BIMA NA ELIMU YA MIPANGILIO YA PESA: NI WATU WACHACHE SANA WENYE UELEWA | JIFUNZE UJASIRIAMALI

BIMA NA ELIMU YA MIPANGILIO YA PESA: NI WATU WACHACHE SANA WENYE UELEWA


Kwa muda mrefu Watanzania wengi tumekuwa na dhana kwamba suala la Bima linahusika tu katika shughuli za magari  hususani yale ya abiria au labda na kwenye majengo marefu pindi moto unapozuka. Na ni hivi karibuni tu imeanza na bima ya matibabu ndipo wengi tukajua kumbe hata hospitalini nako bima inatumika.

Mimi binafsi siku za nyuma niliwahi kuunguliwa moto na biashara yangu ya kioski iliyokuwa Kariakoo maeneo ya Msimbazi, kila kitu kiliteketea kuanzia mafriji, mali zote na pesa. Tena isitoshe nilikuwa na mkopo mahali fulani katika hizi taasisi za fedha lakini wala wazo la kudai taasisi  walao inifikirie au hata kunisamehe marejesho ya mkopo ingawa taasisi hiyo ilikuwa na kitu kinachoitwa bima sikufikiria kabisa wala kuwafikishia taarifa hizo.


Baadaye nilipokuja kuelewa vizuri maswala ya bima yanavyofanya kazi ndipo nilipokuja kugundua kumbe nilikuwa na haki ya kudai kampuni inayotoa bima kwa ile taasisi inilipe kwa ajili ya janga la moto lililoikumba biashara yangu. Nilijikuta najikamua kisawasawa mpaka nikamaliza marejesho ya mkopo ule ambao wakati janga linatokea sikuwa hata nimefikisha nusu ya marejesho.

Matatizo kama hayo huwakumba wajasiriamali wengi, lakini kitu wasichokijua kabisa ni kwamba bima mtu unaweza ukakata kwa kitu chochote, kuna bima za maisha , elimu, biashara, magari moto na kila aina, isitoshe haziangalii ukubwa wa shughuli, unakata bima na kuilipia  kulingana na ukubwa wa biashara /shughuli yenyewe. Kwa kweli mimi sioni hasara ya kutoa kwa mfano shilingi laki moja kwa mwaka mzima, hata kama ikiwa janga halitatokea ukilinganisha na hasara inayopatikana endapo itatokea bahati mbaya biashara au shughuli yeyote ile ikakumbwa na mkasa utakaosababisha hasara isiyomithilika kama moto wizi, mafuriko, ulemavu, kifo nk.   BIMA NI ULINZI KWA BIASHARA YAKO.


Hivi karibuni katika Redio ya CAPITAL FM inayorusha matangazo yake jijini Dar es Salaam kulikuwa na mahojiano mazuri sana kuhusiana na umuhimu wa Bima na elimu ya pesa ambapo Kamishna mkuu wa Bima nchini Tanzania Bwana Israel  Kamuzora alikuwa akifafanua jinsi ambavyo bima inavyoweza kusaidia kuinua uchumi na kuutokomeza umasikini. Chini tumeweka sehemu tu ya mahojiano hayo kwa sauti pamoja na maelezo hayo pia katika maandishi yakiwa yametafsiriwa sawasawa kama alivyoyatamka.
  


“……fundi magari…, au mjasiriamali unayeuza uza vitu sokoni, sasa ukiugua kwa wiki moja mtaji wote umekufa, kwanza wateja wamekuja hawakukupata mahali unapokaa kuuza mchicha, haupo, kwa hiyo watapata mteja mwingine, kwa hiyo umepoteza soko, lakini jambo la pili, ule mtaji wako unaoutumia katika kufanya biashara, ule mdogomdogo, woote umekwenda, kwasababu umekwenda kutibiwa, utafanyaje?. Kwa hiyo kuna Bima  ambayo ukilazwa hospitali inakulipa gharama ile ambayo kiwango kitakusaidia ili utakapotoka hospitali, kila siku kile kiwango, utakapotoka hospitali  kwa siku ulizolazwa hospitali, utakapotoka hospitali  upate pesa itakayokurudisha katika biashara, inaitwa “Hospitalization Cover” kwa kiingereza.

Kwa hiyo zipo Bima nyingi zimeanza kutoka za watu wa kipato cha chini. Nyingine ni Bima ya kilimo, sasa hivi kuna makampuni matano ya Bima, yameingia katika kuuza bima kwa wakulima. Umeenda kulima shamba, na ulipokwenda kulima shamba, dalili zote zilionyesha kwamba mvua itanyesha, na ukapanda mbegu. Mvua ya kwanza ikanyesha, ya pili pengine nayo ikanyesha, lakini ya tatu na ya nne ya kukuzia zile mbegu, haikuja. Kwa hiyo yale mahindi kama yalikuwa yameanza kuota yamefika mahali paku…Sasa utafanyaje!. Na wewe ulikuwa umeingiza pesa katika kulima. Umekwenda kununua mbegu, umeweka mbolea, nguvu zako na mategemeo yalikuwa pale.

Kwa hiyo mbinu ya namna hiyo sasa imeingia tayari katika soko. Kwa hiyo hii ndiyo tunaonyesha kwamba, bima inaanza sasa  kusaidia ukuaji wa uchumi na kufuta umasikini. Ukweli ni kwamba watu wachache wana elimu ya Bima, na hili huwezi kumlaumu yeyote kwa sababu mitaala ya ufundishaji katika mashule na katika vyuo, hata chuo kikuu, ni watu wachache sana wanakumbana na elimu ya mipangilio ya  fedha, inaitwa “Financial Planning”. Watu wachache sana wana uelewa wa mambo ya fedha, na ni elimu yetu ndivyo ilivyo, si Tanzania tu, ee..ni Duniani…ee.. I mean, tuseme Afrika, huko Ulaya wamesha rekebisha rekebisha mitaala, watoto wadogo wanaelewa ee….masuala ya kununua, kwa mfano “Shares” (hisa) ee….Katika makampuni, wanafundishwa habari ya Bima, na Bima wanaiona nyumbani kwao ikifanyika.

Mfano nchi kama za wenzetu zilizoendelea, hakuna mtu anayekwenda kutibiwa hospitali kwa fedha, kwa hiyo tangu mtoto anapokuwa na miaka miwili anamsikia mama yake ndani ya nyumba  anauliza , “Kadi yangu ya matiabu ya hospitali ya bima iko wapi”, haulizi, “Fedha iko wapi”. Sasa elimu ya namna hiyo, ee…kule ulaya kwa mfano, ee…, hakuna mtu ambaye ananunua kitu, ee… na mafeedha…..amebeba  mfuko wa fedha kwenda kununua……ni fedha  ni ndogo anabeba fedha kidogo tu kununua gazeti na mahitaji madpogomadogo.

Watu wanatumia kadi, au sio, sasa huku kwetu, elimu hiyo ndiyo inaingia. Kwa hiyo elimu ya mambo ya fedha, huku kwetu, bado iko chini sana!  Na sisi tumeona kwamba pamoja na huduma nzuri ya Bima, ambayo inatakiwa Watanzania waweze kuipata, hawaipati”.

0 Response to "BIMA NA ELIMU YA MIPANGILIO YA PESA: NI WATU WACHACHE SANA WENYE UELEWA"

Post a Comment