WIZI NA UTAPELI VIBANDA VYA KUTOA/KUWEKA PESA, TIGO VODA AIRTEL NA ZANTEL | JIFUNZE UJASIRIAMALI

WIZI NA UTAPELI VIBANDA VYA KUTOA/KUWEKA PESA, TIGO VODA AIRTEL NA ZANTEL

Katika Jiji la Dar es salaam, wezi na matapeli kila kukicha huvumbua njia mpya za kutekeleza uhalifu wao ilimradi tu wamejipatia pesa pasipo kuvuja jasho jingi. Wakati polisi wakihangaika kuwasaka wezi wanaonyemelea wateja kwenye ATM mashine ili kukopi namba zao za siri na hatimaye kuja kuwaliza, kuna wimbi jingine la wahalifu ambao wao kazi yao ni kuwaliza wahudumu katika vibanda vya kuweka na kutolea pesa maarufu kama Tigo pesa, M-pesa,Airtel money na Ezy pesa.

Leo hii asubuhi, maeneo ya Buguruni stendi ya Muhimbili, jamaa mmoja nusura achomwe moto na wananchi wenye hasira kali baada ya jaribio lake la kuiba na kutokomea na pesa kiasi cha shilingi laki mbili na elfu ishirini kugonga mwamba. Shuhuda wa tukio hilo mwanausalama(lakini siyo wa jeshi la polisi) na ambaye pia kukosa kuwepo yeye huyu kibaka sasa tungelikuwa tunamwita marehemu anasimulia mkasa wenyewe  kama ifuatavyo;

“Nilikuwa nimekaa karibu na kibanda cha kutolea pesa na kuweka pesa katika simu za mkononi, mara akaja kijana mmoja na kumtaka mhudumu amuwekee shilingi laki moja na elfu sabini katika simu. Baada ya kumtajia namba yule dada alitaka kwanza apewe pesa lakini kijana alimwambia asiwe na wasiwasi bali aweke kwanza. Dada aliweka na kutaka sasa apewe pesa lakini kijana badala ya kumlipa alimtaka aongeze tena kiasi kingine cha shilingi elfu hamsini ndipo amlipe, naye akafanya hivyo.

Dada alianza kuingiwa na wasi wasi baada ya kijana yule kutokuonyesha dalili zozote za kulipa pesa zaidi ya kushika bahasha mkononi huku akijisachi sachi kama mtu aliyepoteza pesa. Ikabidi dada yule atuombe msaada watu tuliokuwa karibu pale huku tayari akiwa amekwishamkwida shati na kumnyanganya ile bahasha aliyokuwa nayo mkononi. Tulipoifungua ndani mlikuwa na udi na unga unga mfano wa dawa ya kienyeji.

Kumbe wala mfukoni hakuwa na simu, zile pesa zilitumwa kwa mtu mwingine tapeli mwenzake, dada alijaribu kumpigia simu wala hakupokelea, haraka akapiga simu mtandao uliotumika kutuma zile pesa lakini nao wakamjibu kuwa pesa zilizotumwa zimekwishatolewa.

Raia wengi walikuwa wamekwishaanza kujaa pale, na alijitokeza kijana mmoja akamrukia yule kibaka kwa hasira akitaka kumtoa koromeo huku akidai ni juzi tu mdogo wake anayemuuzia kibanda cha pesa aliibiwa kiasi kikubwa cha pesa kwa mtindo huo. Baada ya kuona vile ilinibidi nimzuie na kumuachanisha lakini watu walijawa na hasira wakidhani mimi ni kibaka mwenzake.

Ikabidi nijitambulishe, ‘jamani mimi ni mwanausalama, na ikiwa mtamuua huyu mtuhumia mbele yangu sitakuwa nimetimiza wajibu wangu, na isitoshe kumuua siyo suluhisho kwani huyu dada hataweza kuzipata pesa zake zilizokwishaibiwa. Inabidi huyu akawaonyeshe hao wezi wenzake aliowatumia hizo pesa, ni lazima anawajua’
Kibaka akichomwa moto na wananchi wenye hasira kali.
Pamoja na kujitambulisha lakini watu hawakujali kitu, mmoja akasema leteni petrol na mara moja ikaletwa , kuona vile ikabidi nitumie nguvu za ziada kumsukumiza yule kibaka mle ndani ya kibanda alikokuwa yule dada na kuufunga ule mlango. Raia mmoja akasikika akisema, ‘sasa umeamua kumingiza huyo mwizi huko ndani ili akambake dada wa watu kabisa siyo?’

Mara bosi wa yule dada naye alifika pale, nikamkabidhi na kumsihi asikubali watu wamuue yule mwizi mikononi mwake kwani itamletea matatizo baadaye, badala yake akaripoti polisi waje wamchukue na ndipo hata pesa zake zinaweza zikapatikana. Mimi niliondoka na kuwaacha lakini wakati huo wote yule kibaka alikuwa amenywea utafikiri alikuwa amemwagiwa maji. Baadaye nilirudi pale kuulizia hatima ya mkasa ule nikaambiwa polisi walifika pale na kuondoka na mtuhumiwa pamoja na wale walioibiwa pesa zao." 

Alimalizia kusimulia mwanausalama huyo kutoka jijini mbeya aliyefika hapa Dar kwa safari ya kikazi.


0 Response to "WIZI NA UTAPELI VIBANDA VYA KUTOA/KUWEKA PESA, TIGO VODA AIRTEL NA ZANTEL"

Post a Comment