ACHA KAZI UONE ILIVOKUWA KAZI KUTAFUTA KAZI | JIFUNZE UJASIRIAMALI

ACHA KAZI UONE ILIVOKUWA KAZI KUTAFUTA KAZI


Ujumbe wetu wa leo kutoka kwenye Daladala ni,“ACHA KAZI UONE ILIVOKUWA KAZI KUTAFUTA KAZI” ijapokuwa ni maneno machache tu yaliyoandikwa nyuma ya bodi ya Dala dala lakini ukweli ni kwamba ujumbe huu umebeba maana kubwa  sana. Watu walioajiriwa huweza kuacha kazi kutokana na sababu mbalimbali kama vile, kufukuzwa, kuona tu uvivu au tabu na kuamua kuacha kazi ukitegemea maisha ‘kujiseti ‘yenyewe, kwenda kufanya kazi yenye maslahi makubwa zaidi, kustaafu, au kwenda kujiajiri binafsi.

Katika njia zote zilizotajwa hapo juu, kuna taratibu ambazo ni lazima zifuatwe kabla mtu hujafanya uamuzi wa kuacha kazi aliyokuwa akiifanya zamani na kuamua kuhamia upande wa pili, hata kama ikiwa ni kuacha kazi kwa kustaafu. Kwa ujumla ni kwamba katika sababu zote hizo, kitu cha msingi sana unachopaswa  kufanya mtu kabla hujaachana na kazi uliyokuwa nayo ni MAANDALIZI. Maandalizi yanajumuisha, kujiwekea akiba ya fedha kwa ajili ya kipindi cha mpito wakati kabla kazi au jukumu jipya la maisha halijaanza kutengeneza fedha.

Jiulize utayamudu vipi maisha  ikiwa mambo yatakwenda  kinyume na ulivyotarajia?. Vile vile katika maandalizi hayo pia ni lazima ufanye utafiti wa kutosha wa lile jukumu, kazi au biashara unayotaka kwenda kuifanya na wala siyo suala la kukurupuka tu, fahamu kila kitu kinachohusiana na mazingira hayo mapya.

Katika njia ambayo watu wengi wamekuwa wakikosea  kwa kuwa na fikra zisizokuwa sahihi ni hii ya kuacha kazi kwa lengo la kujiajiri binafsi, wengi hudhani kwamba, kuwa bosi wako mwenyewe basi ndio kila kitu unafanya kulingana na matakwa yako, la hasha. Kujiajiri binafsi hasa kupitia biashara na ujasiriamali kunahitaji nidhamu ya hali ya juu kabisa kusudi mtu aweze kufanikiwa. 

Kuwa na mtaji unaotosha kuanzisha mradi wenyewe, waweza kuwa pesa zako binafsi au uwe na uwezo wa kuweza kupata pesa/mtaji kutoka vyanzo vinginevyo. Uwezo wa kufanya majukumu mengi kwa wakati mmoja na pasipo kuchoka(uvumilivu), wewe ndiyo mkurugenzi, meneja, afisa masoko, sekretari na msambazaji kwa wakati mmoja. Pamoja na kuhakikisha kuwa kile utakachozalisha au kuuza ni bidhaa/huduma wateja wanayoihitaji kweli. Kushindwa kuyaangazia maswala hayo kwa kina ndiko kunakosababisha biashara zaidi ya asilimia 90% kufa kabla hata miezi sita haijamalizika.

Tengeneza mpango wa kuhama, kwani kutakupunguzia msongo wa mawazo. Kubadilisha kazi uliyoizoea ghafla  siyo jambo rahisi, unaachana na mazingira , watu uliowazoea na kuwapenda, ni lazima ujisikie vibaya lakini kwa kujipanga na kuweka mpango  maalumu hautaathirika kwa kiwango kikubwa. Kitu kingine cha msingi sana ni kuhakikisha hauharibu mahusiano yako na wale uliokuwa ukifanya nao kazi zamani, iwe ni waajiri wako, wafanyikazi wenzako au wateja katika kampuni uliyokuwa ukiifanyia kazi. Katika biashara yako mpya kuna siku unaweza kuja kujikuta ukihitaji msaada wao kwa namna moja au nyingine, hivyo “acha kutukana mamba ungali bado hujavuka mto”

Unaweza ukajiuliza, “Hivi kama nikitaka kuachana na kazi yangu ya zamani na kuamua kuanzisha ujasiriamali kwa kumiliki kabiashara kangu nitafanyaje fanyaje, na mtaji nitatoa wapi? Mbona mshahara wenyewe ninaolipwa ni kidogo wala hautoshelezi mahitaji yangu yote?” Jibu ni rahisi tu, “MIFEREJI YA PESA”. Pamoja na njia za kuondokana na ajira yako ya zamani iliyoelezewa hapo juu, bado unahitaji mambo mengine madogo madogo ili uweze kuhama kwa starehe zaidi. Mambo hayo unaweza ukajifunza kwa undani zaidi ndani ya kitabu kiitwacho Mifereji 7 ya pesa na siri matajiri wasiyopenda kuitoa.






0 Response to "ACHA KAZI UONE ILIVOKUWA KAZI KUTAFUTA KAZI"

Post a Comment