 muhimu vifuatavyo;
·      Wastani wa gharama za kudumu kwa mwezi
·      Asilimia ya Gharama za mauzo kwenye mauzo
·      Kanuni ya kukokotoa mauzo hayo(Break even Formula)
Katika jedwali la Faida na Hasara wastani wa gharama za kudumu kwa mwezi ni zile gharama za uendeshaji kwa mwezi ambazo ni shilingi 827,000 ukitazama jedwali la faida na hasara kwenye mchanganuo wako wa USADO, nimechukua jumla ya gharama za uendeshaji kwa mwaka sh. 9,924,000 kisha nikagawa kwa miezi 12 kupata za mwezi mmoja.

Asilimia ya Gharama za mauzo kwenye Mauzo, nimechukua jumla ya gharama zinazobadilika za mauzo sh. 55,062,400 kutoka katika jedwali la makisio ya faida na hasara mwaka wa kwanza kisha nikagawa kwa Mauzo ambayo ni sh. 75,942,000. Hizi ukichukua za mwezi au za mwaka asilimia utapa hiyohiyo moja ambayo nimepata asilimia 72.5% au 0.725

Kanuni ya kukokotoa “Break Even Sales” zipo nyingi kulingana na data/taarifa unazopewa, kwa mfano hapa tayari tuna mauzo, gharama za mauzo na gharama za kudumu kama ilivyokuwa kwa ‘case’ yetu hapa nitatumia kanuni ifuatayo;

(Nikisema Break Even sales namaanisha Mauzo ya kurudisha gharama zote zilizotumika yaani mapato yamelingana na gharama, hamna faida wala hasara)

Chati ya mauzo hayo nimeitengeneza kwa kutumia data za “Mauzo vs Faida” na data hizi nimezipata kwa kutumia kanuni (formula) hii hapa chini;

Faida = Mauzo – Gharama za mauzo – gharama za kudumu

Kisha nikatengeneza jedwali la Mauzo vs Faida,

Mauzo
0
5,000,000
10,000,000
15,000,000
20,000,000
25,000,000
Faida
- 827,000
548,000
1,923,000
3,298,000
4,673,000
6,048,000

Lakini kumbuka kila thamani ya gharama za mauzo kulingana na data zetu pale juu ni asilimia 72.5% au 0.725 ya Mauzo

Hivyo Fomula yetu itakuwa kama ifuatavyo

 Faida = Mauzo – 0.725Mauzo – 827,000

Baada ya hapo katika kila chumba nilitafuta thamani ya faida kwa kutumia fomula yetu hapo juu katika kila mauzo, mfano nikiweka 0 kila penye mauzo, faida itakuwa kama ifuatavyo;

Faida = 0 – (0.725 X 0) – 827,000 = - 827,000

Mauzo yakiwa 5,000,000 Faida itakuwa kama ifuatavyo;

Faida = 5,000,000 – (0.725 x 5000,000) – 827,000 = 548,000

Na kuendelea hadi viboksi vyote vya faida kwenye jedwali vimejaa. Sasa Nikichora chati kwa kutumia data zangu hizo utaona mahali faida itakapokuwa 0 ndipo Break even point ilipo na hapo ndipo mistari yote 2 ule wa mauzo na wa faida hukutana. Tazama chati hiyo hapa chini;

8.3 Makisio ya Faida na Hasara.
Katika ripoti hii ya faida na hasara nitatumia hesabu ndogondogo ambazo zimeshajitokeza kwenye vipengele vingine vya mchanganuo huu huko nyuma. Ukichunguza mchanganuo wetu huu tangu mwanzoni mpaka sasa utagundua kuna sehemu kadhaa nimekuwa nikigusa hesabu au namba. Kwahiyo katika sehemu hizo zote ndogondogo sasa hapa ndio nitazichukua na kuzitumia kwenye Sura hii kuu inayohusu fedha.

Sura zilizogusa mahesabu au namba ni hizi zifuatazo;
1.   Sura ya pili, Maelezo ya Biashara katika kipengele kidogo cha ‘2.4’ Kianzio kwenye majedwali ya kianzio na Mizania ya biashara.
2.   Sura ya ‘5.0’ kipengele kidogo cha ‘5.3’, Makisio ya mauzo na gharama za mauzo
3.   Kwenye kipengele cha 6.0 cha Uendeshaji katika majedwali ya vifaa, malighafi na gharama
4.   Sura ya ‘7.0’ kipengele kidogo cha ‘7.3’, Uongozi na Wafanyakazi kwenye jedwali la mpango wa mishahara

Katika Makisio ya faida na hasara kuna vitu vikubwa 5 vifuatavyo,
1.   Mauzo
2.   Gharama za mauzo (zinazobadilika)
3.   Gharama za uendeshaji(za kudumu)
4.   Kodi
5.   Faida halisi

1. Mauzo yapo kwenye makisio ya mauzo sura ya 5 kama nilivyoeleza hapo juu na nimekisia mauzo ya mwaka mzima.

2. Gharama za mauzo (zinazobadilika) zinapatikana katika sura hiyohiyo ya 5 kwani huwa zinaambatana na mauzo, ni zile gharama za moja kwa moja za mahindi yanayotumika katika uzalishaji wa dona pamoja na gharama zote za moja kwa moja zinazoambatana na na uzalishaji huo kama, vibarua, umeme, vifungashio na umeme wa kusagia.

3. Gharama za uendeshaji za kudumu; hizi ni zile gharama za kila mwezi ambazo hata kama hamna uzalishaji lakini bado zitalipwa kama vile mishahara ya wafanyakazi wa kudumu, pango la eneo, uchakavu wa vifaa kama mashine nk. Gharama hizi tunazipata katika sura ya 6 kwenye kipengele cha Uendeshaji kwenye jedwali la gharama za kudumu.

4. Kodi ya mapato, imekisiwa kulingana na viwango mamlaka husika inazotoza biashara nyingine zinazofanana na hii.

5. Faida Halisi: Hapa ndiyo hitimisho la taarifa hii ya mapato na matumizi ya USADO Milling. Faida halisi nimeipata baada ya kutoa vitu vyote 3 vilivyotangulia kutoka kwenye Mauzo.

Kwa kawaida Ripoti hii nitaanza na makisio ya kila mwezi kwa miezi yote 12 ya kwanza, kisha ya mwaka 1 na miaka 2 inayofuata.

(a) Makisio ya kila mwezi, miezi yote 12 ya mwaka wa 1
Ili kukisia miezi nitahitaji “Spreadsheet” / “graph paper” au programu ya kompyuta kama vile Microsoft Excell au hata naweza tu kutumia Microsoft word kuchora jedwali lenye miezi 12 ambalo ndilo nitakalotumia kukisia namba zangu. Kama ningeamua kutumia karatasi basi ningechora jedwali lenye safu zilizolala (rows) na zilizosimama (columns) mfano wa grafu.

Jedwali langu zima litaonekana kama hili hapa chini isipokuwa mimi hapa sijaweka miezi yote 12 kutokana na udogo wa nafasi na kwa ajili ya kuonekana vizuri bila ‘kuzoom’, nimeweka tu mpaka mwezi wa 5 ambao ni Julai; Jedwali zima unaweza kuliona katika mchanganuo kamili wa USADO Milling





Kwenye safu zilizosimama (columns), kuna miezi 12. Mwaka wa USADO unaanzia mwezi Machi, hivyo nitaanza kuhesabu mwezi wa kwanza kuttoka “Machi” na kumalizika Februari.

Katika safu zilizolala (rows), kuna vitu vifuatavyo;
1)  Safu ya kwanza kabisa nimeweka mauzo. Mauzo tayari katika sura ya Mikakati kipengele kidogo cha 5.3.1 nilishakisia miezi yote na hapa kazi ni kuyaweka tu, kama uonavyo hapo juu, mwezi januari ni sh. 5,620,000 mwezi Julai sh.  6,030,000 na kuendelea…..mpaka mwezi Desemba sh. 7,830,000  ingawa jedwali limeishia tu Julai

2)  Safu inayofuata nimeweka Ghama za Mauzo, nazo tayari nilishazipata kwa miezi yote 12, ni kuziweka tu.

3)  Safu ya 3 ni Faida Ghafi, Faida ghafi nimechukua mauzo nikatoa gharama za mauzo.

4)  Safu ya 4 nikaweka asilimia ya faida ghafi kwa mauzo ambayo kutokana na mauzo na gharama zake kutofautiana kila mwezi basi kila mwezi una asilimia tofauti mfano Machi ni asilimia 26.3%, Mei 21.2% na Julai 22.7%

5)  Inafuata safu ya Gharama za uendeshaji. Hizi nazo nilikwishakisia katika sura ya 6 ambazo nilizitaja kuwa ni pango, mishahara, matangazo, umeme & maji, tozo mbalimbali, uchakavu na dharura. Jumla yake naweka pale chini kabisa ya vitu vyote hivyo vilivyotajwa

6)  Faida kabla ya kodi na riba, hii ni safu inayopatikana baada ya kuchukua Faida ghafi niliyoipata pale juu namba 3 na kutoa jumla ya Gharama zote za uendeshaji namba 5.

7)  Inafuata Riba ya mkopo ambayo inatokana na mkopo ikiwa USADO Milling wangelikuwa wameomba mkopo mahali. Lakini katika Mpango huu tunaambiwa Isabella na Maurine walitoa fedha zao wenyewe mfukoni walizodunduliza hivyo nimeweka sifuri pale (0) kila mwezi.

8)  Safu ya Kodi ya mapato, Hii imepatikana kutokana na makisio ya yaliyofanyika kulingana na utafiti kwa biashara nyingine zinazofanana na hii ya USADO.

9)  Faida Halisi, safu hii nimechukua Faida kabla ya kodi na Riba niliyokwishapata hapo juu namba 6 kisha nikatoa Riba na Kodi. Jibu lake ndio FAIDA HALISI.

10)       Safu ya mwisho kabisa katika jedwali hili la Faida na Hasara ni asilimia ya faida halisi kwa mauzo ambayo nimechukua faida halisi nikagawa kwa Mauzo kisha kuzidisha mara 100. Na nimefanya hivyo kwa miezi yote 12 kama unavyoweza kuona hapo katika mchanganuo wako wa USADO Milling.
Kwa ujumla jedwali hili linatuthibitishia kanuni isemayo;

FAIDA HALISI = MAUZO – GHARAMA ZOTE - KODI


(b)Makisio ya mwaka wa kwanza.
Ninaposema mwaka wa 1 au nikisema 2020 kwa biashara hii ya USADO Milling ni kitu kilekile. Baaada ya kumaliza kazi ya kukisia miezi yote 12 maana yake na ya mwaka wa kwanza pia nakuwa tayari nimeshamaliza.

Hapa ukijumlisha mauzo yote ya miezi 12 utapata jumla ni sh. 75,942,000 ambayo ndiyo mauzo ya USADO ya mwaka mzima wa 2020 na unaona nimeweka pale chini katika jedwali la mwaka, halikadhalika ukijumlisha safu zingine zote zilizolala (rows) utapata thamani iliyowekwa katika jedwali hili kama unavyoona.

Chakufanya tu ni kujumlisha kila safu iliyolala miezi yote 12 kisha majibu yake unayaweka katika jedwali la mwaka wa 1 kama ifuatavyo;

MUHIMU: Mpaka kufikia hapo watu wengi wanakuwa wameshamaliza kipengele hiki cha fedha ikiwa mchanganuo wako huna ulazima wa kukisia hesabu za miaka 2 inayofuata, pengine umeandika tu kwa ajili ya uendeshaji wa biashara yako hamna mdau au taasisi yeyote ile iliyokutaka uwasilishe mpango wa biashara.


(c)Makisio ya Miaka 2 inayofuata: mwaka wa pili na wa tatu.
Kama utakumbuka wakati nikikisia mauzo na gharama za mauzo katika sura ya 5.0 nilikisia mauzo ya mwaka wa kwanza 2020 kwa kujumlisha mauzo ya miezi yote 12 kisha nikasema kwa miaka miwili inayofuata yaani 2021 na 2022 nitatumia kanuni ya ongezeko la mauzo kwa asilimia na nilipata mauzo ya mwaka wa 2 baada ya kukisia ongezeko la asilimia 25% ya mwaka wa 1 na asilimia 50% mwaka wa 2 kupata mauzo ya mwaka wa tatu.

Nikapata mwaka wa pili kuwa ni sh. 94,927,500 na mwaka wa tatu sh. 142,391,250. Halikadhalika kwa upande wa gharama za mauzo pia nimefanya hivyohivyo kama jedwali linavyoonyesha hapa chini.



Gharama za Uendeshaji mwaka wa 2 na 3.
Kumbuka hapa nataka makisio ya mwaka wa 2 na wa 3 zaidi kwani mwaka wa kwanza tayari nimeshapata kila kitu. Gharama za uendeshaji ni rahisi kukisia na huwa hazibadiliki sana kwa mfano pango ulilolipa mwaka jana si rahisi mwaka huu liwe limepanda na hata mishahara ni hivyohivyo.

Kwa hiyo nitaangalia tu zile gharama ambazo kulingana na biashara kukua au kusinyaa zinaweza kubadilika kwa mfano vitu kama gharama za mishahara, pango umeme, maji, na fedha za dharura. Hapa mtu unatumia tu akili yako ya kuzaliwa“common sense” kama mtu unayetarajia kuifanya hiyo biashara.
1)  Kwa mfano katika biashara hii ya USADO Milling mishahara mwaka wa pili na wa tatu utaona itaongezeka kutoka sh. 4,800,000 mwaka wa 1 mpaka sh. 7,200,000 mwaka wa 2 kutokana na sababu kwamba kuna Meneja atakayeajiriwa kuanzia mwaka huo. Mwaka wa 3 pia ataongezeka mtu mmoja na mishahara nayo itaongezeka na kuwa sh. 12,000,000

2)  Pango la eneo la biashara kwa mwaka wa 2 litaendelea kubakia vile vile lakini litaongezeka mwaka wa 3.

3)  Gharama za matangazo mwaka wa pili zimebakia vilevile sh. 1,200,000 lakini mwaka wa 3 zitaongezeka mpaka sh. 1,500,000 na hii inatokana na kampuni kukua hivyo shughuli za matangazo nazo kuongezeka

4)  Gharama za umeme na maji zitaongezeka kila mwaka kutokana na sababu kwamba shughuli za kiwanda zinakisiwa kukua, vifaa mbalimbali kama vile taa, feni, heater na bomba la maji vinatarajiwa kufanya kazi mara dufu tofauti na mwaka wa kwanza.

5)  Fedha za dharura, matengenezo na tozo mbalimbali pia zinakisiwa kuongezeka kwasababu biashara ikikua changamoto nazo huongezeka pamoja na tozo za serikali.

6)  Gharama za Riba kwenye mchanganuo huu hatuna kwasababu kampuni haikukopa.

7)  Kodi ya mapato nayo nimekisia itaongezeka kidogo mwaka wa 3 kutokana na biashara nayo kukua.
Baada ya kukisia gharama zote za uendeshaji na kupata jumla yake nitakokotoa faida kabla ya kodi na riba kwa kuchukua Faida ghafi kisha nitoe jumla hiyo ya gharama za uendeshaji kwa miaka yote 2.

Pia nitatoa kodi ya mapato kama nilivyofanya katika mwaka wa 1 na kupata FAIDA HALISI. Mpaka hapo nitakuwa nimekwishamaliza kukokotoa Faida na Hasara kwa miaka yote mitatu na jedwali letu sasa litaonekana kama ifuatavyo;










MUHIMU SANA:
Kumbuka jedwali la Faida na Hasara ndio msingi wa majedwali ya Ripoti nyingine zote 2 zinazofuata za “Mtiririko wa fedha” na “Mizania ya biashara” kwani karibu vitu vyote vya ripoti hizo hutegemea namba kutoka katika jedwali hili, hivyo ni vizuri kuhakikisha jedwali hili linakisiwa kwa umakini.

Na pia kama umeandika mpango wako wa biashara unaweza ukaweka jedwali hili tu peke yake likatosha kuwakilisha mawazo yako mazima kwenye kipengele cha fedha kwa ujumla. Na isitoshe hii ndiyo Ripoti rahisi zaidi kukokotoa moja kwa moja bila hata ya kuhitaji utaalamu mkubwa.





8.4 Makisio ya mtiririko wa fedha.

(1)Miezi 12 ya mwaka wa 1
Katika Ripoti hii pia naanza na makisio ya miezi 12 ya mwaka wa kwanza kama tulivyofanya kwenye faida na hasara, kisha nitatafuta jumla ya miezi yote 12 kukamilisha makisio ya mwaka mzima wa kwanza. Baada ya hapo sasa nitakisia miaka 2 inayofuata.

MUHIMU: Lakini kuna kitu kimoja hapa nataka ujue mapema kabla hatujaendelea, Kuna vipengele katika ripoti hii wakati unapokuwa ukivikokotoa, moja kwa moja pia unakuwa ukikamilisha na baadhi ya vipengele katika ripoti ya 3 ya Mali na Madeni (Mizania).

Na hii ndio sababu tunasema kwamba ripoti hizi zote 3 zinategemeana na kuhusiana, makosa katika ripoti moja husababisha ripoti nyingine 2 pia kuwa na makosa na hesabu hazitaoana. Pia vipengele vya ripoti hii vingi vinatokana na jedwali lile la Faida na Hasara tulilomaliza hivi punde.

Ripoti ina jedwali lenye sehemu kuu 2, upande wa juu ni wa Fedha taslimu zinazoingia(Fedha ingia) na upande wa chini ni wa fedha taslimu zinazotoka(Fedha toka). Juu kabisa kuna kianzio na chini kabisa safu mbili zilizolala kuna Mtiririko wa fedha pamoja na salio la mwisho kwa kila mwezi. Hapo chini nimeweka miezi 5 tu, jedwali kamili unaweza kuliona katika mchanganuo kamili wa USADO Mlilling.



8.5 Makisio ya mali na madeni (Mizania ya Biashara).
Jedwali la ripoti ya Mali na Madeni nayo imegawanyika katika sehemu kuu 2, sehemu ya kwanza ni ya juu ambayo hukaa Rasilimali (Mali) au Asseti, Sehemu ya pili ni upande wa chini ambao huwekwa Mtaji wa wawekezaji pamoja na Madeni (vyanzo vya Mali hizo)


Tuanze na makisio ya kila mwezi kwa mwaka wa 1
Baada ya kukamilisha zile ripoti 2, ripoti hii ya tatu nayo inakuwa imekwishakamilika kwani nitakuwa nikitumia namba kutoka majedwali mengine kuikamilisha.

Nitachora jedwali letu lenye safu zilizosimama (columns) 13, safu moja itatumika kuweka namba za kuanzia kutoka katika lile jedwali la Mizania ya mwanzo kabisa wakati nikikisia Mahitaji na chanzo cha mahitaji sura ya 2, huku safu 12 zikiwa ni za miezi 12. Safu zilizolala (rows) zinawakilisha hesabu mbalimbali (accounts)

Ripoti hii tofauti na zile mbili ya Faida na hasara na ile ya Mtiririko wa fedha, ili kupata makisio ya mwaka mzima wa kwanza sitajumlisha safu zilizolala (rows), bali nitachukua safu nzima iliyosimama (column) ya mwezi wa 12. Kwa upande wa miaka 2 inayofuata nitafanya makadirio kwa kutumia asilimia ya mauzo ya kila mwaka. Katika jedwali lifuatalo nimeweka hadi mwezi wa 4 na miezi yote 12 inapatikana katika Mchanganuo kamili wa USADO Milling.


Ikiwa Hesabu zako utakuwa umezifanya kwa usahihi, utaona jumla ya mtaji na deni utakayopata hapo upande wa chini, inalingana sawasawa kabisa na jumla ya (rasilimali) Mali uliyopata upande ule wa juu bila hata ya kulazimisha na huo ndio ushahidi kuwa Ripoti hizi 3 zinashirikiana.



8.6 Sehemu muhimu za biashara.
Kuna uwianao wa aina nyingi lakini hapa nimeweka baadhi yake tu kwa kuziorodhesha. Jedwali zima lenye sehemu hizo zote lipo katika mchanganuo mzima wa USADO Milling.

Asilimia ya Mauzo
Huu ni uwiano unaowezesha mtu kujua sehemu mbalimbali mfano gharama za mauzo, faida ghafi, gharama za uendeshaji na faida halisi ni asilimia ngapi ya mauzo kwa kugawa vitu hivyo kwa mauzo kisha unazidisha mara 100. Hukuwezesha kulinganisha biashara husika na nyingine za washindani.

1) Asilimia ya Faida kwa mali zote/Return on Assets (ROA)
Uwiano huu unachukua Faida halisi kisha unagawa kwa Jumla ya mali zote mara 100

2) Faida halisi kwa mtaji wa wawekezaji / Return on Investment (ROI), huu ni uwiano muhimu unaomwezesha mwekezaji kuwa na matumaini kwamba fedha zake zitarudi, unachukua faida halisi unagawa kwa mtaji wa mwekezaji mara 100. Kwa USADO nimepata ni asilimia 20% mpaka 22%

3) Gharama za mauzo/bidhaa za stoo/Inventory Turn Over.
Uwiano huu unachukua Gharama za mauzo unagawa kwa wastani wa salio la Malighafi za stoo, hupima biashara inauza haraka kiasi gani, uwiano mkubwa, 5 mpaka 9 ni ishara kwamba biashara inauza faster zaidi, mzigo haukai. Katika mpango wa USADO Milling nilipata 8.3 kwa mwaka 2020 ambao ni mzuri

4) PAY BACK PERIOD (Muda wa kurudisha mtaji)
Haya ni makadirio ya muda kianzio chote kitarudi na hupatikana kwa kuchukua kianzio na kugawa kwa Faida halisi. Jibu lake ndiyo muda mtaji wote unakisiwa kurudi

44,600,000 / 10,655,600= 4.18
Sawa na miaka 4 na miezi 2

Mwisho wa Sura hii ya 8 kesho tutamalizia na Sura ya 9. Kwa swali lolote lile au maoni unakaribishwa. Asante.


SEMINA SIKU-5                SEMINA SIKU-7

0 Response to "SEMINA SIKU YA 6: MPANGO WA FEDHA MCHANGANUO WA BIASHARA KIWANDA CHA DONA (USADO MILLING"

Post a Comment