MSICHANA ALIYEJALIWA UWEZO WA AJABU WA KUIMBA MASHAIRI | JIFUNZE UJASIRIAMALI

MSICHANA ALIYEJALIWA UWEZO WA AJABU WA KUIMBA MASHAIRI

Na Jafary Ahmed(Jefryder)

Napenda kuimba na kila nionapo au kusikia  mtu akiimba , huwa “automatically nakuwa attention” kutaka kufahamu, ni nani na anaimba nini.
Amina Hassan

Nimewahi kumuona akipita njiani hasa maeneo ya Buguruni huku akiimba(akighani) mashairi  matamu, hunikumbusha enzi zile Redio Tanzania, RTD sasa TBC walipokuwa na vipindi vya kughani mashairi. Kila nilipokuwa nikimuona  nilikuwa najiuliza maswali mengi juu ya huyu dada, moja likiwa, ni kwa nini huwa anaimba mtaani, na ikiwa kama kipaji chake hiki amewahi kujitangaza mahali popote pale. Nilinuwia kwamba iko siku moja lazima nimuite na kumuuliza.

Leo nilipomuona tu akipita kama kawaida yake akiimba mashairi, sikuweza kujizuia na kwa kuwa alikuwa akipita karibu kabisa na kazini kwangu, nilimfuata na kumuomba asogee barazani, Hakukataa akakubali. Kitu cha kwanza nilimuuliza iwapo anatoza shilingi ngapi kwa shairi moja akanijibu ni shilingi 500/-Sikuchelewa nikamwambia aanze mara moja, naye hakukawia akaanza. Ile sauti kama ya Tausi, kidogo kidogo ikaanza kuwakusanya majirani walioisikia mpaka wakajaa tele! Angalia video chini akiimba,



Baada ya kuimba ndipo na mimi nikamuomba anijibu maswali yangu niliyokuwa nikijiuliza kila siku. Alilitaja jina lake kuwa ni Amina Hassan na kwamba alianza kughani mashairi siku nyingi, hakumbuki ni lini lakini anasema ni tangu akiwa mtoto  na wala hakuna mtu aliyemfundisha bali alikuwa akipenda sana kusikiliza kipindi cha mashairi redioni, na ndicho kilichomvutia na yeye kutunga na kuimba. Video hapa chini akieleza,



Ameniambia kwamba amewahi kupelekwa pale karibu na Tazara, akimaanisha redio ya Taifa TBC  na marehemu Halima Mchuka kupitia kwa Muhidin Maalim Gurumo, akafanyiwa mahojiano, lakini pamoja na kuonekana  kuwa anacho kipaji kikubwa, kikwazo cha yeye kuweza kuendelezwa ama hata kushirikishwa na wasanii wakubwa kilikuwa ni tatizo lake la kiafya  linalomsumbua.

Nilimuomba ataje ni tatizo gani, akasema huwa akikaa kwenye msongamano wa watu mara nyingi anapatwa na ugonjwa wa kuanguka, lakini tatizo hili anasema halimzuii kufanya kazi yake hii ya kuwaburudisha watu kwani kama ilivyokuwa kwa mtu yeyote mwenye tatizo hili huwa haiwezi kumtokea kila wakati, ni ugonjwa wa kawaida kama magonjwa mengine ila tatizo ni watu kutokuelewa na kuwa na unyanyapaa.

Nilipotaka kujua Amina Hassan  anakoishi, alitaja kwamba, anaishi na wazazi wake wote wawili pamoja na ndugu zake wengine maeneo ya Uwanja wa ndege, Karakata, ukifika Karakata tu ulizia kwa KALA. Anasema hana simu ya mkononi, na mtu yeyote akitaka kuwasiliana naye anaweza kufika maeneo hayo aliyotaja na kumuulizia atampata. Video hii hapa chini akitoa mawasiliano yake.







Maoni ya mwandishi.
*Ugonjwa wa kuanguka au Kifafa kitaalamu hauwezi kuambukiza, ni ugonja unaotokana na hitilafu katika mishipa ya fahamu hasahasa katika ubongo na uti wa mgongo. Si vizuri kuwanyanyapaa wenye tatizo hili wala kuhusisha matatizo yao na maswala ya kishirikina. Tuwajali wenye ugonjwa huu na kuthamini kazi wanazozifanya kwani wanaweza kufanya kazi sawasawa na watu wengine licha ya ulemavu waliokuwa nao.

0 Response to "MSICHANA ALIYEJALIWA UWEZO WA AJABU WA KUIMBA MASHAIRI "

Post a Comment