MAAJABU KIFO CHA MTOTO WA KWENYE BOKSI KUMBE ALIKUWA "NABII WA MUNGU" | JIFUNZE UJASIRIAMALI

MAAJABU KIFO CHA MTOTO WA KWENYE BOKSI KUMBE ALIKUWA "NABII WA MUNGU"

Siku ya leo Jumapili tarehe 1/6/2014 kwangu binafsi ilianza vizuri tu asubuhi, huku mawazoni nikitafakari mambo mbalimbali yahusuyo maisha yangu kwa ujumla. Lakini ilipotimu majira ya jioni ghafla hali ilibadilika pale niliposikia redioni kwamba yule mtoto Nasrah Rashid  aliyeishi ndani ya boksi kwa takriban miaka minne ameaga Dunia! 

Naandika makala hii ningali na simanzi kuu machozi yakinilengalenga. Amefia Hospitali ya Taifa Muhimbili baada ya madaktari kuhangaika naye usiku na mchana wakitaka kuyaokoa maisha yake pasipo mafanikio. Najaribu kupata picha ya jinsi mtoto huyu (Malaika) asiyekuwa na chembe ya dhambi jinsi alivyokuwa akiishi gizani ndani ya boksi pembeni kukiwa na dimbwi la maji machafu, sielewi shimo hili lilikuwa la kazi gani.

Kwa kifupi hajawahi kuonja upendo na furaha tangu amezaliwa kutokana na kuzaliwa mama yake angali mgonjwa na hatimaye kufa  isipokuwa tu katika zile siku  chache za mwisho wa uhai wake baada ya wasamaria wema kuja kumuibua ‘shimoni’. Ameondoka na kutuacha kila mtu tukitamani kumpa upendo, ni kama vile amesema, “Kwani mlikuwa wapi siku zote hizo nikipata mateso yasiyomithilika wala kulingana na umri wangu?”

Haya ni matokeo ya binadamu wa siku hizi kutokujali tena hata pale tunapoona kiumbe kama kile kikiteseka. Bila shaka majirani na hata watu wa karibu, ndugu na jamaa wa marehemu mama wa mtoto huyu, ni lazima walifahamu kuteseka kwake kitambpo tu lakini kwa kuwa hakuwahusu sana wakaamua “kupotezea” mpaka mambo yalivyokuja kuwa magumu zaidi ndipo wakaamua kutoa taarifa.

Hivi jamani nauliza mtoto huyu alikuwa halii hata majirani wasisikie? Ni maumivu kiasi gani mtoto huyu alikuwa akiyahisi ndani ya akili yake change? Akili yake ilikuwa ikifikiria nini? Alikuwa anahisi uchungu na mateso au labda alikuwa akiona ni maisha ya kawaida tu? Akili yake ilitambua kuwa alikuwa akiteswa?

Hakika MWENYEZI Mungu ni wa ajabu! Nasema hivyo kwa sababu, mtoto huyu aliweza kuishi kwa muda huo wote ndani ya boksi hilo katika hali ya mateso yote hayo pasipo kufa. Swali jingine ninalojiuliza ni kama alikuwa akiugua  homa kwa kipindi chote hicho, na kama alikua akipatwa na homa basi alikuwa akipona vipi bila matibabu? Nijuavyo mimi kwa kipindi chote hicho kwenye mazingira duni namna ile ilitosha kabisa kuondoa uhai wake tena mapema kabisa.
 
Mtoto Nasrah Rashid aliyeishi ndani ya boksi kwa miaka 4 akiwa amebebwa na baba yake enzi za uhai wake.  
Hebu kama wewe ni mzazi jaribu kufikiria ni mara ngapi umewahi kumpeleka mwanao mwenye umri kama huo hospitalini hata kutokana na malaria tu au kikohozi sembuse Neumonia?
Huenda MUNGU alikuwa na makusudi ya kuuthihirishia umma  mateso makali wanayotendewa watoto wadogo Tanzania nap engine Duniani kwa ujumla kupitia mtoto huyu. Ndiyo maana hakutaka kumchukua mapema, alisubiri aje agunduliwe na wasamaria habari zimfikie kila mtu ndipo sasa amchukue kiumbe wake.

Nakumbuka jinsi nilivyomuona katika vyombo vya habari siku alipookolewa na siku zilizofuata, alionekana mzima tu ijapokuwa alikuwa amedhoofika sana. Hata wandishi wa habari walipojaribu kuzungumza naye, aliweza kujibu vizuri tu na kutia matumaini, aliweza kuzungumza sentesi chache kama vile “Napenda chipsi” nk.

Ina maana kwamba kama asingegunduliwa na akaendelea kuishi mle “jehanamu”(kwenye lile boksi) pengine wiki ile ile ndiyo ingelikuwa mwisho wa maisha yake. Ina maana alikuwa karibu kufa kiasi hicho? Sijui, ndiyo maana nasema hili lilikuwa kusudi la Mwenyezi Mungu mwenyewe kufikisha ujumbe wa kilio cha watoto wadogo kwa Wanadamu wa Ulimwengu huu dhalimu.

Mtoto huyu namfananisha na Nabii, ni kama vile alitumiwa na Mungu  kuwakilisha watoto wenzake kote Duniani na hususan Tanzania wanaopata mateso makali, siyo kutoka kwa watu baki bali bali ni kutoka kwa wale watu wanaostahili kuwa walezi wao, kama vile Baba wadogo, mama wadogo, mama na baba wakubwa, shangazi, mjomba, binamu, bibi, babu na hata wazazi wao wenyewe wa kuwazaa kama ilivyowahi kutokea kwa baadhi ya wazazi waliodiriki kuwatoa watoto wao wenye ulemavu wa ngozi (Albino) kwa wauaji, kisa tu, tamaa ya kupata pesa na utajiri wa haraka haraka.

Mateso ya Nasra yawe chachu ya mapambano dhidi ya mateso ya watoto wengine wadogo wasiokuwa na hatia wanaopata mateso kama hayo. Mungu ailaze Roho yake mahali pema peponi Amina.

Picha na global publishers



0 Response to "MAAJABU KIFO CHA MTOTO WA KWENYE BOKSI KUMBE ALIKUWA "NABII WA MUNGU""

Post a Comment