Dk. Mengi ataka muda kuboresha elimu | JIFUNZE UJASIRIAMALI

Dk. Mengi ataka muda kuboresha elimu


  NA MOSHI LUSONZO.

Mwenyekti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi (kulia), akizindua kitabu cha mashairi kwa lugha ya Kiingereza chenye kichwa cha habari `Ndege anayeimba jina langu`.


Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, amewataka wananchi kuwa wavumilivu katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo la kushuka kwa kiwango cha elimu nchini, kutokana na kazi hiyo kuwa ngumu.

Dk. Mengi, alisema hayo jijini Dar es Salaam wiki iliyopita, wakati akizindua kitabu cha mashairi kiitwacho 'Ndege anayeimba jina langu, Shairi la Moyo wangu' kilichotungwa na Mtanzania Edna Hogan.

Katika uzinduzi huo, Dk. Mengi, amenunua vitabu vyenye thamani ya Sh. Milioni 51 kwa ajili ya shule 30 katika mikoa mbalimbali nchini.
Alisema kazi ya kufanya marekebisho msingi wa elimu wa nchi, unahitaji muda kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu na maslahi ya walimu kuanzia shule za awali, msingi, sekondari na vyuo vikuu.

Dk. Mengi alisema kwamba matokeo ya kazi hiyo yanaweza kuonekana kati miaka 21 hadi 25 kulingana na kasi ya utekelezaji wake.

"Kitu muhimu lazima tukubali kuchukua muda katika kuboresha elimu yetu ambayo imepoteza muelekeo, huwezi kukurupuka tu kuanza kuboresha shule za sekondari wakati shule za msingi zipo taabani, kwani wakifanya hivyo watazalisha wanafunzi wachovu watakaokwenda kwenye shule na vyuo," alisema Dk. Mengi.

Aliitaka serikali kuacha kuwapa ajira walimu wasio na sifa na walio kwenye ajira wafanye utambuzi maalum ili kutambua uwezo wao wa ufundishaji.
\"Nchi ya Finland imefanikiwa kwa kuijenga sekta ya elimu, kiasi ambacho kwa sasa walimu ndiyo kada pekee inayolipwa mshahara mkubwa," aliongeza.

Alimpongeza mtunzi wa kitabu hicho pamoja na Taasisi ya Camara kwa kuchukua hatua ya kuzindua kitabu hicho na kuendesha uchangiaji wa upatikanaji wa kompyuta mpakato kwa baadhi ya shule nchini.

Awali, Hogan alisema kitabu hicho cha mashairi kimelenga kutoa ufahamu na kufundisha watu mbalimbali, hasa wanafunzi katika kukabiliana na masuala mbalimbali ya maisha.

Alisema kitabu hicho chenye kurasa 130 kilichoandikwa kwa lugha ya Kiingereza kimehakikiwa na kupitiwa na wasomi na wanataaluma maarufu nchini na kizuri kutumika katika shule za sekondari.  









CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

0 Response to "Dk. Mengi ataka muda kuboresha elimu"

Post a Comment