SEMINA SIKU YA 2: MUHTASARI, MAELEZO YA BIASHARA NA BIDHAA | JIFUNZE UJASIRIAMALI

SEMINA SIKU YA 2: MUHTASARI, MAELEZO YA BIASHARA NA BIDHAA


SEMINA-2

SASA TUNAANZA RASMI KUANDIKA MPANGO WETU WA BIASHARA YA USADO MILLING HATUA KWA HATUA.

Karibu tena kwemye semina yetu na leo tutaandika Sura/Sehemu 3 ambazo ni  maelezo yanayohusu; 

1. MUHTASARI
2. BIASHARA na
3. SOKO

Lakini kabla ya kuanza rasmi nahakikisha kwanza ninavyo mezani vipengele/sehemu zote 8 za mpango wa biashara nitakazotumia katika kuandika sura baada ya sura lakini bila ya kujali kama nafuata mfululizo kamili kama unavyoonekana katika mlolongo wa vipengele pale juu.


Hata hivyo mimi nimeamua kufuata mlolongo wa vipengele kwa namba kama unavyoonyesha lakini nitaacha kwanza wazi sehemu ya kuandika Muhtasari kwani ingawa ndiyo sehemu ya kwanza kimuonekano lakini huwa inaandikwa mwishoni kabisa kwa kuwa ni ufupisho wa yale yote yaliyoandikwa kwenye mchanganuo mzima.


1.0 MUHTASARI
Aya zinazounda Muhtasari ni ufupisho kutoka katika sehemu nyingine zote za mpango wa biashara. Utaona wakati nikiandika sehemu nyingine zijazo, kila mara nitaanza na ufupisho mdogo wa sehemu husika, mihutasari hiyo midogomidogo yote ndiyo hatimaye huja kuunda muhtasari huu tendaji.

Au Pia naweza tu nikachagua kutoka katika kila sura zile sentensi zilizobeba vitu muhimu kisha nikaziunganisha pamoja na kupata Muhtasari wa andiko hili zima. Muhtasari wa mchanganuo wa USADO Milling nimeandika kurasa 2

(Vitu vitatu vifuatavyo, Dhamira kuu, Maono, malengo na Siri za mafanikio mara nyingi hukaa chini baada ya Muhtasari lakini pia kuna wengine huwa wanaviweka kwenye Sura ya pili ya “Maelezo ya Biashara”. Hamna tatizo kuviweka popote kati ya sehemu hizi mbili)

1.1 Dhamira Kuu.
Dhamira kuu ya USADO Milling nimeandika lile tatizo ambalo wanakusudia kulitatua kwa wateja wao, Unga wa dona inajulikana unatatua tatizo la njaa kwa watu lakini ikiwa kampuni ya USADO Milling itaamua kukidhi tu tatizo hilo la msingi la njaa basi watakuwa hanma chochote kile kipya walichokuja nacho, hamna ubunifu na hivyo hamna ujasiriamali uliotumika.

Kwahiyo imewabidi waje na dhamira bunifu kabisa na ya kipekee kidogo kusudi waweze kuwa tofauti na kukidhi aina fulani tu ya wateja wenye tatizo ambalo makampuni mengine ya unga wa mahindi hayajaweza kulitatua bado kwa uhakika. Cheki dhamira hiyo ndani ya mpango kamili wa USADO Milling. 

1.2 Malengo.
Katika mpango huu wa USADO, nimetaja malengo yanayopimika yenye muda maalumu wa utekelezaji yapatayo 6. Malengo haya ni yale kampuni iliyojiwekea itakayoyatimiza ndani ya mika 3 ijayo.

1.3 Siri za Mafanikio.
Siri za mafanikio nimetaja mambo muhimu 3 ambayo USADO ndiyo watakayoyapa kipaumbele kikubwa katika kuhakikisha biashara yao inapata mafanikio makubwa. Si kama maswala mengine watayapuuzia hapana, bali hayo 3 ndiyo kama silaha yao ya “maangamizi”.

2.0 MAELEZO YA BIASHARA.
Mwanzoni mwa Sura hii naacha nafasi kama aya moja au mbili hivi kwa ajili ya kuja kuandika muhtasari wa sura nzima.

(Kumbuka hata sura nyingine zote zinazofuata baada ya hii, kila moja itakuwa na muhtasari wake mdogo kama huu mwanzoni.)

Kisha baada ya hapo naanza kutazama mlolongo wa vipengele vidogo vya Sura hii ya Maelezo ya Biashara. Vipengele hivyo vidogo kwa mujibu wa mlolongo rasmi wa vipengele vinavyounda mpango wa biashara ni hivi hapa chini;

2.1 Malengo
2.2 Dhamira kuu
2.3 Siri za mafanikio
2.4 Umiliki wa Biashara
2.5 Kianzio (kwa biashara mpya au historia kwa biashara iliyokwishaanzishwa)
2.6 Eneo la biashara na vitu vilivyopo pale

“2.1 Umiliki wa biashara”
Hapa utaona nimetaja kabisa wamiliki wa USADO ambao ni Bibi Maurine Kinyunyu na Isabella Michael, aina ya usajili kisheria ambao ni Kampuni ya Ubia, na kiasi cha mtaji kila mmoja alichochangia. Hata unaweza kuona katika jedwali la mahitaji pale chini gharama za usajili wa kampuni hii siyo kubwa sana kama vile ingelikuwa ni “Limited company”, ubia unasajili kama vile ufanyavyo unaposajili jina la biashara na gharama pia ni kidogo.

2.2 Eneo la Biashara.
Katika kipengele hiki kidogo nataja eneo biashara itakapofunguliwa Mbezi Mwisho pamoja na maelezo mengine yote yanayohusiana na eneo kama vile ukubwa wake, uhusiano wa eneo na wateja walengwa nk. Ningeweza pia kuelezea na miundombinu mbalimbali iliyopo pale kama majengo.

2.3 Tathmini ya Nguvu, Udhaifu, Fursa na Vikwazo (NUFUVI)
Tathmini hii siyo lazima ikae hapa, wakati mwingine unaweza hata ukaiweka katika Sura inayohusika na Soko au ukaamua kuiweka katika Vielelezo. Ndio maana nilisema kwamba vipengele katika mpango wa biashara havina ‘formula’ maalumu, vinaweza kukaa mahali popote ilimradi viwe na maana kwa msomaji wa mpango wako.

“2.4 Mahitaji (mtaji)”
Kwa kuwa ni biashara mpya ni lazima nionyeshe mahitaji ya mtaji na chanzo cha mahitaji hayo kwa kuchora chati na jedwali pamoja na maelezo kidogo. Ningeliweza kuorodhesha tu bila jedwali ilimradi ijulikane jumla ya mahitaji hayo ni kiasi gani. Namba nilizotumia hapa zimetokana na utafiti ule uliofanyika na wamiliki wa biashara hii.

Jumla ya mahitaji yote nimeorodhesha gharama zote zinazohitajika kuanzisha mradi huu kuanzia gharama za awali kabisa kama zile za kusajili biashara na maandalizi ya eneo, gharama za kununulia vifaa na mashine pamoja na malighafi za kuanzia ikiwemo pesa taslimu za kulipia gharama nyingine za kila siku.

Baada ya kumaliza, sasa narudi pale mwanzoni katika aya niliyoiacha wazi kwenye namba “2.0 Maelezo ya Biashara.” ilipoanzia sura, nachagua katika kila kipengele kidogo nilichokwisha andika mstari mmojammoja au maneno muhimu na kuyapanga katika hii aya kutengeneza muhtasari mdogo wa kipengele au sura nzima.

Na hivyo ndivyo unavyoweza kuandika Sura au maelezo ya Biashara katika mpango wa biashara yeyote nyingine.

Hakuna ugumu ila kikubwa nimezingatia tu orodha ya hivyo vipengele vidogo nilivyotaja pale mwanzoni wakati naanza hii sura.



3.0 MAELEZO KUHUSU BIDHAA.
Katika sura hii ya tatu pia huanza na muhtasari mfupi wa Sura nzima na hii inaandikwa mwishoni baada ya kumaliza vipengele vya sura yote. Baadhi ya vipengele muhimu vya sura hii ni hivi hapa chini;

3.1 Maelezo ya bidhaa/huduma
3.2 Utofauti wa bidhaa/huduma na za washindani
3.3 Vyanzo vya malighafi/bidhaa
3.4 Kopi za matangazo
3.5 Teknolojia
3.6 Bidhaa au Huduma za baadae

Si lazima katika mpango wa biashara kuweka kila kipengele kama uonavyo hapo juu, unaweka tu vile vinavyoendana na mazingira ya biashara yako unayoandikia kwa wakati huo. Kipengele kisichokuwa na umuhimu unakiacha.

3.1 Upekee wa bidhaa
Tukianza na “Upekee wa bidhaa” kwenye mchanganuo wa biashara ya USADO Milling, unga wa dona utakaozalishwa utatofautiana na unga uliozoeleka sokoni katika ubora kwa kuwekeza katika vifaa na miundombinu inayowezesha kiwango hicho cha ubora kufikiwa na hivyo kuwafanya wateja warudishe imani iliyopotea kwa unga wa dona. Kabla ya hapo bidhaa ya dona ilitelekezwa.

3.2 Vyanzo vya malighafi
Kama uonavyo katika mchanganuo wetu huu wa USADO Milling, tumetaja ni wapi(mikoa mbalimbali) malighafi ambayo ni mahindi safi na mazuri yatapatikana, ni kina nani watakaohusika kuhakikisha mahindi hayo ni safi na salama nk.

3.3 Teknolojia.
Eneo hili nimetaja teknolojia muhimu biashara inazotarajia kuzitumia na jinsi teknolojia hizo zitakavyopatikana. Pia nimeelezea kidogo mazingira yote kuhusiana na teknolojia hizo mfano nilitaja mifuko maalumu ya PICK ambayo ni teknolojia ya uhifadhi wa mahindi ambayo si wazalishaji wengi wa unga huitumia na pia mfumo wa kuchambulia mahindi kuondoa takataka za aina zote ingawa bado huu wa kwetu hapa unatumia vifaa vya kawaida kidogo, lakini nimeeleza pia kwamba kuna mikakati kabambe ya kununua mtambo wa kisasa zaidi kutoka China uwezo wa pesa ukiimarika.

Vipengele vingine vidogo katika sura hii ni;

3.4 Bidha za baadae.
Ambacho nimetaja bidhaa kampuni inafikiria kuja kuwa nazo siku za baadae. Zipo bidhaa 4 pale nilizotaja ambazo nazo ni bidhaa bunifu zisizozoeleka bado wala kujulikana na washindani wa USADO kuwa zinaweza kuleta mapinduzi makubwa kwenye biashara hii ya usagishaji nafaka.

3.6 Bei ya Bidhaa
Kipengele hiki nacho nimeelezea bei kwa kila kifungashio cha unga wa dona utakaozalishwa. Kwenye upande wa sura ya mikakati na Utekelezaji, mkakati wa bei huzungumziwa kwa kina zaidi lakini hapa ni kwa kifupi tu unataja bei basi

Nimemaliza Sura inayohusu Bidhaa na kesho tutaendelea na Sura nyingine ya 4, Soko. USIKOSE!

SEMINA SIKU-1                SEMINA SIKU-3


.....................................................


Ili uweze kufuatilia vizuri zaidi masomo haya mpaka mwisho ni vizuri ukawa na Mchanganuo kamili wa USADO Milling. Mchanganuo huo unapatikana kwa gharama kidogo ya sh. elfu 10 tu. Nasema ni gharama kidogo kwa sababu kila anayenunua anapata pia na vitu vingine bure vilivyo na thamani zaidi ya mara 5 ya hiyo. Vitu unavypata ni hivi vifuatavyo;


1.   Kitabu cha MICHANGANUO YA BIASHARA NA UJASIRIAMALI -Kiswahili

2.   Kitabu cha Michanganuo ya biashara kwa kiingereza(Ndio hutumiwa zaidi na vyuo vikuu vingi duniani. -Kiswahili

3.   Kifurushi cha Michanganuo ya biashara za ufugaji wa kuku(MKOMBOZI CHICKS PLAN 3PACKS) -Kiswahili

4.   Mchanganuo na semina ya Biashara ya Mgahawa wa chakula(JANE RESTAURANT)Kiswahili & kiingereza

5.   Mchanganuo wa biashara ya matikiti maji(kibada watermelon Project) Kiswahili

6.   Kujiunga na Magroup ya watsap & Telegram ya Michanganuo-online ukitaka.

Kutumiwa mchanganuo kamili wa USADO MILLING pamoja na vitu vingine hivyo vyote 6 nilivyoorodheshwa hapo juu kama OFFA, lipia shilingi elfu 10 kupitia namba zetu zifuatazo, 0765553030 au 0712202244, kisha tuma ujumbe usemao; 

"NITUMIE MCHANGANUO WA USADO NA OFFA YA VITU 6"

Kumbuka hii offa ni ya muda mfupi na pia Group la whatsapp halikawii kujaa, hivyo ni vyema ikiwa unanufaika na masomo haya basi uwahi offa hii mapema kabla haijamalizika au group kujaa.

NAMBA ZETU NI, 0765553030  au  0712202244  jina ni;


Peter Augustino Tarimo


KARIBU SANA! na usisahau kufuatilia mfululizo wa semina hii hapo kesho tena saa 4 -5 asubuhi.

I

0 Response to "SEMINA SIKU YA 2: MUHTASARI, MAELEZO YA BIASHARA NA BIDHAA"

Post a Comment