JE UNA MADENI KAMA UGIRIKI? | JIFUNZE UJASIRIAMALI

JE UNA MADENI KAMA UGIRIKI?


Hali ya madeni ya nchi ndogo ya Ulaya, Ugiriki, ni funzo kubwa kote Duniani siyo kwa ngazi ya nchi tu au Taasisi kubwa kubwa, bali hata kwa mtu mmoja mmoja kama iivyokuwa kwako wewe unayesoma makala hii au mimi binafsi.

Kuwa na madeni ni kitu cha kawaida kabisa kwa nchi au hata kwa mtu binafsi, lakini yanapokithiri na kupindukia mipaka hugeuka kuwa  janga kubwa  na kero, hata kufikia hatua ya nchi kufilisika kabisa na kwa mtu binafsi kufikia hata hatua ya kuamua kujitoa uhai wake.

Sababu zilizoifanya nchi ya Ugiriki kufika hapa ilipo leo hii hazina tofauti na zile ambazo  humfanya mtu wa kawaida kufikia hatua ya kukata tamaa kwa madeni makubwa yasiyolipika kwa urahisi. Wagiriki baada ya kujiunga na Umoja wa Ulaya mnamo mwaka 1981 na hatimaye sarafu ya Euro hapo mwaka 2001 hapo ndipo deni lao lilipoanza kukua kidogo kidogo mpaka pale mgogoro ulipokuwa dhahiri kabisa mwaka 2009 na kuendelea kuitesa hadi hivi leo.

Baada ya kukumbwa na mgogoro kipesa Ugiriki iliendelea kukopa pesa  nyingi na ambazo imeshindwa kabisa kuzilipa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo, uongozi mbovu ulioshindwa kusimamia vyema mapato ya nchi, matajiri kukwepa kodi,  malipo makubwa ya pensheni ya  uzeeni pamoja na huduma za bure za afya. Kwa ujumla Ugiriki ilikuwa inatumia pesa nyingi kushinda vile ilivyokuwa ikizalisha yenyewe huku matumizi hayo yakiwa ni pesa za wakopeshaji.

Hapa ndipo hata mtu wa kawaida kabisa kama wewe na mimi tunapopata funzo kubwa ya kuwa, suala la matumizi hasa ya pesa ni la kufa na kupona kuhakikisha hutumii kiasi kinachozidi kile kinachoingia, na tena kinachoingia kwa maana ya ‘jasho na damu’ yako na wala isije ikawa ni pesa ulizokwenda kukopa kutoka katika taasisi ya pesa kama benki na taasisi nyinginezo.

Baada ya Wakopeshaji wa Ugiriki yaani Nchi za Umoja wa Ulaya EU, Shirika la fedha la Dunia ‘IMF’ pamoja na Benki kuu ya Ulaya ECB kuiwekea masharti  ya kubana matumizi kusudi waipe mkopo wa kuikoa isifilisike, Serikali ya Ugiriki chini ya Waziri mkuu wake Alexis Tsiprasis ilikaidi katakata na kuitisha kura ya maoni hapo jumapili yaani leo, wananchi waamue ikiwa wakubaliane na masharti hayo ya kubana matumizi au wayakatae na kujiondoa kwenye sarafu ya Euro.


Hakuna njia ya mkato kuondokana na madeni kama yanayoikabili Ugiriki, zaidi ya kukubali kubana matumizi na kufanya kazi kwa nguvu zaidi na maarifa, kuendelea kukopa sehemu moja na kwenda kulipa kwingine hakutosaidia bali kuzidi kulimbikiza madeni ambayo nayo yanakuwa na riba ndani yake ambayo huzidi kufanya hali kuendelea kuwa ngumu. 

0 Response to "JE UNA MADENI KAMA UGIRIKI?"

Post a Comment