KUSHUKA BEI YA MCHELE, KILO MOJA HATUUZI TUNAANZIA KILO TANO (5) TU NA KUENDELEA | JIFUNZE UJASIRIAMALI

KUSHUKA BEI YA MCHELE, KILO MOJA HATUUZI TUNAANZIA KILO TANO (5) TU NA KUENDELEA


Baada ya kusikia minong’ono mingi mitaani kuwa mchele umeanza  kushuka bei katika masoko mbalimbali jijini Dar es salaam, binafsi sikukubali nikaamua kufunga safari mpaka katika maduka yanayouza mchele kwa bei za jumla na rejareja pale Mbezi mwisho ili niweze kujionea mwenywe punguzo hilo na ikibidi nijinunulie hapo kilo mbili au tatu za kwenda kula nyumbani.


Si mara yangu ya kwanza kwenda katika maduka haya kununua nafaka mbalimbali hususan mchele, maharage, mahindi, ngano, choroko, kunde na hata wakati mwingine karanga, hivyo mazingira na hata bei za nafaka hizo mbalimbali nilikuwa na aidia nazo ijapokuwa bei hubadilika mara kwa mara kulingana na soko lenyewe lilivyo katika wakati husika kama ilivyotokea wakati huu inaposemekana mchele umeshuka bei kwa sababu ya msimu wa mavuno ya mpunga kuanza katika mikoa mbalimbali ikiwemo Morogoro, Mbeya, Ruvuma Rukwa na maeneo mengine mbalimbali ya nchi ya Tanzania zao la mchele linakolimwa kwa wingi.


Na hata maduka mengi pia nayafahamu vizuri. Kuna duka moja huwa napendelea kununua mara kwa mara kutokana na bei zao kuwa rahisi, wahudumu wenye kauli nzuri na huwa na karibu kila aina ya nafaka ninayoihitaji. Safari hii dukani hapo nilipita tu kuuliza bei ili nizunguke na maduka mengine mawili matatu kuhakikisha kweli kama bei zimeshuka kama watu wanavyodai au la.

Kweli baada ya kuzunguka maduka kadhaa niligundua mchele kupungua bei kulingana na madaraja(grades) husika tofauti na bei nilizozikuta siku chache zilizopita.  Mchele daraja la kwanza kabisa ule super badala ya shilingi mpaka elfu tatu ilivyokuwa zamani sasa mpaka shilingi elfu mbili na mia nne(2,400) unapata mchele kilo moja. Nilikuta pia mchele wa hali ya chini kabisa(chenga) uliokuwa umefikia mpaka shilingi elfu moja na miatano(1,500) kwa sasa unauzwa hadi shilingi elfu moja (1,000) mpaka 900 kwa kilo moja.


HATUUZI KABISA MCHELE KILO MOJA, MBILI WALA TATU , TUNAANZIA KILO TANO NA KUENDELEA…

Kauli hiyo hapo juu ndiyo iliyonifanya nipate wazo la kuandika makala hii ya leo. Baada ya kuamua ninunue mchele kilo 3 katika duka moja(siyo lile nililozoea kununua kila siku lakini) nilimuuliza mhudumu kijana wa kiume niliyemkuta nje ya duka hilo huku nikikunjua hela, “Nipimie mchele ule pale kilo tatu tafadhali”  Kwa mshangao kijana yule alinijibu pasipo kujali hata kidogo, “Mchele kilo 3 hapa hatuuzi, tunanzia kilo 5”


Kwa kuwa mazingira ya maduka ya nafaka pale mbezi karibu yote nayafahamu vilivyo, niliamua kumsisitizia tena yule kijana safari hii kwa ukali kidogo, “Nipimie mchele bwana, kwanini unataka kumrudisha tajiri yako kijijini hivihivi?” Kijana akijua fika kuwa bosi wake angeliweza kuyasikia malumbano yale akiwa mle ndani dukani, alijitahidi sana kushusha sauti chini na kurudia kunisihi; “Nakuambia kilo tatu hapa hatuuzi, mchele unaanzia kilo tano na kuendelea labda kajaribu kwingine” Na mimi kwa makusudi niliendelea kupaaza sauti juu kusudi yule mama(bosi wake) aweze kuyasikia malumbano yetu vizuri. Na kweli kumbe yule mama alikuwa akitusikia kila kitu tokea mwanzo akajitokeza akiwa amejawa na aibu. Alishuhudia nilivyokuwa nimegadhabishwa na yule mfanyikazi wake.

Ukweli ni kwamba maduka yote ya nafaka za jumla ya pale Mbezi nilikuwa nikijua fika kwamba unaponunua kilo kuanzia tano kushuka chini, na siyo mchele tu peke yake ni nafaka za aina zote, bei huongezeka shilingi mia moja, maana yake ni kwamba unakuwa umeuziwa kwa bei ya rejareja hata ununue kilo moja wanakuuzia hawawezi kumrudisha mteja hivihivi kiholela. Nilifahamu kabia kwamba majibu ya yule kijana aidha alikuwa amechoka au tu kilikuwa ni kiburi chake pengine alichozoea.


Sikumficha yule bosi, nikamwambia waziwazi, “Mama angu kwanini usifanye utaratibu wa kuwapa vijana wako angalao mafunzo ya msingi tu ya kutoa huduma nzuri kwa wateja?” Mama alicheka huku akinitaka radhi kwa kutamka, “Kakangu msamehe mdogo wako bure atajirekebisha” Kijana naye baada ya kuona mambo yameshaanza kumchachia, alijitahidi kuonyesha anajutia kosa alilofanya na chapchap akakimbia kwenda kunipimia mchele.

Sikumwacha hivihivi nikaendelea kumpa darasa, “Sasa wewe kijana kwanini ulitaka kumnyima bosi wako na wewe mwenyewe mapato? Hujui mimi mteja ndiye bosi wako namba moja niliyewaajiri bosi wako huyo na wewe pia? Nisiponunua unategemea aje nani kununua? Bosi wako namba 2 hawezi kwenda kukopa pesa aje akulipe wewe, ni lazima pesa za kukulipa zitokane na faida inayopatikana baada ya sisi wateja kuja kununua, hivyo mdogo wangu wajali sana wateja wanaokuja kununua hapa.”

Mwisho niliondoka pale dukani huku moyoni nikitamani sana mama yule japo angepata nakala ya kitabu changu cha; MAFANIKIO YA BIASHARA YA DUKA LA REJAREJA, kitabu kinachofundisha pamoja na mambo mengine mengi jinsi ya kumfanya mteja arudi tena na tena katika biashara yako bila kujali ni biashara ya jumla au ni ya rejareja, kauli ambazo hupaswi kabisa kumtamkia mteja na matendo ambayo mhudumu au wewe bosi unapoyafanya basi jiandae kumtafuta mchawi aliyekuloga ambapo  hautaweza kumpata japo utamaliza waganga wote nchini.


Ilikuwa kidogo tu nirudi kuja kumjulisha kuhusiana na kitabu hicho lakini nikafikiri angeweza kuona labda nilianzisha zogo lile pale kwa madhumuni ya kuuza vitabu vyangu, nikaghairi nikaamua kujiondokea zangu  mdogomdogo huku nikiwa mkononi nimeshikilia kifurushi changu cha mchele.

Kwa hakika kijana yule nisingelikuwa nazifahamu vyema desturi za maduka ya mchele ya jumla pale Mbezi mwisho, ni dhahiri kwamba ningeliondoka mapema sana kabla hata bosi wake hajajua ni nini kilichokuwa kikiendelea kule nje. Najiuliza ni wateja wangapi wanaojiondokea kwa kuambiwa kauli za namna ile?

Alichopaswa kunijibu yule kijana ni kunielewesha hivi kwa lugha ya upole; “Kaka hapa mchele unaponunua chini ya kilo tano, unalipa bei ya rejareja, na kuanzia kilo tano na kuendelea unalipa bei ya kawaida ya jumla” Hapo ningekuwa nimemuelewa na wala pasingekuwa na sababu ya malumbano yasiyokuwa na msingi.

.........................................................................

Kama hukuwa umewahi kusoma moja ya vitabu hivi hapa chini ni wakati wako sasa wa kuagiza nakala yako toka SELF HELP BOOKS TANZANIA

SIMU:       0712202244
WATSAP: 0765553030 
    10,000/=

   5,000/=

   3,000/=

1 Response to "KUSHUKA BEI YA MCHELE, KILO MOJA HATUUZI TUNAANZIA KILO TANO (5) TU NA KUENDELEA"