SIRI 10 ALIZOTUMIA ALIKO DANGOTE TAJIRI NAMBA1 AFRIKA KUTAJIRIKA | JIFUNZE UJASIRIAMALI

SIRI 10 ALIZOTUMIA ALIKO DANGOTE TAJIRI NAMBA1 AFRIKA KUTAJIRIKA

Mwafrika, mtu mweusi tajiri zaidi Duniani Alhaji Aliko Dangote, biashara zake utazikuta katika nchi nyingi Barani Afrika ikiwemo Tanzania. Utajiri wake mwaka jana ulikadiriwa kufikia Dola za Kimarekani, milioni 18 “US$18.9” na utajiri huo unatokana na biashara za cementi, sukari na nafaka.

Alianza rasmi biashara miongo mitatu iliyopita baada ya kukopa fedha za mtaji kutoka kwa mjomba wake kiasi cha Naira za Kinaijeria 500,000. Mjombake huyo ambaye pia hapo kabla alikuwa amemuajiri Dangote alimpatia kiasi hicho cha fedha kwa makubaliano kuwa azirudishe baada ya miezi mitatu. Dangote aliweza kuzirejesha chini ya miezi hiyo mitatu.

Alianza na biashara ya kuuza bidhaa mbalimbali na kilichomsaidia sana ni kubuni mfumo wa usambazaji bidhaa uliokuwa wa haraka kushinda washindani wake.

Sasa basi hebu tuanze kuona zile siri 10 zilizomsaidia Dangote mpaka kufikia pale alipo leo hii, ambazo pia Dangote mwenyewe huwa hapendi kuzificha, huzisema waziwazi kila anapokuwa na fursa ya kuzungumza na watu kuhusiana na mafanikio yake.

1. Zalisha na siyo kubakia kuwa mchuuzi tu.
Aliko Dangote alianza biashara zake kama mchuuzi wa bidhaa wa kawaida  mithili ya unavyoona hapa kwetu  wafanyabiashara wakinunua bidhaa kama nguo,  mafuta, viatu na kisha kwenda kuviuza kwa faida.

Kwa kadiri alivyokuwa akikua Dangote alijipatia uzoefu mkubwa kibiashara  na hali ya kujiamini. Katika mahojiano yake na vyombo mbali mbali vya habari aliyowahi kufanya, mara nyingi hupenda kuweka bayana kwamba, mafanikio yake makubwa kibiashara yametokana na kuhama kutoka uchuuzi wa bidhaa kuwa mzalishaji wa bidhaa.

Dangote mwenyewe anasema,  “Zalisha  na siyo kufanya uchuuzi tu, kuna pesa kwenye uzalishaji , ingawa unahitajika uwekezaji mkubwa. Ili nitoke, nililazimika kuanza kuzalisha bidhaa kama zilezile nilizokuwa nikifanyia uchuuzi(nikiuza). Mimi natetea uzalishaji kwa sababu siyo tu uzalishaji unazidisha hadhi yako katika biashara, bali pia unakusaidia wewe kama mjasiriamali kurudisha kile ulichokipata kwa jamii yako na nchi kwa ujumla kwa njia ya kuongeza nafasi za kazi pamoja na maendeleo ya kiuchumi” Alimalizia Dangote.

2. Jenga jina na kamwe usiliharibu.
Hii ni siri ya pili ya mafanikio ya Aliko Dangote, Mfanyabiashara, Mnaijeria na mtu aliyekuwa tajiri zaidi kuliko mwingine yeyote yule katika Bara la Afrika. Dangote ni muumini mzuri katika “nguvu ya jina” na kifuatacho ndicho alichotamka juu yake;

“Ili ufanikiwe katika biashara, ni lazima utengeneze jina na kamwe usiliharibu. Nguvu kubwa ya kiushindani niliyokuwa nayo wakati nilipoingia ubia katika biashara ya  uzalishaji bidhaa ilikuwa ni jina langu “Dangote” ambalo nililijenga kwa juhudi kubwa katika kipindi changu chote nilichokuwa nafanya biashara ya uchuuzi wa bidhaa.”-Aliko Dangote

Hebu tuchukulie mifano ya makampuni makubwa kama vile Coca Cola na Pepsi, utakuta hata kuna wakati thamani ya majina hayo “brand names” huwa kubwa kushinda thamani halisi ya rasilimali makampuni hayo yanazomiliki. Hiyo ndiyo nguvu ya kujenga jina zuri la biashara.  Sasa kwanini na wewe leo usianze kujijengea la kwako?.

Jina lako la biashara laweza kuwa mwokozi wako katika nyakati ngumu kibiashara, linaweza pia kugeuka nguvu kubwa ya kiushindani katika biashara yako ndogo.

3.  Uza bei nafuu, zingatia ubora lakini angalia usiue ushindani.
Kujenga biashara yenye mafanikio, Dangote anasisitiza umuhimu wa kuuza bidhaa bora katika  bei nafuu. Kuuza bidhaa zilizokuwa bora katika bei ambayo kila mteja ataimudu. Husaidia katika kuongeza utiifu wa wateja. Kuhusiana na ushindani, Dangote alikuwa na haya ya kusema;

“ Usiue ushindani, ushindani ni afya kwa biashara. Unakuweka wewe mjasiriamali katika hali ya kuendelea kufanya jitihada zako zote ili kutimiza malengo.”

Mjasiriamali mwingine, na aliyekuwa mwanaviwanda, Henry Ford kwa upande wake aliwahi kusema hivi;
“Kuna kanuni moja kwa mwanaviwanda nayo ni: Tengeneza bidhaa bora kabisa kwa kadiri inavyowezekana, katika bei nafuu kabisa inayowezekana , huku ukilipa mshahara mkubwa kwa kadiri inavyowezekana.”- Henry Ford  

4.  Anza kidogo lakini ukiwa na maono makubwa.
“Niliunda makampuni na kuwa mtu mweusi tajiri zaidi duniani hapo mwaka 2008, lakini hili halikuweza kutokea kwa siku moja. Ilinichukua miaka ipatayo 30 kufikia pale nilipo leo. Vijana wa leo wanatamani kuwa kama mimi lakini wanataka kufikia lengo hilo kwa usiku mmoja. Hiyo haiwezi kufanya kazi. Kujenga biashara yenye mafanikio, ni lazima uanze kidogo na kuota makubwa. Katika safari ya ujasiriamali, ung’ang’anifu katika kuyafikia malengo ndiyo kila kitu.”- Aliko Dangote

5.  Jenga ushirikiano na tafuta ‘mpenyo mkubwa’.
Siri nyingine ya mafanikio ya Dangote ni ushirikiano kwenye biashara. Aliko Dangote anaheshika kwa mtandao wake imara wa kibiashara pamoja na ushirikiano  wa kisiasa.  Unaweza ukajenga mashirikiano na kukuza  mtandao wako wa kibiashara kwa kuongeza uwajibikaji wa kijamii, kuingia mikataba ya ubia na ushirikiano, kuunda ushirikiano/muungano wa kimkakati, kuhudhuria shughuli na mikutano ya kibiashara, kuchangia shughuli za kisiasa pamoja na kufanya ziara za kihisani.

Kudumu katika biashara, ni lazima uimarishe ushirikiano wako kibiashara pamoja na mtandao, na muhimu zaidi, ni lazima uwinde ‘mpenyo mkubwa’(big break). Mpenyo mkubwa ni muhimu mno katika uhai wa kijasiriamali. Kwa kweli ni vigumu mno kukuta mjasiriamali yeyote mwenye mafanikio ambaye hakupigwa jeki, kupitia mpenyo mkubwa(Big breakthrough).

*Mpenyo mkubwa kwa lugha nyingine ni tukio kubwa maishani lililokuwa na uwezo wa kubadilisha kabisa maisha kutoka hali duni kuelekea maisha yenye fursa nyingi zaidi
1.    Kwa mfano, Diamond Platnumz alipata mpenyo wake mkubwa pale alipopata dili la kurekodi kibao cha Mbagala, kila kitu kilibadilika kuanzia pale!
2.    Aliko Dangote alipata mpenyo wake mkubwa pale alipofanikiwa kupata leseni ya kuagiza simenti kutoka nje ya Nigeria.
3.    Halikadhalika na Bil Gates mpenyo wake mkubwa ni pale aliposaini mkataba na kampuni kubwa ya kompyuta ya IBM
4.    Je na wewe mpenyo wako mkubwa (big breakthrough) ni upi?

6.  Amini kuwa unaweza ukatajirika hata ukiwa katika nchi yako ulikozaliwa.
Dangote anaamini kabisa kuwa, ili mtu uweze kujenga biashara imara na yenye mafanikio, ni lazima uwe na imani thabiti juu ya nchi yako, uamini kwamba fursa zimejaa tele kila mahali, ila tu kinachotakiwa ni mtu awe na jicho la kijasiriamali lililokuwa na uwezo wa kuona fursa hizo pale ambapo mtu wa kawaida asingeliweza kuziona kirahisi. Anamtia moyo kila mtu kuzitafuta fursa ndani ya nchi zao na siyo kwenda kuhangaika katika nchi za watu.

7.  Fanya kazi kwa bidii.
Bidii!, bidii!, bidii, hivi ndivyo Dangote anavyosisitiza mara zote anapopata nafasi ya kuwaelezea watu siri zake za mafanikio.Hebu soma maneno yake mwenyewe hapa chini alivyosema;

Mwenyewe huwa nafurahia sana maisha lakini huwa napatwa na furaha zaidi ninapokuwa nafanya kazi. Ninaamini katika kufanya kazi kwa bidii na moja ya siri zangu za mafanikio kufanya kazi kwa bidii”- Aliko Dangote.

Ingawa Dangote hufanya kazi kwa bidii sana lakini hafanyi kazi tu ilimradi amefanya, la hasha, hutumia akili na zaidi ya yote HUPANGA kabla hajafanya kazi zenyewe. Mfano mmoja wapo ni mradi wa kiwanda cha cementi cha Dangote Mtwara, baada ya kufanya utafiti wa kutosha mwishowe aliamua kukiweka kiwanda hicho Mtwara.
Kiwanda cha cement cha Dangote Mtwara Tanzania
Ni kwa nini asingeamua kukiweka Dar es salaam, Pwani au hata Mwanza kwenye mawe mengi ambayo yangetumika kama malighafi rahisi?. Bila shaka kutokana na mipango na upembuzi yakinifu Mtwara ndiyo mahali panapofaa ili mradi/kiwanda chake kiweze kurudisha gharama zilizotumika.

8. Rudisha kile ulichokipata kwa wale waliokupatia.
Hata ungelikuwa na juhudi ya kazi vipi lakini kamwe hauwezi ukasimama na kudai eti mafanikio yako hakukuchangia mtu, wateja wenyewe wa biashara yako ni moja ya watu wanaochangia ufanikiwe. Huwezi kutajirika kwa mikono yako mwenyewe. Kuna wafanyakazi, wadau mbalimbali, wabia, taasisi, makampuni na jamii kwa ujumla wote wana mchango kwako ili ufanikiwe.

Kwa namna moja au nyingine kuna wakati ulihitaji msaada fulani na ukasaidiwa na watu/mtu fulani ndipo ukaweza kufanikiwa. Kwa hiyo basi ili waendelee kukupa ‘sapoti’ ama kukuunga mkono, huna budi kuwakumbuka kwa kuwarudishia sehemu ya kile walichokupa. Kuna njia nyingi za kuwarudishia ikiwemo, misaada ya kijamii, kufadhili shughuli mbalimbali nk. Dangote hili ameweza kulitimiza kwa asilimia kubwa sana.

9.  Heshimu na kutii sheria za nchi.
Katika hili, masuala kama ya kukwepa kodi hakuna, inatakiwa kuhakikisha sheria zote na taratibu zilizowekwa na mamlaka halali zifuatwe. Dangote hushauri wajasiriamali kuwa watu wenye kufuata sheria za nchi pasipo kupindishapindisha ikiwa nipamoja na kulipa kodi halali.

10. Ni lazima “ujasiriamali uwe ndani ya damu yako.”
Tabia za kijasiriamali ni lazima uwe nazo, na hauwezi ukafanikiwa ikiwa hautazitilia maanani na kuziishi. Haitoshi tu kuzijua kinadharia, kila kitu utakachofanya, ukifikiri, ukiota, ukifanya jambo lolote lile basi liwe ni biashara na siyo kitu kingine. Roho ya ujasiriamali utakayokuwa umeipanda kwa jinsi hiyo haitakufa kamwe hata ikiwa wewe kimwili utakuwa umekufa, yenyewe itaendelea kuishi miaka mingi baadaye.

Ni kama unavyoona wajasiriamali mfano wa kina Thomas Edison, hata baada ya kufa siku nyingi kampuni lake la General Electrics badi lipo. Andrew Carnegie kitabu chake Think & Grow Rich ni miaka zaidi ya 70 sasa na bado kinawavutia watu wengi Duniani. Hata Mzee Warren Buffet aliyewahi kuwa mtu tajiri zaidi Duniani, ingawa ameshazeeka sasa lakini bado ndani ya damu yake ujasiriamali unaendelea kuchemka. 

0 Response to "SIRI 10 ALIZOTUMIA ALIKO DANGOTE TAJIRI NAMBA1 AFRIKA KUTAJIRIKA"

Post a Comment