BIASHARA NDOGONDOGO ZA KUFANYA DAR ES SALAAM KWA MTAJI KIDOGO BILA KULIPIA PANGO LA NYUMBA | JIFUNZE UJASIRIAMALI

BIASHARA NDOGONDOGO ZA KUFANYA DAR ES SALAAM KWA MTAJI KIDOGO BILA KULIPIA PANGO LA NYUMBA

Hakuna kitu kinachomkwamisha mjasiriamali mdogo kama mtaji, jijini Dar es salaam kuna watu wengi wanaoishi kwa kufanya biashara ndogondogo ambazo kwa haraka haraka mtu unaweza ukajiuliza watu hao ni kwa namna gani huweza kupata faida wakaendesha maisha yao na hata wengine kuishia kukuza mitaji yao na kufikia hatua ya kuanzisha biashara kubwa kubwa au za kati. Kitu kingine cha kushangaza zaidi ni kuwa nyingi ya biashara hizo wala hazihitaji gharama kubwa kama za kulipia pango la fremu ya biashara au kukata leseni na kulipia kodi ya mapato.


Biashara ya nguo za mitumba na kutembeza vitu huhitaji mtaji kidogo kuanzisha.
Biashara za namna hii wengi huziita sekta isiyokuwa rasmi, umachinga au biashara ambazo bado hazijarasimishwa. Kuna faida na hasara za kufanya biashara za namna hii lakini kwa mfanyabiashara mwenye mtaji kidogo yeye hawezi kuangalia hasara zake, huangalia faida zake tu kutokana na sababu kwamba hata ikiwa angetaka kufanya biashara iliyokuwa rasmi kikwazo cha mtaji wa kutosha kuanzisha ni lazima kingemzuia.


Mtaji kwa ajili ya kuanzisha biashara nyingi ndogo siyo mkubwa sana, zipo zinazoweza kuanza mpaka na shilingi elfu tatu, elfu 5 na kuendelea, itategemea ni biashara ya aina gani mtu anataka kuanzisha. Moja ya faida kubwa ya biashara za mtaji kidogo ni huo urahisi wa kupata mtaji. Mjasiriamali hana kazi kubwa ya kuanza kuzunguka mabenki au kwa wakopeshaji wengine wakiwemo vyama vya kuweka na kukopa, saccos au ndugu jamaa na marafiki ili kujipatia mtaji wa kuanzisha biashara.

Biashara nzuri yenye mtaji mdogo siyo lazima mtu kuwa na eneo kubwa wala eneo lenye watu wengi sana ndipo aanzishe, mjasiriamali anaweza kuwapelekea bidhaa/huduma popote kule wateja walipo, wapo wengine kama mama huyu hapa, mama mwakipesile niliyemkuta kwenye gari akiuza viungo mbalimbali vya chain a masala kama mdalasini, tangawizi, mchaichai, asali mbichi, mlonge nk.


Kama unapita maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es salaam muda wa jioni utakutana na wafanyabiashara wengi wanaofanya biashara hizi zisizokuwa rasmi kandokando ya barabara, stendi za mabasi, na barazani mwaa nyumba wanamoishi watu. Kimsingi haya ni maeneo ambayo mara nyingi huwa hawayalipii chochote na hata kama hulazimika kulipia basi ni ushuru kidogo sana ambao hauwezi ukaathiri kwa kiasi kikubwa faida wanayoipata.


Ubaya au hasara ya miradi ya aina hii ni kutokuwa na uhakika, kwani maeneo yanayotumiwa mara nyingi kama ni biashara inayotakiwa kupangwa mahali kama barabarani na stendi za mabasi, maeneo hayo utakuta serikali haitaki watu kuyatumia kwa biashara. Serikali hudai wanaharibu mpangilio wa mji na kweli ikiwa ingeruhusu kiholela watu kutumia eneo lolote hata pale nje ya ikulu ungekuta watu wanapanga biashara.
Wafanyabiashara ndogondogo jijini wakiuza bidhaa zao mitaani.
Ili mjasiriamali kukwepa kikwazo hiki cha marufuku ya serikali anapaswa kuwa mbunifu zaidi kwa mfano, kupanga biashara yake muda ambao serikali haihangaiki na mtu kama masaa ya jioni, kubuni biashara isiyochukua eneo kubwa kwa mfano biashara ya kuuza kadi/vocha za mitandao ya simu za mkononi pamoja na kuuza biashara zile mtu unazoweza kuzunguka nazo kwenye begi au mfuko wako kama viungo, nguo, viatu na bidhaa ndogondogo.

Biashara ndogo ndogo unazoweza kufanya Dar kwa mtaji mdogo sana pasipo hata kulipa pango la fremu ya biashara.

Orodha ya baadhi tu ya biashara hizo ni hii ifuatayo, ila na wewe ndugu msomaji unaweza ukaongeza na za kwako kwani zipo nyingi;
  • Biashara ya kuuza vyakula, baba na mama lishe.
  • Biashara ya kuuza mahindi ya kuchoma au ya kuchemsha
  • Biashara ya kuuza mihogo ya kukaanga au ya kuchoma
  • Biashara ya kuuza mishikaki
  • Biashara ya kuuza vitu vya kutafuna kama karanga, ubuyu, kashata, miwa nk
  • Biashara ya kuuza mihogo mibichi na nazi za kutafuna kwa njia ya kutembeza mitaani.
  • Biashara ya kuuza matunda kama maembe, machungwa, matango, mananasi na mafenesi.
  • Biashara ya kuuza vocha na line za mitandao ya simu mbalimbal.
  • Biashara ya kuuza vyombo na vitu vya majumbani.
  • Biashara ya kuuza viatu na nguo za mitumba
  • Biashara ya kuuza maji baridi, soda na juisi.
  • Biashara ya kuuza samaki
  • Biashara ya kuuza uji
  • Biashara ya kuuza mandazi, chapatti, kalimati, ufuta, vitumbua, mikate, skonzi, sambusa na visheti
  • Biashara ya kuuza vifaa vya umeme
  • Biashara ta kuuza nyama za kuku za kukaanga
  • Biashara ya kuuza urembo
  • Biashara ya kutembeza rangi za kupaka kucha na kusafisha
  • Biashara ya kusuka rasta za kimasai chini ya mti
  • Biashara ya kuuza juisi ya miwa kwa mashine ya kuzungusha kwa mkono
  • Biashara ya kuuza maji ya kufunga(Kandoro)
  • Biashara ya kuuza sigara za rejareja
  • Biashara ya kuuza karanga nk.

Biashara hizo nyingi kama nilivyotangulia kusema, hazijapewa ruhusa rasmi  na serikali hasahasa maeneo zinakofanyikia. Lakini kwa mjasiriamali anayetafuta kujikwamua kwa lengo la kupata mtaji wa kuanzia hana budi wakati mwingine kujikuta anakiuka sheria, hata hivyo serikali sasa inaonyesha ina nia ya thati kuhakikisha maeneo mengi yakutosha yanaandaliwa kwa ajili ya wajasiriamali wadogo wasiokuwa na mitaji ya kutosha au hata wenye mitaji midogo sana kama ya kuanzia shilingi elfu 10 nao kupata mahali pazuri pakufanyia biashara zao.
 ...................................................................................................

Ndugu msomaji, napenda kuchukua nafasi hii kukujulisha juu ya kuanzishwa Darasa la Michanganuo ya biashara ambalo linaendeshwa mtandaoni katika blogu ya MICHANGANUO YA BIASHARA. Unapojiunga na darasa hili unajifunza kila kitu kuhusiana na mipango ya biashara kuanzia namna ya kuandaa mpaka michanganuo yenyewe halisi.

Kiingilio mtu anapaswa kununua kitabu cha MICHANGANUO NA UJASIRIAMALI ambacho ni shilingi 10,000/= Unatuma fedha na Email yako ya GMAIL kisha tunakutumia kitabu pamoja na kukuunganisha na blogu hiyo utakayoweza kuingia na kujifunza kozi hiyo.

Kwa maelezo zaidi kuhusu darasa hilo fungua hapa(Tanzania Online School Of Business Planning)

Vilevile vitabu vyetu vingine, kama MIFEREJI YA PESA NA SIRI MATAJIRI WASIYOPENDA KUITOA na SIRI YA MAFANIKIO YA BIAHSRA YA REJAREJA,  vipo na ukihitaji tunakutumia pia kwa email.


SIMU: 0712 202244   AU  0765 553030     Peter Augustino Tarimo

2 Responses to "BIASHARA NDOGONDOGO ZA KUFANYA DAR ES SALAAM KWA MTAJI KIDOGO BILA KULIPIA PANGO LA NYUMBA"

  1. Kaka nimependa kweli umelenga watu wenye kipato kidogo sana na hata umeonyesha njia kabisa za kufanya.
    ila website bado haina muonekano wa kuvutia ukipata msaada wa template nzuri utafanya watu wengi zaida wavutiwe
    elisante Shibanda.
    Tech blogger ecltech.blogspot.com

    ReplyDelete
    Replies
    1. Asante sana Elisante kwa ushauri na pongezi,kuhusu template nitawatafuteni.

      Delete