WATEJA HUPENDELEA URAHISI | JIFUNZE UJASIRIAMALI

WATEJA HUPENDELEA URAHISI


Wateja hupendelea urahisi, ninaposema urahisi simaanishi bei , bali wepesi katika kupata bidhaa au huduma , pasipokuwa na milolongo, usumbufu na ukiritimba usiokuwa na maana

Naandika mada hii kutokana na uzoefu wangu binafsi katika biashara zangu hususani  hii ya vitabu. Wakati tukiuza vitabu vya ‘MIFEREJI 7 YA PESA’ tuliamua pamoja na kuuza vitabu vya kawaida vilivyochapwa katika karatasi vilevile tuuze kwa njia ya mtandao (online) nikiwa namaana, tunamtumia mteja kitabu kikiwa katika mfumo wa faili la PDF kupitia  E-mail (barua pepe) yake na kisha yeye ‘hudownload’ na kukisoma hapohapo au hata kukihifadhi katika hard disk, flas, cd nk. kwa ajili ya kukisoma baadae. Hii lakini ni kwa yule mteja mwenye uwezekano wa kupata intaneti tu.

Uamuzi huu, ulinishangaza! Wateja wengi na kutoka sehemu mbalimbali nchini  walitupigia simu wakitaka watumiwe kitabu kwa njia hiyo. Kaka mmoja jina lake la mwanzo Rajab, wa Tarime hakuamini kama kweli baada ya kutuma sh. 3,000/ kwa njia ya M-pesa angeweza kukisoma kitabu katika muda usiozidi dakika 5. Aliniambia mwanzoni alikuwa na wasiwasi labda ni matapeli wa mtandaoni.

Niligundua kitu kimoja, wateja hawapendi shida, hupendelea bidhaa au huduma  waipate katika hali ya kuvutia, upatikanaji wake uwe rahisi na usiokuwa na vikwazo. Kadiri utakavyoifanya biashara yako kuwa rahisi kupatikana ndivyo na wateja nao watakavyokuwa wengi, hali kadhalika na wewe ndivyo utakavyojipatia fedha zaidi.


Urahisi hautumiwi  katika biashara ya vitabu tu peke yake kama nilivyotolea mfano kwa upande wangu, ni katika kila biashara. Wateja katika biashara ya aina yeyote ile, hiyo ni tabia yao. Uwe unauza karanga, ubuyu, maji, supermarket, au chochote kile, hakikisha bidhaa/huduma zako, mteja anakuwa na urahisi katika kuzipata.

0 Response to "WATEJA HUPENDELEA URAHISI"

Post a Comment