PUNDE KABLA HUJAKATA TAMAA YA MAISHA SOMA VITU HIVI 4 UTABADILI NIA | JIFUNZE UJASIRIAMALI

PUNDE KABLA HUJAKATA TAMAA YA MAISHA SOMA VITU HIVI 4 UTABADILI NIA

Ndugu msomaji natumaini hapo ulipo unasonga mbele licha ya vikwazo vya hapa na pale ambavyo vinaweza kukukatisha tamaa katika safari yako ya kuelekea maisha mazuri yenye mafanikio. Makala hii ni maalumu kwa kukutia moyo endapo labda utafika mahali na kudhani kwamba kila kitu hakiwezekani, ukakata tamaa na kufikia hata hatua ya kujidhuru.

SOMA: MAMA HUBEBA MTOTO TUMBONI MIEZI 9 LAKINI HUMBEBA MOYONI MILELE.

Kama mjasiriamali, kuna vitu 4 vinne muhimu sana ambavyo unaweza ukavitumia na ikawa ndiyo dawa itakayokomesha kabisa hali ya kukata tamaa inayoweza kukusababisha usiweze kuyafikia malengo yako unayojiwekea maishani. Ipo mifano ya watu wengi waliovitumia na wakaweza kufanikiwa.

IMANI.
Chochote kile ukifanyacho ni lazima kwanza uamini kwamba kitu hicho kitawezekana hata kabla hujatekeleza. Imani hiyo ndiyo iliyokuwa muhimu na ndiyo nguvu itakayokuchochea wewe kutimiza hilo unalolipanga kufanya. Mfano mzuri kabisa na uliokuwa wazi ni imani za dini na madhehebu mbalimbali. Waumini wake pamoja na kwamba hawana ushahidi wa moja kwa moja kuwa kuna maisha baada ya kifo, lakini IMANI huwafanya waendelee kusadiki hivyo bila kuchoka.

SOMA: UPENDO WA WAZAZI HAUNA MIPAKA, NI "UNCONDITIONAL LOVE"

SUBIRA.
Ni mara ngapi umewahi kukata tamaa na kusita kufanya jambo fulani, kumbe mafanikio yake, ulibakia muda kidogo sana uyapate? Katika sura ya kwanza 1 ya kitabu “Fikiri Utajirike(Msahafu wa mafanikio)” Kuna simulizi moja maarufu ya mchimba madini aliyejulikana kama Darby, huyu jamaa baada ya kupata habari kuwa yameibuka machimbo ya dhahabu eneo moja huko Magharibi mwa Marekani, (kama ilivyokuwa hapa kwetu, machimbo ya Tunduru na kwingineko kama Samunge) basi bwana huyu akazunguka kwa kila ndugu na jamaa kukopa mtaji aende kubahatisha bahati yake mgodini ikiwa ni pamoja na kuuza kila kitu chake cha dhamani kusudi tu apate mtaji.

Darby alianza kazi ya kuchimba dhahabu kwa matumaini makubwa lakini baada ya muda kupita na kuona hamna mafanikio makubwa haraka, alikosa subira, akakata tamaa na kuamua kumuuzia dalali mmoja wa vyuma ule mgodi, yeye akarudi zake mjini. Madalali kama iulivyokuwa kawaida yao ni wajanja mno kwenye pesa!, alimtafuta injinia(mhandisi wa madini) akaomba ushauri. 

Injinia baada ya kupima pima alimwambia bamba la dhahabu lilikuwa futi tatu 3 tu! kutoka pale Darby alipoachia kuchimba baada ya kukata tamaa. Kilichofuata baada ya hapo ndugu msomaji wangu nadhani unaweza kubashiri mwenyewe. Unaweza ukakisoma kisa/simulizi hiyo vizuri kwa kubonyeza maandishi yafuatayo, Futi tatu tu, kutoka dhahabu ilipo!

UVUMILIVU.
Kama ilivyokuwa Subira, uvumilivu nao kwenye maisha unahitajika sana. Mchimba dhahabu bwana Darby, hakuwa navyo vyote viwili, uvumilivu na subira. Kuna kisa kingine cha kweli katika kitabu hichohicho. Bila shaka katika nyumba unamoishi, kila siku usiku ni lazima uwashe taa ya umeme au balbu. Unajua mgunduzi wa taa hiyo, Thomas Edson alijaribu mara ngapi kabla hajaigundua?. Alijaribu mara 9,999 ya 10,000 ndipo alipofanikiwa! Ungelikuwa ni wewe ungeliachia wapi?, Kwa upande wangu nafikiri hata mara ya 20 nisingefikisha.

Na isitoshe Edison mwenyewe alipohojiwa alikuwa anajisikiaje kufeli mara zaidi ya elfu 9, alijibu hivi; “Nafurahi nimegundua njia 9,999 zisizofaa kugundua balbu”

MUDA. 
Muda ndiyo kiunganishi katika hivyo vitu vingine vyote vitatu, Imani, Uvumilivu na Subira katika safari ya mtu kupata mafanikio. Hakuna mafanikio yanayoweza yakapatikana ndani ya kipindi kifupi kama siku moja, mbili, au tatu labda iwe ni kamari. Yanahitaji muda wa kutosha, hata unapopanda mazao kama vile mahindi huwezi ukategemea kuyavuna kabla ya muda wake kutimia. Watu wengi hukatishwa tamaa wanapofikiria muda waliokwisha upoteza kwenye miradi/shughuli fulani lakini wanashindwa kukumbuka kuwa mafanikio yeyote yale yanahitaji muda kuyatimiza na muda wenyewe ni lazima uwe wa kutosha.

SOMA: NI UA ZURI NA HATARI SANA!, LINA UWEZO WA KUUA MTOTO HARAKA.

Mafanikio ya aina yeyote yale unayojaribu “kuyapika” katika maisha yako ya thamani hapa duniani, hakikisha viungo hivi vinne, IMANI, SUBIRA, UVUMILIVU NA MUDA havikosekani katika “chungu unachotumia kuchemshia mafanikio hayo.” Na hasa hasa Imani, kwani ikiwa kama hauta amini kwa thati kabisa kuwa unalolitaka liwe litakuwa, basi sahau mafanikio kabisa.

Mwisho, usikate tamaa kamwe, jipe tena nafasi nyingine ya kujaribu na inaweza ikawa ndiyo mara yako ya 10,000 kama ilivyokuwa kwa Thomas Edison, mvumbuzi wa glopu ya umeme.

Nakutakia kila la heri katika safari yako ya kutimiza malengo uliyojiwekea maishani na kama bado hujajiweka malengo ama hufahamu jinsi ya kujiwekea malengo mazuri, basi nakushauri ujipatie kitabu hiki kilichobadilisha maisha ya watu wengi waliobahatika kukisoma. Bonyeza maandishi yafuatayo kupata kitabu hicho; “MIFEREJI YA PESA NA SIRI MATAJIRI WASIYOPENDA KUITOA”

Mwandishi na Mhamasishaji wako;

Peter A. Tarimo. 

0 Response to "PUNDE KABLA HUJAKATA TAMAA YA MAISHA SOMA VITU HIVI 4 UTABADILI NIA"

Post a Comment