SIMBA KULIPA FAINI SHILLINGI LAKI 5 VURUGU ZA MASHABIKI MECHI DHIDI YA KAGERA SUGAR | JIFUNZE UJASIRIAMALI

SIMBA KULIPA FAINI SHILLINGI LAKI 5 VURUGU ZA MASHABIKI MECHI DHIDI YA KAGERA SUGAR

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPL Board) imefungia viwanja saba vilivyokuwa 
vikitumiwa na timu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) hadi vitakapofanyiwa marekebisho ili kukidhi mahitaji ya mechi za mpira wa miguu.


Uamuzi huo umefikiwa na TPL Board katika kikao chake cha kwanza kilichofanyika juzi (Novemba 10 mwaka huu) jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine kilipitia ripoti za mechi za VPL na FDL katika mzunguko wa kwanza.

Viwanja vilivyofungiwa na marekebisho yanayotakiwa kufanyika kwanza ili viruhusiwe kutumika tena ni Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba (majukwaa yake yamechakaa, hivyo kuhatarisha usalama wa watazamaji), na Uwanja wa CCM Mkwakwani jijini Tanga (vyumba vya wachezaji kubadilishia nguo (dressing rooms) havina hadhi).


Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya (sehemu ya kuchezea- pitch ni mbovu), Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha (pitch ni mbovu), Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi (vyumba vya kubadilishia kutumika kwa ajili ya shule ya awali), Uwanja wa Majimaji mjini Songea (pitch ni mbovu) na Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro (pitch ni mbovu).

Klabu ambazo timu zake zinatumia viwanja hivyo zimeshaarifiwa rasmi juu ya uamuzi huo ambapo ama vinatakiwa kuwasiliana na wamiliki wa viwanja hivyo ili wafanye marekebisho au kutafuta viwanja vingine vya kuchezea mechi zao.

Kwa upande wa ripoti za mechi za VPL; Mbeya City imepigwa faini ya sh. 500,000 na kupewa onyo kali kwa timu yake ya U20 kutocheza mechi ya utangulizi walipocheza na Yanga. Pia wanatakiwa kulipa gharama za uharibifu baada ya washabiki wao kuvunja kioo cha basi la Yanga baada ya gharama hizo kuthibitishwa na Bodi ya Ligi.

Pia Mbeya City imepigwa faini ya sh. 500,000 kwa washabiki wake kushambulia basi la wachezaji wa Tanzania Prisons baada ya mechi dhidi yao, na kulipa gharama za uharibifu baada ya kuthibitisha na Bodi ya Ligi.

Coastal Union imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake ilipocheza na Azam kwenye Uwanja wa Mkwakwani ambapo mwamuzi msaidizi Hassan Zani alishambuliwa kwa mawe na kujeruhiwa mkononi na kichwa, tukio lililosababisha mchezo kusimama kwa dakika tatu.

Beki wa Coastal Union, Hamad Khamis wa Coastal Union amepigwa faini ya sh. 500,000 kwa kumpiga kichwa kwa makusudi Kipre Tchetche wa Azam. Kitendo hicho kilisababisha refa amtoe nje kwa kadi nyekundu, hivyo atakosa mechi tatu zinazofuata za timu yake.

Mchezaji Cosmas Lewis wa Ruvu Shooting alifanya kitendo cha utovu wa nidhamu kwa kupiga kelele wakati mgeni rasmi akisalimia timu na kukataa kupeana mkono na kamishna kwenye mechi dhidi ya Rhino Rangers, hivyo amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 500,000.

Mtunza vifaa (Kit Man) wa JKT Ruvu, Selemani Oga aliondolewa kwenye benchi la ufundi wakati wa mechi yao dhidi ya Mbeya City kwa kosa la kutoa lugha chafu kwa refa, hivyo suala lake litapelekwa katika Kamati ya Maadili.

Kocha Msaidizi wa Oljoro JKT, Fikiri Elias amepigwa faini ya sh. 500,000 na kufungiwa mechi tatu kwa kumshambulia kwa matusi refa wakati wa mechi yao dhidi ya Ashanti United. Naye mtunza vifaa wa timu hiyo Elas Justin amepelekwa Kamati ya Maadili kwa kumshambulia refa kwa matusi ya nguoni.

Simba wamepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake wakati wa mechi dhidi ya Kagera Sugar.SOMA HABARI HII ZAIDI HAPA TOVUTI YA SHAFII DAUDA

0 Response to "SIMBA KULIPA FAINI SHILLINGI LAKI 5 VURUGU ZA MASHABIKI MECHI DHIDI YA KAGERA SUGAR"

Post a Comment